Na Mwandishi Wetu
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya
Miundombinu, imeitaka serikali kufanya tathmini ya viwanja vya ndege
nchini, inavyojiendesha kwa faida na hasara, ili iweze kuvihudumia
vyema.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo,
Mhe. Hawa Mchafu ametoa kauli hiyo hivi karibuni wakati kamati hiyo
ilipofanya ziara kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius
Nyerere (JNIA), na kupata taarifa mbalimbali za uendeshaji.
Mhe. Hawa amesema tathmini hiyo
itasaidia kupunguza viwanja ambavyo ni mzigo kwa kuwa havizalishi
ipasavyo na kuwa tegemezi kwa vingine.
“Serikali ifanye tathmini upya ya
viwanja vya ndege ili iweze kuangalia vile vinavyozalisha na kuviwekea
mkazo hata ikiwezekana ivigawe kwa kanda,” amesema Mhe. Hawa.
Hata hivyo awali katika taarifa
yake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya
Ndege Tanzania
(TAA), Bw. Richard Mayongela ameiambia Kamati hiyo kuwa moja ya
changamoto TAA inakutana nayo ni pamoja na kujiendesha kwa taabu
kutokana na kuhudumia viwanja vingi visivyozalisha na kuwa tegemezi kwa
vingine vichache vinavyozalisha.
Bw. Mayongela amesema kati ya
viwanja vyote 58 vya ndege vingi ni tegemezi kwa zaidi ya asilimia 90,
ambapo mapato mengi yanatoka kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere (JNIA) na viwanja vichache vinavyozalisha.
Amesema changamoto nyingine ni
uchakavu wa miundombinu ya viwanja, maegesho ya ndege na ufinyu wa
majengo ya abiria katika viwanja vya ndege vya Dodoma, Mwanza, Mafia,
Arusha na Ziwa Manyara; kutokuwa na mfumo wa kuongozea ndege wakati wa
kutua na kuruka, ambapo husababisha viwanja vingi kutumika kwa saa 12
pekee kwa kushindwa kutua nyakati za usiku.
“Tatizo jingine ni uchakavu wa
magari ya zimamoto na uokoaji yaliyopo kwenye baadhi ya viwanja, hivyo
kunahatarisha usalama wa abiria na ndege; hali kadhalika wapo wananhi
wanaovamia maeneo ya viwanja nao husababisha tutumie gharama kubwa za
kuwaondoa,” amesema Bw. Mayongela.
Hata hivyo, Bw. Mayonbgela amesema
pamoja na TAA kukabiliwa na changamoto la kutokuwepo kwa uzio kwa
baadhi ya viwanja vya ndege, sasa wapo mbioni kujenga uzio kwenye
Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, ambapo itasaidia kupunguza wananchi na
mifugo kukatiza kwenye barabara ya kutua na kuruka kwa ndege.
Akizungumzia suala la uvamizi
Mweyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Suleiman Kakoso amewataka wananchi kuacha
kuvamia maeneo ya viwanja vya ndege ambavyo yapo halali kisheria.
“Viwanja vyote ni vya serikali na
hao wanaovamia wanaonekana, basi waondolewe kulingana na sheria kwani
wapo kwenye mikoa ambayo viwanja vipo,” amesema Mhe. Kakoso.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius
Kwandikwa amesema TAA inafanya jitihada ya kununua magari ya zimamoto na
kuboresha miundombinu mbalimbali ili kuviweka viwanja vyake katika hali
bora.
No comments :
Post a Comment