Jovina Bujulu-MAELEZO
Mnamo Aprili 26, 1964, nchi mbili
za Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Zanzibar ziliungana na
kuzaa taifa jipya la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo mwaka huu
linatimiza miaka 53.
Juhudi za kuunganisha nchi hizo
mbili zilitokana na makubaliano ya waasisi wa taifa ambao ni
Hayati Baba
wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati
Mzee Abeid Amani Karume. Lengo la kuunganisha nchi hizo mbili lilikuwa
ni kuwa na taifa moja lenye nguvu kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Muungano huu umedumu kama taifa
moja lenye amani, umoja, utulivu na mshikamano kwa miaka 53, jambo
ambalo baadhi ya nchi nyingine duniani limewashinda. Mfano wa Nchi hizo
ni Senegal na Gambia na Misri na Syria. Hivyo Muungano wetu ni wa pekee
na mfano wa kuigwa katika bara la Afrika na duniani pote.
Ili kuhakikisha kuwa historia na
masuala yote yanayohusu Muungano yanahifadhiwa na kufahamika kwa
wananchi wa pande zote za Muungano, Idara ya Muungano iliyo chini ya
Ofisi ya Makamu wa Rais ilianzisha “Programu ya kutoa elimu kwa umma
kuhusu Muungano” ambayo ilianzishwa mwaka 2014.
Akiongea katika mahojiano maalum
kuhusu Muungano, Mkurugenzi wa Muungano kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais,
ndugu Baraka Rajab Baraka, anasema kuwa madhumuni ya kuanzisha programu
hiyo ni kuhakikisha kuwa historia ya tulikotoka, tulipo na tuendako,
umuhimu na faida ya Muungano inajulikana kwa Watanzania walio wengi, na
pia elimu ya uraia na uzalendo inatolewa kwa wanafunzi wa sekondari na
vyuo nchini ili kuwajengea uelewa mpana kuhusu Muungano wa huo.
“Miongoni mwa majukumu ya Idara ya
Muungano ni pamoja na kuhakikisha kuwa umma unakuwa na uelewa wa
kutosha kuhusu Muungano pamoja na kuondoa kabisa taswira mbaya kuhusu
Muungano na kuwasaidia wanafunzi kuwa na uzalendo na kuwa raia wema kwa
nchi yao na kutambua kuwa amani iliyopo nchini ni moja ya manufaa ya
Muungano”, alisema ndugu Baraka.
Aliongeza kuwa Ilani ya Uchaguzi
ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020 imeweka msisitizo zaidi wa
kutoa elimu ya uraia na uzalendo kwa makundi ya vijana ikiwemo wanafunzi
wa sekondari na vyuo pamoja na makundi mbalimbali katika jamii.
Mwaka 2014 program hiyo
ilifanikiwa kutoa elimu ya Muungano kwa wajumbe wa kamati za kudumu za
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za Uchumi na Fedha pamoja na
Katiba na Sheria.
Aidha, elimu hiyo ilitolewa kwa
baadhi ya wanafunzi wa Vyuo vya elimu ya juu kutoka Zanzibar na mikoa ya
Dodoma, ambapo vyuo vikuu vilivyoshiriki ni pamoja na Chuo Kikuu cha
Dodoma, Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini, Chuo cha Mtakatifu John,
Chuo cha Madini, Chuo cha Elimu ya Biashara , Chuo cha Ustawi wa Jamii
na Chuo cha Serikali za Mitaa cha Hombolo.
Katika mkoa wa Mbeya wanafunzi
kutoka vyuo vikuu vya Mzumbe, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Chuo Kikuu
cha Teophil Kisanji, Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia, Taasisi ya
Uhasibu na Chuo cha Elimu ya Biashara pamoja na vyuo vikuu vya mkoani
Iringa walishiriki kupata elimu ya Muungano kwa njia ya makongamano.
Pamoja na elimu hii kutolewa kwa
wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, pia wanafunzi wa shule za msingi wa
mkoa wa Dar es salaam zaidi ya 300 walipatiwa elimu hiyo kwa njia ya
maigizo, nyimbo, ngonjera na mashairi.
Vyombo vya habari pia vilitoa
elimu ya Muungano kupitia katika vipindi mbalimbali, ambapo mwaka 2015
redio Uhuru, TBC, Upendo na Televisheni za Azam, ITV na wadau mbalimbali
waliongelea masuala ya Muungano na hivyo kuwapa ufahamu zaidi wananchi.
Ndugu Baraka anasema kuwa katika
kutoa elimu hiyo, Idara yake huandaa makongamano ambapo mada mbalimbali
huwasilishwa kwa kina. Mada hizo huwa zinahusu uchumi, siasa, masuala
ya kijamii yanayohusu pande zote mbili na umuhimu wa watu kuishi pamoja
na kushirikiana.
Akizungumzia mwitikio wa elimu
hiyo kwa walengwa, ndugu Baraka alisema kuwa ni mzuri sana na wamegundua
kuwa watu wengi hawafahamu masuala muhimu ya Muungano, hasa faida zake.
Naye mwanafunzi Nadhifa Hassan
kutoka Zanzibar alisema kuwa elimu ya Muungano ni nzuri na wameipokea
kwa mikono miwili kwani wamekuwa wakielezwa taswira mbaya kuhusu
Muungano kuwa ni mbaya na unawaonea wananchi wa Zanzibar.
“Tumekuwa tukielezwa mtazamo
tofauti kuhusu Muungano kuwa unawanufaisha watu wa Tanzania Bara na kwa
upande wa Zanzibar hauna faida yoyote bali unawakandamiza” alisema
Nadhifa.
Kuhusu maadhimisho ya mwaka huu,
ndugu Baraka alisema Idara yake imejipanga kutoa elimu hiyo kwa
wanafunzi wa shule za msingi kutoka mkoani Dar es Salaam.
“Lengo ni kuwafanya wanafunzi hao waone kuwa nchi yetu ni moja na kuwa na mawazo chanya kuhusu Muungano.” anasema ndugu Baraka.
Akizungumzia faida za Muungano
anasema unawaunganisha wananchi wa pande zote mbili, kushirikiana katika
nyanja mbalimbali kiuchumi, kijamii na kisiasa na kuwa na taifa moja
lenye nguvu kiuchumi na kijamii na kiulinzi.
Baadhi ya wananchi
waliokwishahudhuria midahalo na kupata elimu juu ya Muungano walitoa
maoni yao kuwa ni vizuri baadhi ya viongozi wa siasa wakawa na dhamira
ya kweli ya kuuimarisha Muungano ili mwenendo wa Muungano usiwe na
mwelekeo wa kuuvunja na waliwataka wahusuka kupeleka elimu hii
vijijini ili umuhimu wake ufahamike kwa watu wote.
No comments :
Post a Comment