Na Ismail Ngayonga,MAELEZO
DAR ES SALAAM
UHARIBIFU wa mazingira
umeendelea kuathiri kila sekta ya uchumi na maisha ya Watanzania, ambapo
katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kasi ya upoteaji wa misitu
imezidi kuongeza kutokana na matumizi makubwa ya nishati itokanayo na
misitu.
Kutokana na uharibifu huo,
inaelezwa kuwa vyanzo vingi vya maji kwa sasa vimeharibiwa,
mvua
zimekuwa hazitabiriki, ukame umeongezeka, rutuba ya ardhi imepungua,
maporomoko ya ardhi katika maeneo ya milima yameongezeka, mafuriko
yanaharibu miundombinu na mali na kupoteza maisha ya watu.
Utafiti umebaini kuwa kila mvua
inapopungua kwa asilimia 10, pato la taifa linalotokana na kilimo
hupungua kwa asilimia 2 na makisio hayo ya kitaalamu yanaeleza pia joto
la dunia likiongezeka hadi kufikia nyuzijoto 2 za sentigredi juu ya
wastani, mavuno ya mahindi hupungua kwa asilimia 13 na mavuo ya mpunga
hupungua kwa asilimia 17.
Kwa msingi huo, Serikali ya Awamu
ya Tano kuanzia mwaka wa fedha 2016/17 imedhamiria kuyaweka masuala ya
mazingira kama sehemu ya mhimili wa ajenda ya uchumi na Maendeleo ya
Taifa.
Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano
na Mazingira inaratibu Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na
Kuongeza Uzalishaji wa Chakula (LDFS) unaotekelezwa katika nchi 12 za
Bara la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ikiwemo Tanzania, Kenya,
Malawi, Ethiopia, Uganda, Burundi, Swazland, NigerIa ,Ghana, Bukinafaso,
Niger na Senegal.
Mradi huo unatarajia kuipa
serikali fursa ya kutambua teknolojia na maeneo yanayofaa kwa uvunaji wa
mvua na maeneo ya vyanzo vya maji kupitia teknolojia itakayosaidia
kupunguza upotevu wa maji na kuongeza uzalishaji hasa kipindi cha
kiangazi.
Aidha wananchi na vikundi
mbalimbali vya wazalishaji wanatarajia kuwapatia mafunzo ya shamba
darasa wananchi kuhusu kilimo hifadhi na mbinu bora za kilimo rafiki
kwa mazingira, uboreshaji na urutubishaji wa udongo, mbinu za kilimo
misitu, kilimo cha makinga maji, kilimo cha mzunguko na usimamizi
shirikishi wa kudhibiti wadudu na magonjwa ya mazao.
Akiwasilisha Hotuba ya Makadirio
ya Bajeti ya mapato na matumizi kwa mwaka 2019/20, Waziri wa Nchi, Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Waziri Makamba
anasema Serikali inatekeleza mradi wa LDFS katika kipindi cha miaka
mitano kuanzia Julai, 2017 hadi Septemba, 2022 na kutekelezwa katika
maeneo yenye changamoto za ukame zilizopo katikati ya nchi na pwani.
Kwa mujibu wa Waziri Makamba
anasema mradi huo unaofadhiliwa na Mfuko wa Dunia wa Mazingira (GEF)
kupitia Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) utagharimu
kiasi cha dola za Marekani milioni 50 ambapo dola za Marekani milioni
7.156 zinatoka GEF na mchango wa nchi ni kiasi cha dola za Marekani milioni 42.94.
“Fedha zinazotolewa na GEF
zinalenga kuchangia katika kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, na
Hifadhi ya Bioanuai na Usimamizi Endelevu wa Ardhi na utatekelezwa
katika Kata ya Haubi katika Halmashauri ya Kondoa, Kata ya Sigili katika
Halmashauri ya Nzega, Kata ya Mpambala Halmashauri ya Mkalama, Kata ya
Sukuma, katika Halmashauri ya Magu na Shehia 8 katika Wilaya ya
Micheweni Kaskazini Pemba” anasema Waziri Makamba.
Akifafanua zaidi Waziri Makamba
anasema jumla ya Tsh. Bilioni 1.2 ziliidhinishwa katika mwaka 2018/19.
Hadi kufikia Machi, 2019 kiasi cha Tsh. Milioni 667.9 kilitumika
Tanzania Bara na kiasi cha Tsh. Milioni 158. 5 kwa upande wa Zanzibar.
Kwa ufupi hakuna sekta yoyote ya
kiuchumi na kijamii isiyoathiriwa na uharibifu wa mazingira, na kwa
msigi huo bila kuwekeza katika hifadhi ya mazingira, jitihada za
uwekezaji katika sekta nyingine za kiuchumi na kijamii hazitazaa matunda
tuliyoyatarajia.
No comments :
Post a Comment