Friday, September 29, 2017

SERIKALI YAAPA KUZIWAJIBISHA TAASISI ZILIZOBAINIKA NA MADUDU KTK UKAGUZI WA UNUNUZI WA UMMA


Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Phillip Mpango akipokea Ripoti ya Tathmini ya Utendaji kwa mwaka wa fedha 2016/17 kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya PPRA, Balozi, Dkt. Matern Lumbanga leo Septemba 28, 29, 2017 mjini Dodoma.
WAZIRI wa Fedha na Mipango Dkt. Phillip Mpango amesema serikali itaziwajibisha taasisi zote zilizobainika kufanya vibaya katika manunuzi yake ya mwaka 2016/17 kwa mujibu wa sheria ikiwa ni pamoja na wote waliohusika kufikishwa mbele ya vyombo vya dola ikiwemo Takukuru kwa uchunguzi zaidi.
Dkt. Mpango amesema hayo leo mjini Dodoma mara baada ya kupokea Ripoti ya Tathmini ya Utendaji ya PPRA kwa mwaka wa fedha 2016/17 ambayo pamoja na mambo mengine muhimu, inajumuisha matokeo ya ukaguzi wa manunuzi yaliyofanywa na taasisi za umma katika mwaka husika. Ukaguzi huo ulihusisha Taasisi za Umma 112.
Ripoti hiyo inaonesha baadhi ya taasisi kufanya malipo yenye utata/hewa ambazo ni pamoja na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) na Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba ambapo kiasi cha shilingi milioni 483.44 zililipwa kwa wakandarasi kwa kazi ambazo hazikuwa zimefanyika.
Aidha, Ripoti hiyo imeonesha kuwepo kwa taasisi sita zilizofanyiwa uchunguzi na kubainika kuisababishia Serikali hasara kubwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo; ucheleweshaji wa malipo kwa wakandarasi uliosababisha ongezeko la riba, pamoja na faini zilizotokana na ukiukwaji wa taratibu za kijamii na mazingira kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa kazi za ujenzi. Taasisi hizo ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Taasisi ya Mifupa (MOI), Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Shirika la Bima la Taifa (NIC), Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano (TCRA), Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA), Wizara ya Fedha na Mipango, pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa.
“Naahidi kuyafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na Ripoti hii na ni lazima tuhakikishe kuwa fedha za umma zinalindwa kwa nguvu zote. Kila mtu aliyehusika kuisababishia Serikali hasara ni lazima atawajibika na sheria lazima isimamiwe kwa ukamilifu,” alisema Waziri.
Pia, Waziri Mpango aliongeza kuwa kwa zile taasisi zilizobainika kuwa na viashiria vya rushwa wahusika wote watajieleza na pia watawasilishwa Takukuru kwa uchunguzi zaidi na mamlaka za uteuzi na baada ya hapo hatua stahiki zitachukuliwa dhidi yao.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurungezi ya PPRA, Dkt. Balozi Matern Lumbanga alisema kuwa ripoti imejumuisha matokeo ya ukaguzi uliofanywa na PPRA kwa taasisi nunuzi ili kupima kiwango cha uzingatiaji sheria na pia upatikanaji wa thamani ya fedha ambapo jumla ya taasisi nunuzi 112 zilifanyiwa ukaguzi huu.
Aidha, Balozi Lumbanga aliongeza kuwa matokeo ya ukaguzi wa uzingatiaji sheria yanaonesha kuwa wastani wa uzingatiaji kwa taasisi zilizokaguliwa ni asilimia 74 ambayo ni ongezeko la asilimia moja ikilinganishwa na wastani wa mwaka uliopita ambao ulikuwa asilimia 73.
Kwa upande mwingine, taasisi 81 kati ya 112 zilifanyiwa ukaguzi wa kupima thamani halisi ya fedha. Jumla ya mikataba ya miradi 345 ilikaguliwa ambapo miradi 87 ilipata alama za kiwango cha kati/kawaida, na saba ilipata alama za kiwango kisichoridhisha.
“Miradi iliyopata kiwango kisichoridhisha inajumuisha miwili ya ujenzi wa majengo yenye thamani ya shilingi 201.542 milioni, mradi mmoja wa ujenzi wa barabara wenye thamani ya shilingi 146.92 milioni, miradi miwili ya ujenzi yenye thamani ya shilingi 405.63 milioni. Mingine ni mmoja wa huduma za ushauri wa kitaalam wenye thamani ya shilingi 25.46 milioni, na mradi mmoja wa usambazaji wa maji wenye thamani ya shilingi 1.59 bilioni” alisema Balozi Lumbanga.
Kuhusu viashiria vya rushwa, PPRA pia ulipima uwezekano wa uwepo wa rushwa katika taasisi au miradi husika. Tathmini ya jumla ya viashiria vya rushwa ilionesha kwamba miradi 33  katika taasisi 17 ilibainika kuwa na kiwango kikubwa cha viashiria vya rushwa ikimaanisha kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa uwepo wa vitendo vya rushwa katika taasisi na miradi hiyo.
Taasisi hizo ni Mamlaka za Maji Safi na Maji Taka za Moshi (Muwasa), Mwanza (Mwauwasa) na Arusha (Auwasa); pamoja na Halmashauri za Wilaya za Msalala, Kibondo na Moshi. Taasisi nyingine ni Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Chuo cha Ufundi Arusha, Halmashauri ya Mji wa Kahama, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Taasisi ya Uhasibu Arusha (IAA), Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Halmashauri ya Mji wa Masasi, pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Ripoti hii ni ya 11 tangu PPRA ilipoanzishwa. Ripoti hii inatoa tathmini ya utendaji ambapo imeelezea kwa kina kazi mbalimbali zilizotekelezwa na PPRA katika kusimamia shughuli za ununuzi wa umma katika mwaka wa fedha 2016/17 ambapo pamoja na mambo mengine, ni pamoja na Ujengaji uwezo kwa taasisi nunuzi, Usimamizi wa mifumo ya habari za ununuzi, Utoaji huduma za ushauri katika ununuzi na pia kusimamia Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410.

Waziri wa Fedha Dkt. Phillip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya PPRA mjini Dodoma leo.


Waziri wa Fedha Dkt. Phillip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya PPRA.


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya PPRA, Balozi, Dkt. Matern Lumbanga akitoa maelezo mafupi kuhusu Ripoti ya Tathmini ya Utendaji kwa Mwaka wa fedha 2016/17 kwa Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Phillip Mpango mjini Dodoma leo. Kulia kwake ni Mjumbe wa Bodi ya PPRA, Prof. Sufian Bukurura pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa PPRA, Dkt. Laurent Shirima.


No comments :

Post a Comment