Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akifungua kikao cha pamoja cha
Mawaziri wa Serikali za Tanzania na Uganda pamoja na wadau kuzungumzia
mradi wa ujenzi wa Bomba la Kusafirishia Mafuta Ghafi kutoka Hoima
nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.
Mkutano huo, uliofanyika Ikulu,
Dar es salaam, Jumanne Machi 28, 2017, ulihudhuriwa na Mawaziri wa
Nishati na Madini pamoja na Mawaziri wa Ardhi wa nchi hizo mbili,
Wanasheria wa Serikali na kampuni washirika wa mradi huo Lake Albert
(CNOOC, TOTAL na TULLOW).
Pamoja na mambo mengine, Mawaziri,
Maafisa na Wataalam wa pande zote husika walikaa na kukubaliana kwamba
rasimu ya makubaliano rasmi ya kuanza kwa mradi yawe yamekamilika na
kuwa tayari katika kipindi cha wiki mbili ili kuwezesha Marais wa
Tanzania na Uganda kuweka jiwe la msingi kuashiria kuanza ujenzi wa
kihistoria wa mradi huo wa
bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda
hadi Chongoleani mkoani Tanga, Tanzania.
PICHA NA IKULU.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 28 Machi, 2017 alikutana
na Mawaziri wa Nishati na Madini wa Serikali za Tanzania na Uganda
katika Ukumbi wa Baraza la Mawaziri Ikulu, jijini Dar es Salaam kwa
ajili ya kujadili Maendeleo ya Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika
Mashariki kutoka Hoima Nchini Uganda hadi Chongoleani, Tanga – Tanzania,
hususan katika masuala ya kikodi yatakayotumika katika mradi huo.
Mawaziri hao ni pamoja na Waziri
wa Nishati na Maendeleo ya Madini Nchini Uganda, Mhandisi Irene Muloni
pamoja na ujumbe wake na Waziri wa Nishati na Madini Nchini Tanzania
Profesa Sospeter Muhongo pamoja na wataalam kutoka Serikali zote mbili.
Wajumbe wengine ni pamoja na
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. John Lukuvi,
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Mcheche Masaju pamoja na Makampuni
ya Uwekezaji ya Mkondo wa Juu wa Ziwa Albert Nchini Uganda ya TOTAL,
CNOOC na TULLOW.
Masuala ya kikodi ni moja ya vipengele muhimu katika ukamilishwaji wa mkataba wa kimataifa kati ya nchi ya Tanzania na Uganda.
Mbali na kukaribisha washiriki wa
mkutano huo, Mhe. Dkt. Magufuli alisisitiza ahadi yake na Rais wa
Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Museveni ya kuhakikisha kuwa mradi huo
unakamilika kwa wakati.
Aidha, Dkt. Magufuli aliagiza
wawekezaji kutekeleza mradi huo bila kuchelewa kwa maana Serikali
imeshaweka mazingira mazuri ya utekelezaji wa mradi ikiwa ni pamoja na
masuala ya usalama, upatikanaji wa ardhi, kodi hivyo kupunguza gharama
za ujenzi Tanzania.
Pamoja na mambo mengine
mawaziri, maafisa na wataalam wa pande zote husika walikaa na
kukubaliana kwamba, rasimu ya makubaliano rasmi ya kuanza kwa mradi yawe
yamekamilika na kuwa tayari katika kipindi cha wiki mbili ili
kuwezesha Marais wa Tanzania na Uganda, kuweka jiwe la msingi kuashiria
ujenzi wa kihistoria wa mradi huo wa bomba la mafuta kutoka Hoima
Nchini Uganda hadi Chongoleani, Tanga-Tanzania.
Mradi huu upo katika hatua ya
awali ya tahmini ya mazingira pamoja na kubaini maeneo mradi utakapopita
ili mradi kuweza kutekelezwa kwa kasi pindi utakapoanza.
Imetolewa na:-
Kitengo cha Mawasilino Serikalini
Wizara ya Nishati na Madini
Machi 29, 2017
No comments :
Post a Comment