Mkurugenzi Msaidizi TEHAMA, Ofisi
ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Bw. Bartazal
Kibola akifungua mafunzo ya mfumo wa malipo (epicor 10.2) kwa Waweka
Hazina na Wahasibu (hawapo pichani) kutoka Halmashauri za Mikoa ya
Arusha na Manyara, leo Jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Idara ya Tawala za
Mikoa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)
Bibi Beatrice Kimoleta akitoa maelekezo ya mafunzo ya mfumo wa epicor
10.2 kwa Waweka Hazina na Wahasibu (hawapo pichani) kutoka Halmashauri
za Mikoa ya Arusha na Manyara, leo Jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa
mafunzo hayo yanayoendelea jijini humo.
Meneja wa Mradi wa Mifumo ya
Sekta za Umma (PS3) Mkoani Dodoma, Bw. Gideon Muganda akitoa maelekezo
kuhusu ushiriki wa PS3 katika mfumo wa malipo (epicor 10.2) wakati wa
ufunguzi wa mafunzo ya mfumo huo kwa Waweka Hazina na Wahasibu kutoka
Halmashauri za Mikoa ya Arusha na Manyara, leo Jijini Dodoma.
Waweka Hazina na Wahasibu kutoka
Halmashauri za Mikoa ya Arusha na Manyara wakimsikiliza mgeni rasmi
Mkurugenzi Msaidizi TEHAMA, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (TAMISEMI) Bw. Bartazal Kibola (aliyesimama) ambaye alifungua
mafunzo ya
mfumo wa malipo (epicor 10.2) kwa niaba ya Mkurugenzi wa
TEHAMA, Ofisi Rais TAMISEMI, leo Jijini. Waweka Hazina na Wahasibu
kutokana Mamlaka za zote za Serikali za Mitaa wanajengewa uwezo wa
kutumia mfumo huo utakaohusisha masuala yote ya fedha ikiwemo mapato,
matumizi pamoja na bajeti za Halmashauri husika. Mfumo huo utaanza
kutumika rasmi Julai 1, mwaka huu.
………………..
Na: Lilian Lundo – MAELEZO, Dodoma.
Waweka Hazina na Wahasibu kutoka
Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini wametakiwa kuzingatia matumizi
sahihi ya fedha zinazotumwa katika Halmashauri zao.
Hayo yameelezwa leo Jijini Dodoma
na Mkurugenzi Msaidizi TEHAMA, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa (TAMISEMI) Bw. Bartazal Kibola alipokuwa akifungua mafunzo ya
mfumo wa malipo (epicor 10.2) kwa Waweka Hazina na Wahasibu kutoka
Halmashauri za Mikoa ya Arusha na Manyara. Lengo la mafunzo hayo ni
kuwajengea uwezo Wahasibu hao namna ya kutumia mfumo huo ambao
umeboreshwa zaidi.
“Mfumo huu mpya utakapoanza
kutumika lazima sheria na taratibu zifuatwe, matumizi ya fedha yaendane
na bajeti ya Halmashauri husika, vilevile ni muhimu kuhakikisha kuwa
vifungu vyenu vya fedha vinakaa vizuri,” alisema Kibola.
Aliendelea kusema, mfumo huo
umerahisha kazi na kupunguza gharama ambapo mabadiliko yote ya bajeti
yatakuwa yakifanyika kupitia mfumo huo tofauti na ilivyokuwa awali
ambapo Halmashauri zililazimika kutuma barua za mabadiliko ya bajeti
ofisi za TAMISEMI.
Aidha, amesema mfumo huo utatatua
baadhi ya changamoto zilizokuwepo katika mfumo uliopita epicor toleo
Na. 9.05 ikiwa ni pamoja na changamoto ya kutoa taarifa za utekelezaji
mara baada ya kufanya matumizi kwa kuzingatia mipango iliyojiwekea
Halmashauri husika.
Hivyo basi epicor toleo namba 10.2
itaondoa kabisa tatizo la taarifa hizo kwani mfumo huo baada ya malipo
kufanyika utakuwa na uwezo wa kupeleka taarifa hizo kwenye mfumo wa
mipango na bajeti ambapo pia mfumo wa FFARS utakuwa umepokea taarifa
hizo za matumizi ya vituo na hivyo taarifa zote za utekelezaji
kupatikana moja kwa moja kutoka mfumo wa Plan Rep ambao pia
umeunganishwa na mfumo wa epicor 10.2.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa
Idara ya Tawala za Mikoa Ofisi ya Rais, TAMISEMI Bibi Beatrice Kimoleta
amewataka Wahasibu hao kuingiza takwimu sahihi katika mfumo huo ili
mfumo uweze kuongea taarifa ambazo ni sahihi.
Vile vile, ameshukuru Mradi wa
Uimarishaji wa Mifumo ya Sekta za Umma (Ps3) kupitia Shirika la
Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) kwa kuwezesha uboreshaji wa
mfumo huo ambao utaleta uwazi katika mapato na matumizi ya fedha za Umma
katika Halmashauri zote hapa nchini.
Mfumo wa malipo (epicor 10.2)
unatarajiwa kuanza kutumika katika Mamlaka zote za Serikali za Mitaa
nchini kuanzia Julai 1 mwaka huu. Mfumo huo utahusisha masuala yote ya
fedha za Mamlaka hizo ikiwa ni pamoja na mapato, matumizi pamoja na
bajeti nzima ya Mamlaka husika.
No comments :
Post a Comment