Thursday, February 23, 2017

“UNESCO TANZANIA KUWAJENGEA UWEZO WAANDISHI WA HABARI”

index
Na Judith Mhina – MAELEZO
Shirika la Kimataifa la Elimu Sayansi na Utamaduni UNESCO Tanzania limeadhimia kuwajengea uwezo wa Waandishi wa Habari nchini ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kwa kufuata Sheria Kanuni na taratibu zinazosimamia taaluma yao.
Hayo yamesemwa na Kaimu Katibu Mtendaji wa UNESCO Taifa Dkt. Moshi Kimizi katika uzinduzi wa Kamati ya Kimataifa ya Mpango wa  Maendeleo ya Mawasiliano – IPDC iliyokutana Magogoni Jijini Dar-es-hivi karibuni.
Akizindua Kamati hiyo Dkt Kimizi alisema, Kamati ya Kimataifa ya Mpango wa Maendeleo ya Mawasiliano, inajukumu kubwa la kuelimisha, kuleta mageuzi na maendeleo katika mawasiliano.
Shirika hilo limedhamiria kuwajengea wanahabari uwezo katika nyanja za uhuru wa
upatikanaji wa habari bila vikwazo,  pia kuwawezesha Waandishi wa Habari, kumudu majukumu yao na kuhakikisha haki ya mwanahabari ya kufanya kazi yake kwa weledi bila kubughudhiwa inaenziwa.
Kamati ya kitaifa ya mpango wa mawasiliano inaundwa na wajumbe saba ikiongozwa na Mwenyekiti Dkt. Eva Solomon Msangi, Mhadhiri kutoka Shule Kuu ya Mawasiliano ya Chuo Kikuu cha Dar-Es-Salaam, na wengine wane ambao ni, mjumbe mmoja kutoka Wizara za Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wadau muhimu wa Habari kutoka Baraza la Habari Tanzania – MCT na Media Institute of Southern Africa – Tanzania -MISA TAN pamoja na Wawakilishi wawili kutoka UNESCO.
Dkt Kimizi aliwajulisha wajumbe kuwa wanajukumu la kuhakikisha sauti za walio  pembezoni au waliosahaulika zinasikika ,hivyo, Kamati inapopanga mipango yake iweke kipaumbele kwa kutenga rasilimali kwa ajili ya kuwajengea uwezo, pamoja na kuwaimarisha ili waweze kutoa habari na kupata habari bila vikwazo.
Akitoa taarifa ya Kikao cha Paris Ufaransa kwa kamati hiyo ya IPDC Dkt Eva Msangi alisema kikao kilisisitiza juu ya usalama, ulinzi dhidi ya Waandishi wa Habari uimarishwe na kuzingatiwa, kwa kuwa Waandishi wengi duniani wako katika hatari ya kuteswa au kuuwawa wakati wakitekeleza wajibu wao.
Dkt Msangi aliongeza kuwa baraza la Maendeleo la Mawasiliano la Dunia lilipendekeza na kuchagua mwenyekiti ambapo Bi Albana Shala kutoka Netherlands alichaguliwa kuendelea kwa kipindi kingine cha miaka minne. Katika kuweka uwiano wakijiografia wa Baraza, washirika wote wa UNESCO huwekwa katika makundi ya kikanda au kijiografia.
Makundi hayo sita ya kijiografia ni Ulaya ya Magharibi na Mataifa ya Amerika ya Kaskazini, kundi la pili Mataifa ya Ulaya Mashariki, kundi la tatu ni Mataifa ya Latin Amerika na Karibiani, kundi la nne ni Asia na Mataifa ya Pasifiki na kundi la tano ni Mataifa ya Afrika kipengele (a) na tano (b) ni Mataifa ya Kiarabu.
Tanzania ipo katika kundi la 5 (a), ambalo lipo chini ya uenyekiti wa Zambia. Pamoja na kwamba UNESCO katika Maendeleo ya Mawasiliano Kimataifa, imejikita katika masuala ya ulinzi na usalama wa Waandishi wa Habari lakini nchi husika inaweza Kuandaa miradi mingine ambayo inahusiana na maendeleo ya Waandishi naVyombo vya Habari.
Majukumu mengine ni kuwa na majukwaa ya kuchambua na kuelimishana il ikuwajengea uwezo kutoka ngazi ya chini na kwa wale wasio na sauti katika jamii. Kupanga mipango mbalimbali na kuridhia matumizi ya rasilimali fedha na kuitekeleza, Kuwa daraja kati ya wanataaluma wa Habari na Wadau wa habari.
Naye Mratibu wa Kamati ya Kimataifa ya Maendeleo ya Mawasiliano kutoka Tume ya Taifa UNESCO Tanzania Bi Christina Musaroche alisema ilikupanua wigo na idadi ya wajumbe kamati ina mpango wa kuongeza wajumbe wawili kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yaani Wizara ya Habari, Utamaduni na Utalii na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania TCRA.
Alisema mwakilishi kutoka Zanzibar ni muhimu katika kufanya kamati kuwa ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mwakilishi kutoka TCRA kwa ajili ya utambuzi wa sheria za mitandaoni sekta ya masiliano kwa ujumla.
Mwisho

No comments :

Post a Comment