Wednesday, September 19, 2018

LUGOLA APIGA MARUFUKU WATUMISHI WIZARA YAKE KUNYANYASWA, AFUNGUA MILANGO KULETA KERO ZAO OFISINI KWAKE


PIX 3 (9)Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto), akimsalimia Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Jacob Kingu alipokua anawasili katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Veta, jijini Dodoma kwa ajili ya kuzungumza na watumishi wa wizara hiyo, leo. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Ramadhan Kailima. Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
PIX 1.Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akizungumza na watumishi wa Wizara yake, kuhusu masuala mbalimbali ya utendaji kazi. Pia Lugola aliwataka watumishi hao kufanya kazi kwa bidii na kuwataka baadhi ya viongozi wa wizara hiyo kuacha tabia ya kuwanyanyasa watumishi wao. Lugola alikutana na watumishi hao katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha Veta, jijini Dodoma, leo jana. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali, Jacob Kingu. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
PIX 2 (9)Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akizungumza na watumishi wa Wizara yake (hawapo pichani), kuhusu masuala mbalimbali ya utendaji kazi. Pia Lugola aliwataka watumishi hao kufanya kazi kwa bidii na kuwataka baadhi ya viongozi wa wizara hiyo kuacha tabia ya kuwanyanyasa watumishi wao. Lugola alikutana na watumishi hao katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha Veta, jijini Dodoma, leo jana. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali, Jacob Kingu, na kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Ramadhan Kailima. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
PIX 4 (5)Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akizungumza na watumishi wa Wizara yake, kuhusu masuala mbalimbali ya utendaji kazi. Pia Lugola aliwataka watumishi hao kufanya kazi kwa bidii na kuwataka baadhi ya viongozi wa wizara hiyo kuacha tabia ya kuwanyanyasa watumishi wao. Lugola alikutana na watumishi hao katika ukumbi wa
mikutano wa chuo cha Veta, jijini Dodoma, leo jana. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Na Felix Mwagara, MOHA
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka viongozi na watumishi mbalimbali wa wizara yake wafanye kazi kwa kushirikiana na kuacha tabia ya kunyanyasana wakati wanatekeleza majukumu yao ya kikazi.
Lugola pia amesema kila mtumishi wa wizara yake ana umuhimu mkubwa kwa kufanikisha mafanikio ya wizara hiyo kwakuwa watumishi hao wanafanya kazi kwa kutegemeana.
Akizungumza na watumishi wa makao makuu wa wizara hiyo katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Veta, jijini Dodoma jana, Lugola alisema kikao hicho alikiitisha kwa lengo la kujuana na watumishi hao pamoja na kujua changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi.
“Mambo muhimu ambayo yatatuletea mafanikio ndani ya wizara yetu ni kufanya kazi kwa bidii, kufanya kazi kwa kushirikiana na tukifanya hivyo hakika tutapendana na kuzidi kufanikiwa,” alisema Lugola.
Lugola aliongeza kuwa, hapendi kuona mtumishi yeyote ananyanyaswa kwa kutopewa haki zake au kucheleweshewa pasipo kuwa na sababu za msingi ikiwemo malipo mbalimbali ya watumishi wanayodai, na endapo yatatokea hayo watumishi hao wamletee kero zinazowakabili ofisini kwake na kwa kushirikiana na katibu mkuu wa wizara hiyo watazitatua.
“Utumishi wa umma naujua, na pia nimepitia manyanyaso kadhaa mpaka leo nimefikia hapa kutokana na historia yangu, kwanini tusipendane?, kwanini tunyanyasane?, kwanini tusishirikiane?, ni tabia mbaya na inatakiwa kulaaniwa kwa baadhi ya wakuu wa idara na vitengo pamoja na wengineo ambao wanatabia ya kunyanyasa watumishi waliochini yao,” alisema Lugola.
Mkutano huo ambao ni wa kwanza kwa Waziri Lugola, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Meja Jenerali, Jacob Kingu pamoja na Naibu Katibu Mkuu, Ramadhan Kailima, kuzungumza na watumishi wa Wizara hiyo tangu walipoteuliwa miezi kadhaa iliyopita, walitaka kujuana zaidi na watumishi wa wizara hiyo pamoja na kujua changamoto zao zinazowakabili.
Aidha, Katibu Mkuu, Meja Jenerali Kingu, kwa upande wake aliwataka watumishi wa wizara yake kupendana na kutengeneza umoja wa kusaidiana katika matukio mbalimbali yakiwemo ya furaha na matatizo.
“Anzisheni umoja, mpendane, mshirikiane katika matukio mbalimbali, wekeni utamaduni ya kuchangiana, hii itasaidia sana kufanya kazi kwa umoja na kupata mafanikio zaidi,” alisema Meja Jenerali Kingu.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Ramadhan Kailima alisema katika maisha yake anachukua unyanyasaji wa watumishi na wa aina yoyote, hivyo hatakubaliana na kiongozi yeyote atakaye mnyanyasa mtumishi.
“Tufanye kazi vizuri bila kunyanyasana, wanaojijua wanatabia hizo wajirekebishe tuweze kufanya kazi kwa upendo, anayedai haki zake apewe kwa mujibu wa utaratibu, sisi ni viongozi na moja ya kazi zetu ni kutokuaona mtumishi yeyote ananyanyaswa,” alisema Kailima.

No comments :

Post a Comment