Friday, November 13, 2020

TTB YAONGOZA WATALII WA NDANI KUTEMBELEA MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO


Wafanyakazi wa benki ya CRDB ambao ni watalii wa ndani wakishiriki burudani baada ya kuwasili katika ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Arusha kutoka jijini Dar es Salaam,watatembelea vivutio vya kitalii kwenye Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Baadhi ya wafanyakazi wa benki ya CRDB wakiwa katika picha ya pamoja mbele ya jengo la Mkuu wa mkoa wa Arusha kabla ya kuanza ziara ya kutembelea vivutio vya utalii .

Katibu Tawala mkoa wa Arusha,Richard Kwitega(kushoto) akiwapokea watalii wa ndani ambao ni wafanyakazi wa benki ya CRDB waliowasili kutoka jijini Dar es Salaam kutembelea vivutio vya kitalii.

Mkuu wa mkoa wa Arusha,Idd Kimanta(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa utalii pamoja na watalii wa ndani kutoka benki ya CRDB .

 Mkurugenzi wa Masoko wa Bodi ya Utalii(TTB),Mindi Kasiga(kushoto) akizungumza jambo na watalii wa ndani walitoka jijini Dar es Salaam kuanza ziara ya kitalii mkoa wa Arusha.

 

Mwandishi Wetu,Arusha

Mkuu wa mkoa wa Arusha,Idd Kimanta amesema Utalii wa Ndani ndio njia sahihi ya kuendeleza

sekta hiyo iliyoporomoka baada ya ulimwengu mzima kukumbwa na janga la ugonjwa wa Corona.

Janga hilo limeathiri kwa kiwango kikubwa mapato yanayotokana na sekta ya utalii baada ya shughuli nyingi za kiuchumi kufungwa ili kuepuka kusambaa zaidi ya ugonjwa huo ikiwemo baadhi ya viwanja vya ndege kufungwa.

Kimanta amesema hata baada ya mafanikio ya kukabiliana na janga hilo hapa nchini kufanikiwa,kiwango cha watalii  bado hakijafikia idadi ya watalii walioingia nchini mwaka 2019 waliofikia 1.9 milioni na kuingiza mapato yanayokadiriwa dola 2 bilioni.

“Katika kipindi cha janga hili kati ya hoteli 170 za kitalii tulizo nazo ambazo zilikua na wafanyakazi 250,000 takribani asilimia 70 zilifungwa na kusababisha wafanyakazi wengi kupewa likizo bila malipo,”amesema Kimanta

Ametoa wito kwa Chama cha Waendeshaji wa Utalii nchini (TATO) kuchangamkia soko la watalii wa ndani kwa kushusha gharama zinazoendana na kipato chao ili kuhakikisha sekta ya utalii inaendelea kuchochea uchumi .

“Nchi yetu ina watu takribani milioni 50 iwapo sekta ya utalii ikipata watalii milioni 4 kwa mwaka itaongeza hamasa kwa wananchi wetu kujenga tabia ya kutembelea vivutio vya utalii na kuongeza mapato ya serikali,”amesema 

Mkurugenzi wa Masoko wa Bodi ya Utalii walioandaa safari hiyo ya wafanyakazi 80 wa benki ya CRDB amesema wamekuja na ubunifu wenye lengo la kuendeleza sekta ya utalii na kuhamasisha watanzania zaidi kutembelea hifadhi za Taifa na maeneo mengine ya kitalii.

Amesema katika kiindi hiki cha kuelekea mwisho wa mwaka watakuja na mikakati itakayoongeza ushiriki wa wazawa kutembelea vivutio vya kitalii kwa wingi.

Naye kiongozi wa msafara kutoka CRDB,Shima Danford amesema wamepokea mapokezi mazuri tangu uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA) hadi jijini Arusha  wakiwa njiani kwenda Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kujionea vivutio mbalimbali.

mwisho

 

No comments :

Post a Comment