Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka
ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (aliyesimama)
akiikaribisha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kwenye Jengo la
Watu Mashuhuri (VIP) walipotembelea Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere (JNIA) hivi karibuni. Katikati ni Mwenyekiti wa kamati
hiyo, Mhe. Suleiman Kakoso na kushoto ni Naibu Waziri, Wizara ya Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa.
Naibu Waziri Wizara ya Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa
(aliyesimama) akieleza jambo fulani kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu ilipotembelea kwenye Kiwanja cha Ndege cha
Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) hivi karibuni. Katikati ni
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mhe Suleiman Kakoso na kulia ni Kaimu
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Bw. Richard
Mayongela.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu wakiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe Suleiman Kakoso
(wa tatu kulia), wakimsikiliza kwa makini Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela
(mwenye kipaza sauti) akielezea magari ya zimamoto na uokoaji, ambayo
yapo kwenye Kituo cha Zimamoto cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere (JNIA), wakati walipotembelea kituo hicho hivi karibuni.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu hivi karibuni wakiwa kwenye Ukumbi wa Watu
Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),
walipofanya ziara ya kupata taarifa mbalimbali za utekelezaji.
Kamanda wa Kituo cha Zimamoto na
Uokoaji cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),
Bw. Juma Yange (wa nne kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Askari
wa kituo hicho pamoja na mtaalam wa magari ya zimamoto, Bw. Roland Loitz
(wa tano kushoto) aliyetoka Kampuni ya Kimataifa ya Rosenbauer AG kwa
ajili ya kutoa mafunzo kwa
askari hao baada ya kuwasili kwa gari jipya.
……………..
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege
Tanzania (TAA), imekusanya sh. Bil 98,140,621,387.54 kutoka vyanzo vyake
mbalimbali vya mapato kwa mwaka 2016/2017, imeelezwa.
Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni
na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Richard Mayongela wakati akisoma
taarifa fupi ya uendeshaji wa viwanja vya ndege vinavyosimamiwa na
serikali kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge iliyofanya ziara kwenye Jengo la
Kwanza la abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere
(JNIA-TB1) na kituo cha Zimamoto cha kiwanja hicho.
Bw. Mayongela amesema chanzo
kikubwa cha mapato ni tozo ya Huduma za abiria, ambacho kimekuwa
kikiongezeka kila mwaka ambapo kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017
zilikusanywa Tsh. Bil. 66.5; wakati kwa mwaka zimekusanywa 2015/16 Bil.
67.3 na mwaka 2014/2015 zimekusanywa Tsh. Bil. 51.4.
Amesema pia TAA imekuwa ikikusanya
mapato kutoka vyanzo vingine vya mapato ambapo kwa mwaka 2016/2017
imekusanya Bil. 31.6 ambazo zimeongezeka kutoka Tsh. Bil. 20.3 kuanzia
mwaka 2012/2013 hadi 2014/2015.
Bw. Mayongela amesema pamoja na
kukusanya mapato mengi bado TAA imekuwa ikipewa kiasi kidogo cha
asilimia 40 ambacho kwa pamoja hakitoshelezi kwa matumizi mbalimbali
yakiwemo ya gharama za uendeshaji ambazo zinaongezeka kwa kasi.
“Mapato yanayozalishwa na TAA
yameongezeka kutoka sh. Bil 3.9 mwaka 1999/2000 hadi kufikia sh. Bil.
98.140 katika mwaka wa fedha 2016/2017, lakini kwa kuwekewa wigo
tumerejeshewa asilimia 40 tu, ambazo hazitoshelezi kutokana na gharama
za uendeshaji kupanda kwa kasi na kusababisha kuzorota kwa baadhi ya
huduma katika viwanja tunavyosimamia,” amesema Bw. Mayongela.
Bw. Mayongela ameiomba kamati ya
Miundombinu kuwasilisha maombi ya TAA katika Bunge kurejeshewa fedha za
tozo za abiria kwa asilimia 100, ambazo zamani zilikuwa zikisaidia
katika kuboresha miundombinu ya viwanja mbalimbali kwa kuwa baadhi ya
viwanja havizalishi na vinavyozalisha havizidi vitano kati ya 58
vilivyopo.
Akizungumzia hali ya biashara
katika viwanja vya ndege Bw. Mayongela amesema idadi ya safari za ndege
imeongezeka kwa asilimia 136 kutoka jumla ya safari 62,221 mwaka
1999/2000 na kufikia safari 147,057 mwaka 2016/2017, ambapo ongezeko
hilo ni kutokana na kuongezeka kwa mashirika mapya ya ndege na mengine
kuongeza idadi ya safari.
Mbali na safari za ndege pia idadi
ya wasafiri wa ndege wameongezeka kwa asilimia 301 kutoka jumla ya
abiria 846,906 mwaka 1999/2000 hadi kufikia 3,393,006 mwaka 2016/2017 na
ongezeko hilo limechangia kukua kwa shughuli za kiuchumi, hali
kadhalika tani za mizigo zimeongezeka kwa asilimia 21 kutoka tani 16,463
mwaka 1999/2000 hadi 19,995 mwaka 2016/2017.
Naye Mwenyekiti wa Kamati hiyo,
Mhe. Suleiman Kakoso ameipongeza TAA kwa kufanya kazi nzuri ya kukusanya
mapato mengi na kuongeza abiria, lakini amewataka wasibweteke na
wafanye kazi kwa bidii kwa kuwa wamekuwa na washindani hususan Kenya
ambao sasa wanafikisha abiria milioni tano kwa mwaka.
Hatahivyo, amemuomba Naibu Waziri
wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe.
Elias Kwandikwa kushirikiana na Waziri wa Wizara ya Fedha ili kurudisha
asilimia 100 ya mapato yanayotoka TAA ili waweze kujiendesha.
“Nakuomba Mhe. Waziri
ukashirikiane na Waziri wa Fedha muone ni namna gani mnaweza kurudisha
kwa TAA hiyo asilimia 100 ambazo zipo kisheria zinazopelekwa serikalini,
kwani viwanja vya ndege ndio vinavyokuza uchumi wa nchi, angalia
majirani zetu Kenya wanaweza kwa kuwa wameachiwa kila mapato wanayatumia
kwa matumizi ya uendeshaji,” amesema Mhe. Kakoso.
Kwa upande wake, Naibu Waziri,
Mhe. Kwandikwa amesema lengo la serikali ni kufanya maboresho katika
taasisi zake, lakini ameahidi kuwasilisha suala la kurejeshewa asilimia
100 ili waweze kujiendesha kwa kuwa wanachangia uchumi wa nchi.
No comments :
Post a Comment