Saturday, February 11, 2017

WAZIRI MKUU ATAKA KERO ZA WANANCHI ZITATULIWE


 
BUNGEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEEE
*Asema mikutano ya vijiji, kata na mitaa haifanyiki kama inavyotakiwa
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema amebaini kuwa kero nyingi za wananchi hazitatuliwi na viongozi wa ngazi ya chini kwa sababu mikutano ya vijiji, kata na mitaa imekuwa haifanyiki kama inavyotakiwa kisheria.

“Azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kumtumikia kila Mtanzania popote pale alipo. Lakini nimebaini baadhi ya kero za wananchi ambazo zingeweza kutatuliwa katika ngazi za Wilaya, zinaletwa kwenye ofisi za Viongozi wa Kitaifa, au zinasubiri ziara za viongozi hao.”
Ametoa kauli hiyo leo jioni (Ijumaa, Februari 10, 2017) bungeni mjini Dodoma wakati akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa sita wa Bunge la 11.
“Nawasihi viongozi wa Mikoa na Halmashauri, tembeleeni vijijini na mtatue kero za wananchi huko vijijini; aidha, hakikisheni mikutano ya vijiji iliyowekwa kwa mujibu wa sheria inafanyika na maazimio yake yanafika kwenye vikao halali vya maamuzi. Waheshimiwa Wabunge, ninyi ni sehemu ya Halmashauri zenu, nawasihi toeni msukumo unaostahili kwa suala hili,” amesisitiza.
Waziri Mkuu amesema suala la kutotatua kero za wananchi katika ngazi ya Serikali za Mitaa ni kinyume na dhamira ya Serikali ya kuwatumikia wananchi wote bila ubaguzi ambalo pia ni kinyume na msimamo wa Ibara ya 146 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akinukuu ibara hiyo Waziri Mkuu amesema: “Madhumuni ya kuwapo Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi. Na vyombo vya Serikali za Mitaa vitakuwa na haki na mamlaka ya kushiriki na kuwashirikisha wananchi katika mpango wa shughuli za utekelezaji wa maendeleo katika Serikali zao na nchi kwa ujumla.”
Akisisitiza suala hilo, Waziri Mkuu amesema Sheria ya Serikali za Mitaa inaelekeza kuitishwa kwa Mikutano Mikuu ya Vijiji kila baada ya miezi mitatu. Sheria pia inatoa fursa ya kuitishwa kwa mikutano ya dharura, endapo ipo haja ya kufanya hivyo.
“Kutokana na msimamo huo wa kisheria na kutokana na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kutatua kero za wananchi, suala la utatuzi wa kero za wananchi halitakiwi kuendelea kusubiri ziara za viongozi, badala yake, kero hizo zitatuliwe kwenye ngazi zinazohusika na zitatuliwe kwa wakati,” amesisitiza.
Amesema watendaji wa kata, vijiji na mitaa hawana budi kuitisha mikutano ya kisheria ya viijiji na kata na mitaa na kusoma taarifa za mapato na matumizi ya miradi ya maendeleo katika maeneo yao. Amewataka viongozi na watendaji katika ngazi ya Mkoa, Wilaya na Halmashauri wajenge utamaduni wa kuwatembelea wananchi vijijini na kusikiliza kero na changamoto zinazowakabili ikiwa ni pamoja na kuzitafutia ufumbuzi.
“Wakurugenzi wa Halmashauri nao wanaagizwa kusimamia kikamilifu uitishaji wa mikutano mikuu ya vijiji na mitaa kwa mujibu wa sheria na kuchukua hatua dhidi ya viongozi wote watakaoshindwa kutekeleza sharti hilo la kisheria. Tembeleeni vijiji kusikiliza kero za wananchi,” amesisitiza.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesisitiza haja ya kila kaya kujiwekea akiba ya chakula ili Taifa liwe na uhakika wa chakula. “Usalama wa chakula unaanzia katika ngazi ya kaya, kila kaya inatakiwa iwe na utaratibu wa kuwa na chakula cha akiba. Wakati Serikali inaendelea na wajibu wake wa kuwa na hifadhi ya chakula, kila mwananchi anao wajibu wa kujiwekea akiba ya chakula cha kaya yake,” amesisitiza.
Akizungumzia kuhusu upatikanaji na usambazaji wa mbegu bora za mifugo, Waziri Mkuu amesema Serikali kupitia mashamba ya mifugo na vituo vya taasisi za Serikali vilivyoko kwenye maeneo mbalimbali, itaendelea kuhakikisha kuwa mbegu bora za mifugo zinazalishwa kwa ajili ya uhamilishaji, na mitamba na madume bora yanazalishwa kwa wingi na kusambazwa ili kukidhi mahitaji ya wafugaji.
“Ili kukabiliana na changamoto ya migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi, Serikali inahimiza wananchi waondokane na mazoea ya uchungaji na kujikita katika ufugaji wa kisasa ambao utawawezesha kuwa na mifugo michache yenye ubora ambayo itawaongezea tija katika uzalishaji wa nyama na maziwa mengi zaidi kwa ng’ombe mmoja.”
Amesema Serikali itaendelea kuimarisha Taasisi zinazoagiza mbegu za mifugo kutoka nje ya nchi kama vile Heifer Project International (HPI) na SAGCOT – Catalytic Trust Fund (CTF) na kwa kushirikiana na mashamba makubwa ya kisasa ya sekta binafsi ili wafugaji wawe na wigo mkubwa wa kuchagua aina bora zaidi za mifugo.

Vilevile, amesema Serikali itaendelea kuboresha na kuendeleza mashamba ya mbegu za malisho ya mifugo yaliyo chini ya Serikali katika maeneo mbalimbali nchini. “Nitumie fursa hii kuwaagiza maafisa ugani wa mifugo katika Halmashauri zote nchini, wafungue mashamba darasa ya kuzalisha mbegu hizo na kuhamasisha wafugaji kupanda malisho katika maeneo yao na kutoa stadi za ufugaji bora na wa kisasa. Baada ya miaka mitatu, Wizara husika ifanye tathmini ya utekelezaji wa agizo hili na kuwasilisha taarifa ofisini kwangu,” amesema.
Bunge limeahirishwa hadi Aprili 4, 2017.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
  1. L. P. 980,
DODOMA.
JUMAMOSI, FEBRUARI 11, 2017

No comments :

Post a Comment