Monday, June 11, 2018

SEKRETARIETI YA MAADILI KUHAKIKI MALI ZA VIONGOZI WA UMMA


1
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Jaji Mstaafu Harod Nsekela akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Taasisi hiyo jengo la Sukari ghorofa ya Tatu jijini Dar es salaam , kuhusu Kazi ya uhakiki wa mali na madeni ya viongozi kazi ambayo  itajumuisha kuwafuata viongozi kwenye maeneo yao kuanzia tarehe 18/6/2018 hivyo kila kiongozi baada ya kupewa barua ya mali zake  atatakiwa kujiandaa kuhakikiwa.
02
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Jaji Mstaafu Harod Nsekela akisoma moja ya kifungu kinachotumika kuhakiki mali za viongozi mbele ya waandishi wa habari leo.
2
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Jaji Mstaafu Harod Nsekela akimsikiliza Afisa Habari wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Johanither Barongo alipokuwa akimkaribisha ili kuzungumza na waandishi wa habari leo.
3
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Jaji Mstaafu Harod Nsekela akiwa katika picha ya pamoja na John Kaole Katibu Viongozi wa Utumishi wa Umma Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kushoto na Waziri Kipacha Katibu Viongozi wa Siasa Sekretarieti ya maadili Viongozi wa Umma.
4
Baadhi ya viongozi wa Sekretarieti hiyo na waandishi wa habari wakiwa katika mkutano huo.
………………………………………………………………………………..
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Sekretarieti ya Maadili ya  Viongozi wa Umma ni Idara ya Serikali inayojitegema  ambayo imeanzishwa kwa Mujibu wa Ibara ya 132 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kusimamia mienendo na  tabia za Viongozi wa Umma ili kuhakikisha kuwa Viongozi hao  wanazingatia Masharti ya Sheria ya Maadili  ya Viongozi wa Umma Sura ya 398 ya Sheria za
Nchi.
Mojawapo ya kazi za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ni kupokea Matamko  ya Rasilimali na Madeni ya Viongozi wa Umma na Kuhakiki Mali zilizotajwa kwenye matamko hayo. Mamlaka hayo yametolewa na Vifungu 18 (2) (a) na 18 (2) (e)mtawalia vya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma pamoja na Sheria ya Marekebisho ya Sheria  mbalimbali  Na. 4 ya mwaka 2016.
Mtakumbuka kuwa tarehe 27/12/2017 tulikutana na kuwaeleza kuhusu urejeshaji wa Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni.Zoezi hilo lilifanikiwa kwa 98% ambapo viongozi waliotakiwa kurejesha fomu walikuwa 16,339.
Kama nilivyotangulia kuwaeleza baada ya urejeshaji kukamilika uchambuzi ulifanywa na kuchagua viongozi946 ambao mali zao zitafanyiwa uhakiki.  Lengo la Uhakiki huo ni kuthibitisha uhalisia wa mali hizo kulinganisha na
Tamko la Rasilimali na Madeni la Kiongozi, thamani halisi ya mali hizo na uhalali wa mali hizo kwa kuangalia namna mali hizo  zilivyopatikana.
Zoezi la Uhakiki litafanywa na Maafisa wa Sekretarieti ya Maadili.  Kila Kiongozi anayetakiwa kuhakikiwa ataandikiwa barua kwanza, ili aweze kujua rasilimali na madeni yake ambayo yatahakikiwa;Pili waandae nyaraka  mbalimbali za mali hizo na tatu ili waweze kuwaonyesha Maafisa wa Sekretarieti  mali hizo zilipo ili uthamini wa mali hizo  uweze kufanyika.  Kazi ya uhakiki itajumuisha kuwafuata viongozi kwenye maeneo yao kuanzia tarehe 18/6/2018 hivyo kila kiongozi baada ya kupewabarua ya kuhakikiwa mali zake  atatakiwa kujiandaa.
Lengo la barua  hiyo pia ni kuepusha watu wenye nia ovu kutumia uwepo wa zoezi la Uhakiki kutapeli viongozi kwa kuwatisha ili kujipatia manufaa mbalimbali ya kiuchumi.Viongozi watakaohusika na zoezi la kuhakikiwa wawatake maafisa wa Sekretarieti kuwaonyesha vitambulisho vyao.  Pia Kiongozi ambaye hataridhika na utambulisho huo anaweza kuwasiliana na Ofisi ya Sekretarieti ya Maadili kupitia Simu Na. 0222111810/11
Napenda kupitia kwenu kuwapa taarifa hii viongozi husika na wananchi kwa ujumla kuhusu kufanyika kwa uhakiki wa Rasilimali na Madeni ya Viongozi wa Umma.  Mahsusi kwa viongozi ambao hawakuwasilisha  nyaraka wanatakiwa kufanya hivyo wakati wa uhakiki.  Nyaraka zinazotakiwa kuwasilishwa ni Hati za Mikopo naHati za Miamala ya Benki ili kuthibitisha fedha zilizopo Benki na taasisi mbalimbali  za Fedha;
Kwa muhtasari nyaraka kwa kila rasilimali au madeni zinazotakiwa kuwasilisha ni kama ifuatavyo:-
  RASILIMALI/MADENI NYARAKA INAYOTAKIWA
  Ø Fedha zilizopo Benki / Taasisi nyingine za fedha. ·        Nyaraka zinazothibitisha taarifa za mikopo uliyochukua benki ·        “Bank Statement”.
  Ø Hisa na gawio ndani na nje ya Tanzania. ·        Hati ya umiliki wa hisa (Share certificate) idadi na thamani yake.
  Ø Nyumba na  majengo mengine ndani na nje ya tanzania. ·        Hati miliki/ Nyaraka za umiliki wa Viwanja, ·        Hati Miliki/ Nyaraka za umiliki wa Nyumba,
·        Mkataba wa Mauziano.
  Ø Mashamba, mifugo, madini ndani na nje ya Tanzania. ·        Nyaraka za umiliki wa Ardhi mfano Hati Miliki,  wa mauziano/ kukodi Ardhi n.k ·        Leseni ya utafiti, umiliki na uchimbaji Madini
·        Leseni na nyaraka za umiliki Kitalu/Vitalu vya Madini.
  Ø Mashine, viwanda na mitambo ndani na nje ya nchi. ·        Leseni ya biashara, cheti cha umiliki.
  Ø Magari na aina nyingine za usafiri, (boti, ndege,  ndani na nje Tanzania. ·        Hati ya usajili (kadi ya gari).
  Ø Rasilimali au maslahi mengine ya kibiashara ndani na nje yaTanzania. ·        Nyaraka zinazoonyesha umiliki wa kampuni (Memorandum and Articles of Association), Company Profile, Company Registration).
  Ø Madeni na mikopo unayodai au unayodaiwa. ·        Mkataba wa mikopo ·        Taarifa ya mkopo
·        Taarifa ya salio la makato ya mikopo.











Mwisho napenda kuwashukuru kwa kuitikia mwito, kufika kwenu kunadhihirisha umakini wenu katika kuisaidia Sekretarieti ya  Maadili ya Viongozi wa Umma kutekeleza majukumu  yake.  Kwa dhati napenda kuwashukuru kwa kutumia kalamu na Sauti zenu kuelimisha viongozi na jamii ya watanzania kuzingatia maadili katika kujenga uzalendo nchini.
Maadili ni Nidhamu,  Nidhamu inajenga Uwajibijkaji, Utu na Haki Kuelekea Uchumi wa Kati  wa Viwanda.
Jaji (Mst.) Harold R. Nsekela
KAMISHNA WA MAADILI

No comments :

Post a Comment