Saturday, February 11, 2017

UZINDUZI WA KAMPENI ZA UZAZI WA MPANGO ZANZIBAR


UDA
 Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akipata maelezo ya matumizi ya huduma za uzazi wa mpango kutoka kwa mhamasishaji wa Shirika la Engender Health Joyce Ishengoma alipotembelea banda la maonyesho wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha huduma hiyo iliyofanyika kijiji cha Mkwajuni Wilaya Kaskazini A.
UDA 1
Mwakilishi wa Shirika la Engender Health Dkt. Martha Kisanga akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Kaskazini A wakati wa uzinduzi wa kampeni maalumu ya uhamasishaji wa uzazi wa mpango katika kijiji cha Mkwajuni.
 UDA 2
Wananchi waliojitokeza katika uzinduzi wa kampeni maalum ya uzazi wa mpango wakifuatilia uzinduzi huo uliofanyika Mkwajuni Wilaya ya Kaskazini A Unguja.
 UDA 3
Baadhi ya watoto walioshiriki uzinduzi wa kampeni maalum ya kuwahamasisha wazazi wao kujiunga na uzazi wa mpango wakifuatilia uzinduzi huo uliofanyika kijiji cha Mkwajuni.
 UDA 4
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na wananchi na wageni waalikwa katika uzinduzi wa kampeni ya uhamasishaji uzazi wa mpango uliofanyika Mkwajuni Wilaya ya Kasakazi A Unguja.
Picha na Makame Mshenga-Maelezo
……………..
Na Ramadhani Ali/Maelezo                
Zaidi ya akinamama 236 kati ya laki moja wanaofika hospitali na vituo vya afya kujifungua Zanzibar wanafariki kila mwaka kutokana na sababu mbali mbali zikiwemo kuacha kutumia huduma za uzazi wa mpango.

Kutokana na tatizo hilo Wizara ya Afya imeanzisha kampeni maalum ya wiki moja ya kuwahamasisha akina mama na akinababa kujiunga na uzazi wa mpango katika juhudi za kuokoa maisha ya wazazi na watoto.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo alizindua kampeni hiyo katika kijiji cha Mkwajuni Wilaya ya Kaskazini ‘A’ na kuwashauri akinababa kuwaruhusu wake zao kujiunga na uzazi wa mpango .
Alisema hidi sasa wanawake wanaostahiki kujiunga na uzazi wa mpango Zanzibar ni asilimia 14 tu waliojiunga na juhudi inatakiwa ifanywe ili iweze kufikia asilimia 20 ifikapo mwaka 2020 ili kulinda afya ya mama na mtoto.
Waziri Mahmoud alisema idadi ya akinamama wanaofariki ni kubwa zaidi ya takwimu zilizopo kwani wanaojifungulia hospitali ni asilimia hamsini tu na asilimia iliyobaki wanajifungulia majumbani na hakuna takwimu zao. 
Aliongeza kuwa Serikali imefanya juhudi kubwa za kusambaza huduma za uzazi wa mpango katika vituo vyote vya afya mijini na vijijini ili kuwaondoshea usumbufu wananchi hivyo amewashauri kuvitumia.
Akizungumzia vifo vya watoto chini ya miaka mitano, Waziri wa Afya alisema bado ni tatizo kubwa Zanzibar watoto 56 kati ya 1000 wanaozaliwa wakiwa hao hufariki dunia.
Alisema sababu kubwa ya vifo hivyo inatokana na wazazi kucheleweshwa kupelekwa hospitali ama kutopelekwa kabisa na kupelekea kujifungua katika mazingira yasiyo salama.
Kutokana na matatizo mengi yanayowapata akinamama wajawazito na watoto wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua, Waziri Mahmoud Thabit Kombo ameagiza kuundwa Kamati ya kitaifa itakayowashirikisha viongozi kutoka kada mbali mbali na washirika wa maendeleo kukabiliana nalo.
Mwakilishi wa Shirika la Engender Health Dkt. Martha Kisanga alisema ushiriki mdogo wa akinababa katika huduma ya uzazi wa mpango unachangia wanawake wengi kutojiunga na huduma hizo.
Katika risala ya wananchi wa Wilaya Kaskazini A iliyosomwa na Tatu Khamis Kombo walisema pamoja na vituo vingi vya afya kutoa huduma za uzazi wa mpango, mwamko bado ni mdogo na kufanyika kwa kampeni hiyo katika wilaya yao itasaidia wananchi wengi kujiunga.
Wilaya Kaskazini A na Wilaya ya Micheweni Pemba ndizo zenye asilimia ndogo zaidi ya akinamama waliojiunga na huduma ya uzazi wa mpango Zanzibar.
IMETOLEWA NA MAELEZO ZANZIBAR

No comments :

Post a Comment