Wednesday, April 25, 2018

MIAKA 54 YA MUUNGANO NA KUSHAMIRI KWA MATUMIZI YA KISWAHILI DUNIANI


A
Na. Immaculate Makilika
Mapema wiki hii, tumeshuhudia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli  akihutubia  kikao cha Bunge la Afrika Mashariki kilichofanyika mjini Dodoma, akiomba Bunge la Afrika Mashariki (EALA), kutumia lugha adhimu ya Kiswahili wakati wa
uendeshaji wa vikao vyao katika kuenzi lugha hiyo kongwe na maarufu  ikikadiriwa kuwa ni tangu katika milenia ya kwanza tangu kuzaliwa kwa Yesu Kristo, yaani mnamo miaka ya 800 hadi 1000.
Ambapo Rais Magufuli anasema “nimefurahi kusikia Spika wa Bunge hili amesoma Tanzania, sekondari hadi chuo kikuu  na baada ya kumaliza hapa, ndipo akarudi nchini mwao Rwanda na nimefurahi kusikia Kiswahili kitaendelezwa katika bunge hili”.
Huku akiunga mkono kauli ya Spika wa Bunge hilo Dkt. Martin Ngoga kuwa wanahitaji kuendeleza matumizi ya Kiswahili katika Bunge lao.
Ambapo  kukipa hadhi zaidi Kiswahili katika nchi za Afrika Mashariki, Jumuiya hiyo ilianzisha Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki ikiwa ni sehemu  ya ufufuzi wa Kamati ya Taifa ya Lugha iliyoanzishwa na Wakoloni 1930 ili kuendeleza matumizi ya Kiswahili.

Tukumbuke kuwa lugha hii ya Kiswahili ambayo imekuwa ikizungumzwa nchini Tanganyika na Zanzibar tangu enzi za ukoloni, ilikuwa chachu ya kuchagiza nchi hizi mbili kuungana mnamo April 26, 1964.
Leo tunapoadhimisha miaka 54 ya Muungano wa Taifa la Tanzania, Kiswahili kimewakusanya na kuwajumuisha pamoja watu wa makabila zaidi ya 120 kikitumika kuwa lugha ya mawasiliano inayoeleweka na watu wote.  Hii si ajabu, ikizingatiwa kuwa, kwa asili yake, Kiswahili ni lugha unganishi, yaani yenye hulka ya kuunganisha na siyo kutenganisha au ya kibaguzi (Mazrui & Mazrui 1999) kama, kwa mfano, Kiafrikana.
Mazrui anayasema hayo katika kitabu maarufu cha Political Culture of Language: Swahili, Society and the State.
Ama kwa hakika Kiswahili kinavuka mipaka si tu imekuwa na sifa kuu ya kuunganisha watanzania, waafrika mashariki ila lugha hii adhimu imeendelea kusaambaa duniani kote.
Aidha Kiswahili kinatambulika kuwa lugha ya kazi katika Jumuiya za Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika, ambapo kwa kuzingatia hilo, Rais Mstaafu wa Msumbiji, Joachim Chisano alithibitisha  hili alipohutubia Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali za Umoja  wa Afrika kwa Kiswahili kwa mara ya kwanza alipokuwa akiaga AU Julai , 2004 Addis  Ababa, Ethiopia.
Waasisi wetu yaani Hayati Mwalimu Julius Nyerere pamoja na Hayati Abeid Aman Karume, walifanya mengi kwa kutumia lugha hii adhimu ya Kiswahili. Na kwa kutumia lugha hii adhimu wameweza kujenga umoja wa kitaifa na utamaduni wa kiafrika pamoja na kuushinda ubaguzi wa rangi, kutetea usalama wa Taifa katika vita dhidi ya Nduli Idi Amin Dada wa Uganda.
Leo tunapoadhimisha miaka hii 54 ya Muungano wetu mujarabu tunayo mengi ya kujivunia kwa hatua muhimu tu tunazoendelea kupitia, ambapo Kiswahili kimekuwa ni moja ya nyenzo muhimu.
Kiswahili kimekuwa mithili ya mhisopo (mmea wenye harufu nzuri), kama ambavyo tunashuhudia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameendelea kukienzi, kukikuza, kukieneza na kukipa heshima zaidi kwa kukitumia kikiwa lugha yake rasmi katika shughuli za kitaifa na kimataifa.
Mfano, Rais Magufuli amehutubia Kikao cha 17 cha Dharura cha Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) kilichofanyika jijini Dar es Salaam kwa kutumia lugha adhimu ya Kiswahili. Januari 29 mwaka 2017 Rais Magufuli amehudhuria mkutano wa 28 wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika  Mjini Addis Ababa, Ethiopia na kuhutubia kwa lugha aushi ya Kiswahili.
Halikadhalika, amehutubia kwa lugha ya Kiswahili katika ziara mbalimbali za viongozi wa Kimataifa hapa nchini kama ile ya Waziri Mkuu wa India, Narendra Modi aliyefanya ziara yake nchini Julai 11 mwaka 2016. Aidha, Katika azma hii Rais Magufuli amesisitiza kuwa “lengo la kutumia lugha hiyo ni kukikuza na kukitangaza Kiswahili kama lugha mama ya taifa.”
Huu ni muda muafaka Watanzania wanapotakiwa kukitazama Kiswahili zaidi ya sasa, nikimaanisha kwamba huenda katika  mwaka 2064  yaani katika maadhimisho ya miaka 100 ya Muungano kutakuwepo  na watu wengi wa aina ya Rais Magufuli ambao hawataona soni kuzungumza lugha hii adhimu katika mikutano mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Kwa kuangalia namna ambavyo lugha hii imeendelea kushika hatamu, Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) limeandaa mpango wa kuhakikisha lugha hiyo adhimu inakuwa bidhaa ya kimataifa na itakayounganisha watu wengi zaidi  duniani ikiwa ni pamoja na kutoa ajira kwa wapenzi na wadau wake.
Baraza limeweka mikakati ya kuchangamkia fursa zinazojitokeza za walimu wa Kiswahili katika nchi za nje ambapo Serikali kupitia BAKITA itaandaa mpango ambao utawezesha taifa kunufaika na utaalamu wa walimu hao kwa kiasi fulani cha mapato yao kurejeshwa katika mfuko wa taifa.
Katibu Mtendaji wa Bazara la Kiswahili la Taifa (BAKITA), Dkt. Selemani Sewanga anasema katika mahojiano maalum kuwa watanzania ni lazima wajivunie lugha hii adhimu kwa kuwa imeendelea kukua kwa kasi duniani na kuifanya kuwa si lugha ya Tanzania pekee, bali Afrika Mashariki lakini pia ni lugha ya 10 kwa kuwa na wazungumzaji wengi zaidi duniani ambapo inakadiriwa kuzungumzwa na watu takribani milioni 200 duniani kote.
Kutokana na umuhimu wa lugha hii, baadhi ya wageni mbalimbali wanaokuja nchini kwa ajili ya utalii au kufanya kazi wamekuwa wakifanya jitihada kujifunza Kiswahili.
“Ni lugha inayoendelea kukua kwa sababu ya asili yake na kumekuwepo shughuli za ukuaji wa uchumi ikiwemo uchimbaji gesi na madini mbalimbali, shughuli hizi zinasaidia wageni kujifunza lugha hii adhimu ili waweze kuwasiliana na wenyeji,” anasema Dkt. Sewange.
Hivi sasa kuna nchi mbalimbali duniani zimeanzisha programu ya somo la Kiswahili katika vyuo vyake vikuu au katika taasisi zake za lugha ya kigeni. Baadhi ya nchi hizo ni pamoja na Marekani, Uchina, Urusi, Italia, Ujerumani, Korea Kusini, na ufaransa.
Aidha, Kiswahili kinatumika katika idhaa mbalimbali za kimataifa kama vile Sauti ya Amerika, Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Redio Deusche Welle, Redio France International, China Redio International, Idhaa ya Kiswahili Redio Japan, Idhaa ya Kiswahili Redio Tehran, Idhaa ya Kiswahili Redio ya Umoja wa Mataifa, Redio Vatican, Redio India, Redio ya Korea Kusini na Redio Moscow International.
Kiswahili sasa kitafundishwa kama chanzo cha ajira tofauti na mtazamo uliokuwepo zamani. Hivi sasa wataalamu wa Kiswahili wanaandaliwa kwa kulenga soko mfano wanafundishwa tafsiri na ukalimani ili waweze kwenda kutoa huduma hiyo ndani na nje ya nchi.

Kushamiri huku kwa matumizi ya Kiswahili duniani kunategemea zaidi mipango madhubuti ambayo Serikali imeendelea kuweka kwa ustawi wake ikiwa pamoja na kuwa na kanzidata ya wataalamu wa Kiswahili nakupata taarifa sahihi za wataalamu wote nchini ili ile rahisi kuwasiliana nao pale zinapotokea fursa za ndani na nje ya nchi.

Licha ya kuwa Kiswahili ni lugha ya pili kwa kuwa na wazungumzaji wengi barani Afrika, juhudi zaidi zinahitajika kuikuza zaidi lugha hii. Katika kuadhimisha miaka 54 ya Muungano, huu ni wakati muafaka sasa wa kuhakikisha Kiswahili si tu kinaunganisha watanzania na waafrika lakini pia kiwe chachu ya maendeleo na kuitambulisha Tanzania kimataifa.

No comments :

Post a Comment