Friday, April 21, 2017

KUAJIRIWA NCHINI MADAKTARI WALIOTAKIWA KUFANYAKAZI KENYA, NI FURSA KWA TAIFA KUIMARISHA AFYA ZA WATANZANIA.

www.focusmedia.co_.tz rais
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
21/04/2017
Kihistoria Tanzania ina mahusiano mzuri na jirani zake, katika miaka ya hivi karibuni imekuwa ikishiriki kwa ukamilifu katika juhudi za kuhimiza usuluhishi wa migogoro kwa njia ya amani.
Sera ya Nchi za Nje ya Tanzania inalenga kupanga, kukuza na kulinda maslahi ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kwa kutumia kikamilifu na kwa uendelevu diplomasia ya
kiuchumi, kuhakikisha uhusiano wake na mataifa mengine, taasisi za kimataifa unazingatia maslahi ya kiuchumi, kujenga uchumi wa kujitosheleza, kudumisha amani na usalama wa taifa pamoja na kusaidia jitihada za kikanda na kimataifa kwa ajiili ya kuhakikisha kunawapo ulimwengu bora wenye amani. 
Hakika palipo na nia pana njia, nia njema ya kiongozi wa nchi ndio taswira halisi ya taifa katika kujali utu, mwandishi wa makalama haya anaunga mkono utayari wa kiongozi wa nchi kwa kujali watu ambao wapo tayari kuitangaza Tanzania nje ya mipaka yake kwa kufanyakazi ya kuokoa maisha ya watu wa mataifa mengine kulingana na sera yake.
Msukumo wa sera ya nchi umewapelekea Watanzania kuthamini taaluma zao na kuwa tayari kuitendea haki taaluama ya udaktari bila kujali mipaka ya nchi kwa ajili ya kujenga mahusiano mema na nchi nyingine, huo ni moyo wa kizalendo kwa taifa na watu wake.
Nichukue fursa hii kumpongeza kwanza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa utayari wake wa kujenga mahusiano mazuri na nchi jirani kwa tayari kwa utayari wake wa kutoa Madaktari kwenda kufanyakazi nchini Kenya.
Huo ni moyo wa kizalendo na utu ambao unapaswa kuigwa na wakuu wa nchi nyingine kuwa tayari kusaidia inapotokea uhitaji wa jambo fulani maana akufaaye wakati wadhiki ndiye rafiki, ni vema majirani wasaidiane ili kutoa huduma hitajiwa kwa haraka na kwa gharama nafuu kwa manufaa ya taifa.
Ni dhahiri jemedari Rais Dkt. Magufuli akiwa pia Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ameonesha nia ya dhati ya kuhudumia wananchi ndani ya jumuiya hiyo kwa kuwa tayari kutoa madaktari 500 kulingana na maombi ya Serikali ya Kenya.
Hakika madaktari Watanzania wapatao 496 waliwasilisha maombi yao, baada ya kufanyiwa uchambuzi ilibainika Madaktari 258 na wataalamu wa Afya 11 ndio walikidhi vigezo vinavyotakiwa kwenda kufanya kazi nchini Kenya.
Kwa mujibu wa Waziri wa afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari hivi karibuni mjini Dodoma, amethibitisha kuwa Serikali imeamua kuwaajiri madaktari hao 258 waweze kutoa huduma nchini badala ya kwenda kufanya kazi nchini.
Hatua hiyo ya Serikali ya Tanzania ya kuwaajiri madaktari hao imefikiwa baada ya madaktari wa Kenya watano kuwasilisha pingamizi mahakamani kuitaka Serikali ya nchi yao kusitisha kuajiri Madaktari kutoka Tanzania.
“Kwa upande wetu sisi ratiba ya utekelezaji wa ajira hizi za madaktari hao ilikubalika na pande zote iwe tarehe 6 Aprili 2017 madaktari hao wawe tayari kusafiri kwenda nchini Kenya kati ya tarehe 6 hadi 10 Aprili 2017. Hadi tarehe ya taarifa hii Mahakama nchini Kenya haijaondoa pingamizi lililofunguliwa kuhusu ajira za madaktari wa Tanzania nchini Kenya” alisisitiza Waziri Ummy.
Hakika uamuzi huo ni wa busara unaosimamia kujali utu wa watu bila kujali mipaka, kwa dhamiri hiyo na uamuzi Serikali, Madaktari hao watapangiwa vituo wawe tayari kwenda kufanyakazi yao ya kusimamia afya za Watanzania ili waweze kuwa na afya bora inayowawezesha kufanyakazi kwa juhudi na maarifa kwa maendeleo endelevu.
Msingi wa madaktari wa Tanzania kwenda kufanya Kenya ulitokana na nia ya Serikali Serikali ya Kenya kupitia ujumbe wa uliofika nchini Machi 18, 2017 ukiongozwa na Waziri wa Afya Dkt. Cleopa Mailu kuonana na Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa madhumuni ya kumuomba kuajiri kwa Mkataba Madaktari wa Tanzania ili kupunguza uhaba wa Madaktari nchini Kenya na kukubali ombi hilo.
Utayari wa Rais Dkt. Magufuli unakwenda sanjari na maneno ya aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Umoja Umoja wa Mataifa Boutros Boutros-Ghali kupitia Mkataba wa umoja huo ambapo aliwahi kusema “…….Umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa ni kudumisha amani na kuleta maendeleo, haki za binadamu, kuanzisha mazingira yatakayowezesha kupatikana kwa demokrasia, kukuza maendeleo ya kijamii na kuleta maisha bora”.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kupitia Mkutano wa Kimataifa wa Afrika juu ya Agenda Afya (AHAIC) ulifanyika Machi 7, 2017 Nairobi, nchini Kenya, yaliwekwa malengo kuwa Serikali za nchi za Afrika zinatakiwa kufanya utafiti katika sekta ya afya kwa kuwashirikisha vijana na watendaji wengine na kuweka nguvu ya pamoja katika kushughulikia matatizo ya magonjwa ndani ya bara la Afrika ambapo Tanzania ilitumia fursa hiyo ili kudumisha ushirikiano na jirani zake.
Aidha, ushirikiano unaooneshwa na Serikali ya Tanzania kwa mataifa mengine umejikita katika usemi wa Shirika la Afya Duniani unaohimiza mataifa yote kuwa “Kwa pamoja tujitahidi kupambana na magonjwa” ili kujenga afya bora kwa ajili ya watu wote duniani kwa kushirikiana na Serikali na Washirika wengine katika kuhakikisha watu wote wanapata huduma bora za afya.

No comments :

Post a Comment