Mtaalam wa Kuongoza ndege kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Anga Nchini (TCAA), Bw. Godwin Mutarubukwa (mwenye shati la blue),
akiwaonyesha Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu namna
ya kuongoza ndege kwa kutumia ramani, wakati kamati hiyo ilipotembelea
Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA).
Meneja wa Huduma za Ufundi wa
Kampuni ya Uendelezaji wa Kiwanja cha Ndege Kilimanjaro (KADCO),
Mhandisi Mathew Ndosi (wa tatu kushoto), akitoa maelezo kwa Wabunge wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu maboresho yaliyofanyika
katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA), wakati
kamati hiyo ilipotembelea kiwanja hicho, hivi karibuni.
Naibu Waziri wa Uchukuzi na
Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye (kushoto) akiteta na Mwenyekiti
wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mhe. Moshi Selemani Kakoso,
baada ya kamati hiyo kukagua Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Kilimanjaro (KIA).
Katibu Mkuu wa Sekta Uchukuzi,
Dkt. Leonard Chamuriho, akitoa ufafanuzi kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu
ya Bunge ya Miundombinu kuhusu juhudi za Serikali kuendeleza Kiwanja
cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) mara baada ya kamati hiyo
kutembelea Kiwanja hicho.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu, Mhe. Moshi Selemani Kakoso, akitoa maelekezo kwa
uongozi wa Kampuni ya Uendelezaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Kilimanjaro (KADCO), mara baada ya kutembelea na kukagua kiwanja hicho.
Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya KADCO, Bw. Gregory Teu.
………………..
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Miundombinu imeupongeza uongozi wa Kampuni ya Uendelezaji wa Kiwanja cha
Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KADCO), kwa usimamizi na
uendeshaji mzuri wa kiwanja hicho na kuwezesha kiwanja kuendelea kuwa
daraja la tisa kimataifa.
Akizungumza mara baada ya kukagua
maendeleo ya kiwanja hicho, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Moshi
Selemani Kakoso, amesema ongezeko la idadi ya watalii wanaoingia na
kutoka kiwanjani hapo ni sababu ya usimamizi mzuri na kusisitiza kampuni
hiyo kubuni
utaratibu mzuri wa kuongeza idadi ya mizigo.
“Niwapongeze sana uongozi na
watumishi wa KADCO kwa mabadiliko makubwa mliyoyafanya katika kiwanja
hiki kwani kwa muda mfupi baada ya miundombinu kuboreshwa mumeweza
kuongeza idadi ya ndege na kuongeza pato la kampuni” amesema Mhe.
Kakoso.
Aidha, Mhe. Kakoso ameitaka
Kampuni hiyo kuongeza fedha kwenye huduma ya jamii ili wananchi
wanaozunguka kiwanja hicho waweze kunufaika.
Ameongeza kuwa uboreshaji wa
miundombinu katika kiwanja hicho lazima uende sambamba na utoaji bora wa
huduma ili watalii mbalimbali wanaoingia na kutoka nchini wafurahie
huduma.
Kuhusu mgogoro wa wananchi
wanaozunguka kiwanja hicho, Katibu Mkuu wa Sekta ya Uchukuzi, Dr Lenard
Chamuriho amesema kuwa tayari mgogoro huo unaelekea ukingoni na muda
wowote kuanzia sasa utapatiwa ufumbuzi na kuliachia eneo husika.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi
wa KADCO, Bw. Gregory Teu amesema kuwa kwa sasa kampuni imejipanga
kuongeza wafanyakazi kulingana na mahitaji na kabla ya mwezi wa nane
wakurugenzi ambao hawajathibitishwa watadhibitishwa ili kuongeza tija
katika utendaji.
Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa
KADCO, Mhandisi Christopher Mukoma, amesema ukarabati wa kiwanja hicho
ulihusisha sehemu ya maegesho ya ndege, ukarabati na uboreshaji wa
mfumo wa maji safi na taka na uboreshaji wa jengo abiria umeongeza idadi
ya abiria kutoka laki tano kwa mwaka mpaka milioni 1.2 na kuweza
kuhudumia ndege 11 kutoka ndege 6 kwa wakati mmoja.
No comments :
Post a Comment