Saturday, November 25, 2017

WANAWAKE WATAKIWA KUSHIRIKI KATIKA MICHEZO.

Waziri wa Habari,Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akifyatua bastola juu leo Jijini Dar es Salaam kuashiria Ufunguzi wa Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan.
NA SHAMIMU NYAKI-WHUSM
WANAWAKE nchini wametakiwa kushiriki katika Michezo mbalimbali kwani ni fursa nzuri ambayo inasaidia kupata ajira na kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja pamoja na kuitangaza nchi kama ambavyo wanafanya wanamichezo wakiume.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe Dkt. Harrison Mwakyembe alipokuwa akizindua Mashindano ya Riadha kwa wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan ambapo amewataka wanawake waliopata fusa ya kushiriki katika mashindano hayo kujituma zaidi na kujiamini ili wapate nafasi ya kushiriki katika Olimpiki hiyo na kuiletea heshima Nchi yetu.
“Leo vitaibuka vipaji vingi vitakavyosaidia nchi yetu kupiga hatua katika mchezo wa Riadha,nawaasa mjitume zaidi muwe na nidhamu pamoja na kujiamini ili mfanye vizuri katika mashindano haya hatimaye mpate nafasi ya kushiriki Olimpki ya  mwaka 2020 kule nchini Japan”.Alisema Mhe. Mwakyembe.
Aidha amewataka waamuzi wa mchezo huo kutumia vizuri taaluma yao kwa kufuata Sheria,taratibu na kanuni walizofundishwa na kutii kiapo walichoapa katika kuchezesha mchezo huo kwa kutoa matokeo sahihi na kwa wakati ili kuepusha manung’uniko.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe.Juliana Shonza amesema Serikali ipo tayari kutoa ushirikiano kwa wanamichezo wote ambao wapo tayari na wanashiriki katika michezo mbalimbali kwani nia ya Serikali ni kukuza na kuendeleza Michezo hapa nchini.
“Ni fursa ya pekee kwenu vijana na wanawake kwa ujumla kutumia nafasi hii kuonyesha uwezo wenu katika michezo hii ili mpate nafasi ya kushiriki mashindano malimbali duniani na hatimaye mpate ajira itakayowezesha kutengeneza maisha yenu ya baadae.”Alisisitiza Mhe.Shonza.
Naye mwanariadha wa mbio za mita mia Bi. Winifrida Makenji kutoka Shule ya Sekondari Makongo ya Jijini Dar es Salaam ambaye ameingia katika fainali itakayochezwa hapo kesho amesema sifa kubwa ya yeye kufikia hatua hiyo ni kujiamini,kufanya mazoezi pamoja na kufuata maelekezo ya mwalimu.
Mashindano hayo yaliyofadhiliwa na Kampuni ya Ushirikiano ya Japan (jicA) yamehusisha michezo ya Riadha,kurusha mikuki pamoja na Kisahani ambapo yatamalizika kesho katika Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Habari Sanaa na Michezo Mhe.Juliana Shonza akizungumza leo Jijini Dar es Salaam katika Ufunguzi  wa Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan.Kulia ni Waziri wa Wizara hiyo  Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe.

Waziri wa Habari,Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akimpongeza mshindi wa kurusha kisahani Bi. Mwanjala Abdala kutoka Dodoma wakati wa Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Habari Sanaa na Michezo Mhe.Juliana Shonza akimvalisha Medali ya ushindi mshindi namba mbili wa kurusha kisahani leo Jijini Dar es Salaam katika Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan.Kulia ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa Bw. Mohamed Kiganja.

Waziri Mhe.Dkt Mwakyembe na Naibu Waziri Mhe.Juliana Shonza wa Wizara ya Habari Sanaa na Michezo wakimvalisha medali ya ushindi mshindi namba moja wa kurusha kisahani Bi.Joyce Barnabas kutoka Dodoma leo Jijini Dar es Salaam katika Ufunguzi wa Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo nchini Japan.


Waziri Mhe.Dkt Mwakyembe na Naibu Waziri Mhe.Juliana Shonza wa Wizara ya Habari Sanaa na Michezo wakiwa katika picha ya pamoja na wanamichezo pamoja na wafadhili kutoka kampuni ya jiCA ya nchini Japan wanaoshiriki Mashindano ya Riadha kwa Wanawake kuelekea Olimpiki ya mwaka 2020 yatakayofanyika Tokyo Nchini Japan yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.Wa pili kushoto waliokaa ni Balozi wa Japan hapa nchini Mhe.Masahran Yoshida.
NA ISMAIL NGAYONGAMAELEZO
WAFANYABIASHARA na Wajasiriamali Wanawake nchini wametakiwa kuwa na uthubutu wa kutenda na kufikia malengo waliyojiwekea kwa kutumia fursa zilizopo ili kujiletea maendeleo ya kiuchumi katika jamii inayowazunguka.
Wito huo huo umetolewa (juzi) Novemba 23, 2017 Jijini Dar es Salaam na Afisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Mwajuma Magwiza wakati wa mkutano wa Jukwaa la Mwanamke Mjasiriamali na Ubunifu liliondaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect.
Magwiza alisema Wanawake ndio kundi kubwa katika jamii ya Watanzania na wanapaswa kutambua kuwa hakuna njia ya mkato katika kuyafikia mafanikio yao kiuchumi na badala yake wajihangaishe katika kutatua changamoto zilizopo ili kupata mafanikio katika shughuli mbalimbali za kila ikiwemo biashara na ujasiriamali..
“Serikali imefungua milango ya ushirikiano kwa kuanisha fursa za kujikwamua kiuchumi kwa Wafanyabiashara na Wajasiriamali wanawake, zipo taratibu zilizoanishwa katika kuzifikia fursa hizo na hivyo ni wajibu wetu kuachana na mazoea ya utamaduni ulijiongezeka katika jamii yetu” alisema Magwiza.
Kwa mujibu wa Magwiza alisema Serikali inatambua changamoto mbalimbali zinazowakabili Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake nchini ikiwemo ukosefu wa mtaji ya biasharara, ambapo hata hivyo halmashauri mbalimbali nchini zimeanza kutekeleza maelekezo ya Serikali ya kutenga asilimia 5 ya bajeti zao kwa ajili ya kusaidia vikundi vya Wanawake na Vijana.
Aidha Magwiza aliwataka Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake kutambua kuwa mtaji sio kigezo cha kukwama katika kujiletea maendeleo yao na badala yake watumie majukwaa yao kuwa chachu ya mabadiliko ya kifikra na hatimaye kufikia malengo waliyojiwekea.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya GIBR FARM, Hadija Jabir alisema safari ya mabadiliko ya kiuchumi kwa Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake nchini itapata mafanikio makubwa iwapo jamii hiyo itaunganisha nguvu ya pamoja katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowazunguka.
Aliongeza kuwa ili mafanikio hayo yaweze kupatikana ni wajibu wa Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake walielezane ukweli na uwazi uliopo katika kubaini fursa na kutumia rasilimali zilizopo ili ziweze kuwaletea maendeleo ya haraka.
“Safari ya kujikwamua kiuchumi huwa ngumu katika ngazi za awali, kwa upande wetu kampuni ya GIBR FARM inayojihusisha na uzalishaji wa mbogamboga na matunda, tumefanikiwa kupanua wigo wa soko na sasa tunauza bidhaa zetu katika nchi za Sweden, Italy na Ujerumani” alisema Hadija.
Naye Mwanzilishi wa Kampuni ya uzalishaji kuku ya GOKUKUZ, Bulla Boma alisema kumekuwepo na changamoto ya fursa za masoko katika mauzo ya bidhaa kwa Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake hususani waliopo katika mfumo usio rasmi, hatua inayowafanya wengi wao kukatishwa tamaa wakiwa katika ngazi za awali.
Hata hivyo alisema kutokana na kupanua wigo wa ushirikano na mawasiliano na Wafanyabishara na Wajasiriamali wakubwa waliopo nchini, kampuni yake kwa sasa imejiwekea malengo ya kupanua wigo wa bidhaa hiyo katika soko la kimataifa.
Kongamano hilo lilibeba kauli mbiu ya “Mwanamke Mjasiriamali na Ubunifu” lililenga katika kuhamasisha Wafanyabiashara na Wajasiriamali wanawake nchini kuibua na kutumia fursa za kiuchumi ili kuweza kuwaletea maendeleo yao katika jamii.
 
Mmoja wa wawezeshaji wa mkutano wa jukwaa la Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wanawake ulioandaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect akizungumza na wajumbe wa jukwaa lililofanyika Novemba 23, 2017 Jijini Dar es Salaam. Mkutano huo ulilenga kuwajengea uwezo Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake kukabiliana na changamoto mbali katika fursa za kiuchumi.


Baadhi ya Wafanyabiashara na Wajasirimali Wanawake wakifuatilia mkutano wa jukwaa la Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wanawake ulioandaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect lililolenga kuwajengea uwezo na Wajasiriamali wa kukabiliana na changamoto mbali katika fursa za kiuchumi. Mkutano huo ulifanyika Novemba 23 2017
 

Baadhi ya Wafanyabiashara na Wajasirimali Wanawake wakifuatilia mkutano wa jukwaa la Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wanawake ulioandaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect lililolenga kuwajengea uwezo na Wajasiriamali wa kukabiliana na changamoto mbali katika fursa za kiuchumi. Mkutano huo ulifanyika Novemba 23 2017.


Mwanzilishi wa Tamasha la Nyamachoma, Carol Ndosi akizungumza na Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wanawake wakati wa mkutano wa jukwaa la Wafanyabiashara Wanawake lililoandaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect lililofanyika Novemba 23, 2017 Jijini Dar es Salaam. Mkutano huo ulilenga kuwajengea uwezo Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake kukabiliana na changamoto mbali katika fursa za kiuchumi.


Afisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni Mwajuma Magwiza akuzungumza na Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wanawake wakati wa mkutano wa jukwaa la Wafanyabiashara Wanawake lililoandaliwa na Taasisi ya Dominion Leadership Connect lililofanyika jana Novemba 23, 2017 Jijini Dar es Salaam. Mkutano huo ulilenga kuwajengea uwezo Wafanyabiashara na Wajasiriamali Wanawake kukabiliana na changamoto mbali katika fursa za kiuchumi.(PICHA NA MPIGA PICHA WETU)

No comments :

Post a Comment