Saturday, November 30, 2019

WATAKAOAJIRI WATOTO CHINI YA MIAKA 18 KWENYE TUMBAKU KUKIONA CHA MOTO – MHE HASUNGA \

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akizungumza na waandishi wa habari tarehe 30 Novemba 2019 kwenye mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Kilimo Jijini Dar es salaam.
Na Mathias
Canal, Wizara ya Kilimo-Dar es salaam
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet
Hasunga (Mb) amesisitiza marufuku yake aliyoitoa hivi karibuni kuhusu ajira kwa
watoto ambao wapo chini ya miaka 18.
Mhe Hasunga amepiga
marufuku hiyo leo tarehe 30 Novemba 2019 wakati akizungumza kwenye mkutano na
waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Kilimo Jijini Dar es
salaam.
Alisema kuwa suala la ajira
kwa watoto ni miongoni mwa mambo yanazuiliwa kwenye Sheria za kimataifa kupitia
Shirika la Kazi Duniani (International Labour Organization) na Sheria za
Ajira hapa nchini hivyo mdau yeyote atakayebainika kukiukwa maelekezo hayo
atashtakiwa.
“Nawasihi wadau wote hususani
wakulima wa Tumbaku tuendelee kupiga vita ajira kwa watoto kwa kuwa ni eneo
ambalo limeendelea kulalamikiwa na wadau wengi” Alikaririwa Mhe Hasunga
Kadhalika, Mhe Hasunga
alisema kuwa katika kuhakikisha zao la tumbaku linaendelea kutoa mchango mkubwa
katika pato la mkulima na Taifa, Wizara imejiwekea malengo ya haraka
yanayopaswa kutekelezwa ambayo ni pamoja na usajili wa wakulima wote wa tumbaku,
kuwapatia vitambulisho na kuwaingiza kwenye kanzidata ili kupata takwimu za
uhakika za maeneo wanayolima na kuiwezesha serikali kusimamia upatikanaji wa
pembejeo kulingana na mahitaji yao.
Aidha, mipango mingine ni
kuhakikisha upatikanaji wa pembejeo kwa wakati kwa kuweka utaratibu wa
kumwezesha mkulima kujitegemea kwa pembejeo ili aache kuwa tegemezi wa mikopo
ya mabenki yenye riba kubwa.
Pamoja na malengo hayo ya
haraka, Wizara ya Kilimo inasimamia utekelezaji wa malengo ya muda mrefu
yakiwemo Upatikanaji wa wanunuzi wapya wa tumbaku kwa sasa na kwa miaka ijayo
kabla ya Juni, 2020, Kuongeza ubora wa zao la tumbaku kutoka asilimia 87 ya
sasa hadi asilimia 92 ifikapo Juni 2022 na Kuongeza mbegu mpya na bora za
tumbaku ili tuweze kupata masoko katika nchi nyingine kama vile China.
Alisema ili kufikia malengo
hayo wadau wote wa tasnia ya tumbaku wanapaswa kushirikiana ili kufikia malengo
hayo na wakulima kunufaika na jasho lao.
Tumbaku ni miongoni mwa
mazao makuu ya kimkakati ya yaliyopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Tano
chini ya uongozi wa Mhe Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania. Mazao mengine ni pamoja na Tumbaku,  Kahawa,
Pamba, Korosho, Chai, michikichi na alizeti.  
Mhe Hasunga alisema kuwa
Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa malengo ya uzalishaji yanafikiwa kwa
kuimarisha mifumo ya upatikanaji wa pembejeo kwa wakati, kuboresha huduma za
ugani na kutafuta masoko mapya ya tumbaku.
Waziri
Hasunga amesema kuwa katika msimu wa kilimo 2019/2020 ambao masoko yake
yataanza mwezi Mei 2020, kampuni za ununuzi zilizopo nchini ambazo ni Alliance
One Tanzania, Premium Active Tanzania na Japan Tobacco International zimetoa
mikataba ya kilo 42,225,985 na tayari wakulima wapatao 33,000 wameomba
kusajiliwa na Bodi ya Tumbaku kutokana na uzalishaji huo. Uzalishaji huo ni
mdogo na hivyo unaacha wakulima takribani 16,000 bila kulima tumbaku msimu huu.
 
Kutokana
na hali hiyo, Wizara ya Kilimo kupitia Bodi ya Tumbaku ilianzisha jitihada za
kutafuta masoko mengine ili kuziba pengo la kampuni ya Tanzania Leaf Tobacco –
TLTC ambayo haijatoa makisio ya uzalishaji msimu huu.
 
Jihada
hizo zimepelekea kupata kampuni nne (4) mpya ambazo zimeonesha nia ya kununua
tumbaku ya Tanzania msimu ujao . Kampuni hizo Kampuni za Zambia kupitia kampuni
ya kizawa ya MAGEFA GROWERS Ltd itanunua kilo 5,500,000, Kampuni ya TRANSAFRICQUE kupitia kampuni ya kizawa ya
GRAND TOBACCO GROWERS Co. Ltd imeomba kununua kilo 9,000,000, Kampuni ya PETROBENA
itanunua kilo 300,000, na Kampuni ya
PACHTEC
Limited imeomba kununua kilo 500,000
 
Takwimu zinaonesha kwamba
kwa kipindi cha zaidi ya miaka 10 hadi kufikia mwaka 2016 tumbaku imekuwa na
mchango mkubwa wa kuliingizia Taifa fedha za kigeni.  Kwa mfano
katika mwaka 2017, tumbaku iliingiza fedha za kigeni kiasi cha Dola za
Kimarekani Milioni 195.8 ikishika nafasi ya pili baada ya zao la korosho. Licha
ya faida kwa taifa, pia, uzalishaji wa tumbaku unawanufaisha wakulima,
wanunuzi, viwanda vya kusindika tumbaku, mabenki, wasambazaji wa pembejeo,
Halmashauri za wilaya na wadau wengine katika mnyororo wa thamani.

No comments :

Post a Comment