Thursday, December 17, 2020

UJENZI WA KIVUKO CHA MV. CHATO II 'HAPA KAZI TU' WAKAMILIKA.



 

**********************************

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, amesema kuwa ujenzi wa kivuko cha MV. Chato II “hapa kazi tu” umekamilika kwa asilimia 99 na kinatarajiwa kuanza kutoa huduma kati ya Chato na Nkome, katika Ziwa Victoria.

Kasekenya amesema hayo mkoani Mwanza, mara baada ya  kukagua ujenzi wa kivuko hicho

ambao ulianza mwezi Februari mwaka huu na umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 3.1 na kuridhishwa na hatua ya ujenzi huo.

“Kivuko kimekamilika na kimefungwa vifaa vya kisasa na vinavyoendana na wakati, hivyo natoa rai kwa wananchi kutumia kivuko hiki kwani kina usalama wa kutosha”, amesisitiza Mhandisi Kasekenya.

Aidha, Naibu Waziri huyo ametoa siku tatu (3) kwa taasisi za Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) na Chuo Cha Bahari Dar es Saalaam (DMI) kuhakikisha  wanakagua kivuko hicho na kutoa vibali ili kianze kutoa huduma.

Naye Mkandarasi wa kivuko hicho, Major Songoro, ameishukuru Serikali kwa kuipa kazi kampuni hiyo na hivyo kuwajengea uwezo mkubwa katika ujenzi wa vivuko na meli nyingi hapa nchini kwa ajili ya kuboresha huduma za usafiri kwa wakazi wa maziwa makuu.

Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Umeme na Ufundi (TEMESA) Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Karonda Hassani, amesema kuwa kivuko hicho kinauwezo wa kuchukua abiria 200, magari 10 na mzigo wa tani 100 kwa wakati mmoja.

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi amefanya ziara ya kikazi katika mikoa ya Mwanza na Singida kwa ajili ya kukagua utekelezaji wa miradi inayoendelea na ile iliyopo katika hatua za awali za ujenzi ya sekta hizo.

 

No comments :

Post a Comment