Monday, February 26, 2018

WATANZANIA KUPENYA SOKO LA KENYA


Pix 01
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Adolf Mkenda akifafanua jambo kwa washiriki wa kikao cha kujadili maandalizi ya wiki ya Tanzania nchini Kenya mapema hii leo jijini Dar es Salaam. Kuia ni Balozi wa Tanzania nchini Kenya Dk. Pindi Chana na katikati ni Mtendaji Mkuu wa TANTRADE Edwin Rutageruka.
Pix 02
Baadhi ya washiriki wa kikao cha kujadili maandalizi ya wiki ya Tanzania nchini Kenya wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Adolf Mkenda (hayupo pichani) wakati wa kikao hicho mapema hii leo jijini Dar es Salaam.
Picha na Eliphace Marwa – MAELEZO
…………………………………………………………………………………………
Jonas Kamaleki- MAELEZO
Serikali imetoa wito kwa  wafanyabiashara wa Tanzania kupeleka bidhaa zao katika soko la Kenya ili kupanua wigo wa masoko ya bidhaa zao.

Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Adolf Mkenda wakati wa kikao cha Maandalizi ya Wiki ya Tanzania nchini Kenya.
Prof. Mkenda alisema kuwa ni nia ya Serikali kuhakikisha watanzania wanapenya katika masoko ya kimataifa ili kuongeza pato la mtu binafsi na la Taifa kwa ujumla.
“Hali ya biashara kwa sasa ni nzuri sana, hivyo vikwazo visiwepo kabisa kati ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki”, alsiema Prof. Mwaikenda.
Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Balozi, Dkt. Pindi Chana amesema kuwa watanzania inabidi wathubutu na kuingia katika soko la Afrika Mashariki hususan soko la Kenya.
Amesema kuwa wafanyabiashara wa Kitanzania wasiogope kuingia katika masoko ya nje ya nchi, wajitahidi ili waweze kuongeza vipato kutokana na ukubwa wa soko lililopo nchini na Kenya kwa ujumla.
“Mkifanya biashara Kenya mtaongeza mitaji, ajira na kipato kwa ujumla kwani nchi hizi mbili zina zaidi ya watu milioni 90”, na hii inaendana na falsafa ya Mhe. Rais John Pombe Magufuli ya Uchumi wa Viwanda, hivyo hatuna budi kufuata maono ya Kiongozi wetu na kutengeneza na kuuza bidhaa za viwandani nje ya nchi”, alisema Balozi Pindi Chana.
Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Juma Ali Juma amesema wazo la kufungua soko la Kenya ni zuri na kumpongeza Balozi Pindi Chana kwa ubunifu huo.
Aliongeza kuwa anafahamu kuwa zipo changamoto ndogo ndogo katika masoko lakini zinafanyiwa kazi ili kuhakikisha biashara kati ya Tanzania na Kenya inaenda vizuri.
Bwana Juma alisisitza kuwa bidhaa zinazozalishwa nchini inabidi ziwe na ubora na kuwa na vifungashio bora ili kumvutia mteja kununua.

No comments :

Post a Comment