Saturday, November 30, 2019

KIKAO CHA BASHE NA WADAU WA PAMBA KUONGEZA KASI YA USAMBAZAJI MBEGU ZA PAMBA KWA WAKULIMA




************************************
“Taasisi za fedha zaahidi kuongeza kasi ya malipo kwa wakulima ambao bado hawajalipwa”
Shinyanga,
Naibu Waziri wa Kilimo ndugu Hussein Bashe amefanya kikao na wadau zao la pamba kujadili
changamoto zinazolikabili zao hilo. Kikao hicho kilichofanyika mkoani Shinyanga katika ofisi za Bodi ya Pamba kiliwahusisha wanunuzi wakubwa wa pamba, taasisi za kifedha na wakuu mikoa, wilaya zinazolima pamba nchini.
Kikao hiki kimefanyika kufuatia malalamiko ya baadhi ya wakulima kucheleweshewa malipo ya fedha zao za msimu uliopta pia kukiwa na uhaba wa mbegu za pamba kwa wakulima wakati msimu wa kupanda ukiwa unaelekea ukingoni.
Akiongoza kikao hicho ndugu Bashe alisisitiza umuhimu wa wanunuzi wa pamba na taasisi za kifedha kufanya kazi kwa ukaribu ili kuhakikisha malipo yanafanyika mara moja kwa wakulima, ambapo baada ya majadiliano ya muda mrefu ilikubaliwa malipo yote yawe yamefanyika kufikia Disemba 8.
Pia wasambazaji wakuu wa mbegu kwa pamoja wamekubaliana kushirikiana kuhakikisha wakulima wanakopeshwa mbegu bora upesi katika maeneo wanayohudumia kwa kutumia mfumo wa wasambazaji hao kubadilishana mbegu ili kupunguza muda unaotumika kusafirisha mbegu hizo.
Wakuu wa mikoa na wilaya waliohudhuria kikao hicho walielezea wasiwasi wao juu ya baadhi ya vyama vya ushirika (AMCOS) kutowalipa wakulima, pamoja na kwamba vimekwisha lipwa fedha ambapo iliamuliwa vyama hivyo na wakulima wafungue akaunti katika mabenki ili utaratibu wa malipo kuanzia msimu ujao ufanyike kwa njia ya benki chini ya usimamizi wa wakuu wa wilaya.
Nao wawakilishi wa taasisi za kifedha walielezea namna walivyojipanga kuhakikisha malipo ya wakulima yanalipwa kupitia benki kwa kuhakikisha kila mkulima anafungua akaunti katika benki zao. Taasisi zilizohudhuria ilikuwa benki za NMB, CRDB, Azania, NBC na Benki ya Posta.
Naibu Waziri wa Kilimo Hussein Bashe alitumia fursa hiyo kuwafahamisha wafanyabiashara juu ya tamko la Rais John Pombe Magufuli kuwa Serikali haitoingilia kupanga bei ya mazao ya wakulima na badala yake itabaki kuwa msimamizi wa kuhakikisha mkulima anapata haki yake, ambapo aliwapa onyo wafanyabiashara kutotumia mwanya huo kujaribu kuwanyonya wakulima.

No comments :

Post a Comment