Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Idara
ya Uhamiaji Kamishna Msaidizi Mwandamizi Mohammed Bakar (kati kati) na
Mdhibiti wa Pasipoti Kamishna Msaidizi Dorah Luoga (kulia) wakiwa pamoja
na Mkurugenzi wa Airtel Money Isaack Nchunda wakionyesha bango baada ya
pamoja kusaidia ushirikiano ambapo kwa sasa Watanzania wataweza kulipia
pasipoti kwa kutumia Airtel Money.
Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Idara
ya Uhamiaji Kamishna Msaidizi Mwandamizi Mohammed Bakar akizungumza
wakati wa kuzindua ushirikiano baina ya Idara ya Uhamiaji na Airtel
ambapo kwa sasa Watanzania wataweza kulipia pasipoti kwa kutumia Airtel
Money. Kulia ni kuu wa Kitengo cha TEHAMA Idara ya Uhamiaji Kamishna
Msaidizi Mwandamizi Mohammed Bakar.
*******************************
Dar es Salaam Alhamisi 5 Machi 2020….Kampuni
ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania kwa kushirikiana na Idara ya
Uhamiaji nchini leo wametangaza kuzindua rasmi huduma ya
kulipia
gharama za pasi za kusafiria kwa kupitia huduma za “Airtel
Money”. Uzinduzi huo wa malipo ya ada za pasi za kusafiria kwa njia ya
“Airtel Money” ni muendelezo wa ushirikiano uliopo kati ya Kampuni ya
Airtel na Serikali katika kutumia mfumo wa kisasa wa kiteknolojia
kufanya malipo ya huduma na bidhaa mbali mbali njia ambayo ni salama,
haraka na nafuu.
Akizungumza
leo jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza huduma hiyo ya kulipia
huduma za Pasi za kusafiria kwa kutumia huduma ya Airtel Money, Mkuu
wa Kitengo cha TEHAMA Idara ya Uhamiaji, Kamishna Msaidizi Mohamed
Bakar alisema kuwa, hiyo ni moja ya njia rahisi ambayo itawafanya
Watanzania kulipia gharama za ada za pasi za kusafiria kwa urahisi zaidi
na popote walipo.
‘Kama
mnavyojua, fomu za maombi ya Pasipoti zinajazwa kwa njia ya mtandao.
Hii imekuwa ni njia rahisi sana kwani Mtanzania popote alipo haitaji
kutembelea ofisi za Uhamiaji ili kupata fomu ya Pasipoti, bali anaweza
kutembelea tovuti ya Idara ya Uhamiaji,. akajaza fomu yake na kuilipia
kwa njia ya mtandao na kisha kuiwasilisha fomu hiyo Ofisi ya Uhamiaji
kwa taratibu zinazofuata.
Kwa
sababu hiyo, leo ni siku nyingine muhimu kwetu kuweza kuungana na
wenzetu wa Airtel ili kurahishisha malipo ya ada za pasi za kusafiria,’
alisema Kamishna Bakar.
Serikali
ilishaweka mikakati ya kutumia njia ya kisasa katika kufanya malipo ya
huduma mbalimbali kwa haraka na usalama na kuzielekeza taasisi zake zote
kutumia Mfumo wa Serikali wa malipo kwa njia ya Mtandao GePG. Mfumo huu
umerahishisha sana malipo na umekuja na faida nyingi kama vile
kurahisisha malipo, kuimarisha utunzaji wa kumbukumbu, kupunguza upotevu
wa mapato ya Serikali, kuondoa mianya ya rushwa pamoja na kuongeza
mapato ya serikali. Kwa sababu hiyo, nachukua fursa hii kuwapongeza
Airtel kwa kuweza kuungana nasi ili kuwawezesha Watanzania kufanya
malipo ya pasi za kusafiria kwa kutumia Airtel Money. Natoa wito kwa
watanzania kutumia huduma hii ambayo kufanya malipo yao kwani ni salama
na rahisi kutumia, Kamishina Bakar aliongeza.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania Isack Nchunda alisema,
‘Kuunga mkono juhudi za Serikali imekuwa ni moja ya agenda kubwa kwetu.
Tunaelewa umuhimu wa Serikali wa kuhakikisha kuwa malipo yote ya kwenda
serikalini yanafanyika kwa mfumo wa GePG. Tutaendelea kushirikiana na
taasisi pamoja na mashirika mengine ya serikali kwa ajili ya kutoa
suluhisho ili kutimiza haya’.
Nchunda
alitoa wito kwa Watanzania kuendelea kutumia huduma za kielectroniki za
Airtel kwani zina ubunifu mkubwa pamoja na kuwa rafiki. “Ni muhimu kwa
Watanzania kuelewa kuwa Airtel inamilikiwa na Watanzania kupitia
serikali kwa asilimia 49. Na hii inamaanisha kuwa ukitumia huduma za
Airtel unatumia kilicho cha kwetu. Nia yetu ni kuendelea kutoa huduma
ambazo zinakidhi matakwa ya sasa ya kidigitali.
Nchunda aliongeza kuwa ili wateja waweze kukamilisha malipo ya huduma za pasi za kusafiria wafuate njia ifuatayo:
Piga namba ya Airtel Money *150*60# na chagua malipo ya Serikali-Namba 5
Weka namba ya kumbukumbu (ziko namba 12)
Weka kiasi cha malipo
Weka namba ya siri kuruhusu malipo
Mara
baada ya kukamilisha muamuala, mteja atapokea ujumbe mfupi wa maneno
kuthibitisha malipo yake. Risiti hiyo ya kielectroniki itakuwa ndio
uthibitisho wa malipo na ni rahisi kwa kuhifadhi au kwa kufuatilia kwa
baadae kwani haiwezi kupotea au kuharibika.
Airtel Money kwa
sasa imeunganisha kwa kulipia huduma za malipo zaidi ya 1,000 kwa watoa
huduma na vile vile mabenki pamoja na taasisi za kifedha zaidi ya 40
ambapo mteja anaweza kuweka au kutoa pesa zake akiwa popote. Airtel
Money pia inazidi kukua ambapo kwa sasa ina maduka ya Airtel Money na
matawi zaidi ya 1500 yanayotoa huduma mbalimbali pamoja na bidhaa za
Airtel.
No comments :
Post a Comment