Friday, September 22, 2017

TCRA: Blogu na Online Tv Zitumike katika Ujenzi wa Taifa


DSC_0023
Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka ya Mawasiliano nchini James Kilaba (katikati) akiandika maoni ya wadau wa mitandao ya blogu na Online Tv wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kusisitiza matumizi bora ya mitandao ya kijamii kwa awamu ya pili mapema hii leo jijini Dar es Salaam.
…………….
Na. Paschal Dotto-MAELEZO.
22/09/2017
Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Mamlaka ya Mawasiliano nchini(TCRA) imetia nia kuboresha mawasiliano kwa umma hasa katika matumizi ya mitandao ya kijamii ili kuwawezesha watanzania kupata elimu bora ya...
maendeleo na kujenga uchumi uliobora.
Haya yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Bodi wa Mamlaka hiyo Dkt. Jonas Kilimbe  alipokua akihutubia hadhara ya wamiliki wa vyombo vya habari mtandaoni (blogu na Online TV) katika uzinduzi wa kampeni ya awamu ya pili ya “kusisitiza matumizi bora ya mitandao ya kijamii”  iliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.
Katika hafla hiyo, Dkt. Kilimbe alisema kuwa kwa sasa teknolojia ya mtandao inakua kwa kasi kwa hiyo huduma za habari zinapatikana kila sehemu kwa njia ya mtandao na kufanya matumizi ya mitandao kuwa makubwa.
“Sekta ya mawasiliano kwa umma imepiga hatua kubwa sana duniani kwa sasa, kwa kiasi kikubwa mtandao unachangia kuwepo kwa habari nyingi. Tanzania inajumla ya televisheni za mitadaoni zipatazo 50 pamoja na blogu 150 ambazo zote zinatoa taarifa kwa wananchi, hii inaashiria kuwa mawasiliano kwa umma yamehamia zaidi kwenye mtandao”, alisema Dkt.Kilimbe.
Aidha Dkt.Kilimbe alisema kuwa sekta hii inapaswa kuangaliwa zaidi kwani ni sekta muhimu kwa ujenzi wa Taifa na kuwaasa vijana kutumia vizuri teknolojia hiyo kwa kujielimisha kuhusiana na masuala ya maendeleo kuliko kutumia vibaya mitandao hiyo.
“Tuna jukumu zito na ni kubwa kwa sababu sekta hii ya mawasiliano imeshikiria kila kitu na tasnia ya habari ina nguvu kubwa sana kwa kuleta elimu ya maendeleo kwa wananchi kwa hiyo waandishi mitandaoni tumieni weledi  mkubwa kwa habari za maendeleo.”, alisisitiza Dkt. Kilimbe.
Dkt.Kilimbe alisema kuwa katika matumizi ya teknolojia hii mpya yanapaswa kuzingatiwa  kwa ajili ya ujenzi wa taifa hasa kwa wale wanaotumia vizuri mitandao ya kijamii inawapa elimu kubwa ya maendeleo.
Aidha Dkt. Kilimbe amekishukuru chama cha wamiliki wa blogu na televisheni mtandaoni(TBN) kwa kuleta umoja na kuzingatia maadili na weledi wa umilikajia wa vyombo hivyo kwa kuwahabarisha wananchi.
Naye mtoa mada na mwakilishi kutoka TCRA Bw. Thadeus Lingo alisisitiza usalama wa matumizi ya mtandao akisema kuwa idadi ya watumiaji wa mitandao imeongezeka duniani kuanzia Julai 1, 2017 na kufikia bilioni 3.8 huku kati ya hao bilioni 3.4 ambayo ni sawa na asilimia 92 ni watumiajia wa mitandao ya kijamii hali iliyosababisha kuongezeka kwa vyombo vya habari kuhamia mtandaoni, kwa hiyo weledi unahitajika katika kuhabarisha umma kwa njia hii.

No comments :

Post a Comment