Mkurugenzi mtendaji wa tume ya
Kikristo ya Huduma za Jamii Bw. Peter Maduki, akizungumza na waandishi
wa habari (hawapo pichani) leo jijini Dar es salaam
Mkurugenzi wa Idara ya Elimu, Bw.
Petro Pamba akisisitiza jambo wakati wa mkutano wa waandishi wa habari
juu ya maadhimisho ya miaka 25 ya CSSC.
Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Dr Josephine Balati, akifafanua jambo mbele ya waandishi wa habari
…………..
Alex Mathias,Dar es salaam
Tume ya Kikristo ya Huduma za
jamii (CSSC), inatarajia kuadhimisha miaka ishirini na mitano (25),
tangu kuanzishwa kwake mwaka 1992, maadhimisho yatakayofanyika kwa siku
mbili tarehe 21 na 22 mwezi Februari katika ukumbi wa Diamond Jubelee na
kuhudhuriwa na
wadau mbalimbali.
Akizungumza na waandishi wa habari
jijini Dar es salaam leo, mkurugenzi mtendaji wa tume hiyo, Peter
Maduki amesema, maadhimisho hayo yatatumika kutafakari na kuangalia
mafanikio na changamoto zinazoikabili sekta ya afya na Elimu nchini
pamoja na kuangalia mchango unaotolewa na taasisi za Mkanisa katika
maeneo husika.
“Tunaadhimisha miaka 25 ya
kuhudumia jamii kwakuwa sisi ni wadau wakubwa katika kushirikiana na
serikali kutoa huduma za jamii, ndiyo maana ukiangalia takwimu, utaona
kuwa Makanisa yanamiliki asilimia 14 ya taasisi zote zinazotoa huduma ya
afya hapa nchini, wakati huohuo makanisa yanamiliki takribani asilimia
42 ya hospitali zote nchini” Alisema Maduki.
“Makanisa bado yanaendelea
kuanzisha na kuendesha taasisi za elimu katika ngazi mbalimbali , hadi
mwishoni mwa mwaka 2016, Makanisa yalikuwa yanamiliki taasisi zipatazo
1006. Idadi hii ikiwa ni pamoja na vituo vya Elimu ya Awali
vilivyosajiliwa serikalini 300, shule za msingi 172, shule za Sekondari
318, Seminari 52, Vyuo vya Ualimu 11, Vituo vya Mafunzo Stadi 126, Vyuo
Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki 27” Aliongeza mkurugenzi huyo.
Akizitaja changamoto
wanazokabiliana nazo kwa kipindi chote hicho, mkurugenzi Maduki alisema
kuwa Uelewa, Umaskini na Utashi miongoni mwa watendaji na wananchi
vimekuwa ni kiwazo kikubwa ambacho hata hivyo alisema wanaendelea
kupambana navyo ili kuhakikisha Kanisa linaendelea kutoa huduma zake kwa
jamii kwakuwa huo ni wito wake.
Tume ya Kikristo ya Huduma za
Jamii (CSSC) inaundwa na Baraza la Maaskofu katoliki Tanzania (TEC) na
Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) na ilianzishwa mwaka 1992, kwa
dhumuni la kuratibu na kusimamia huduma za kijamii zitolewazo na Taasisi
za makanisa hususani za Elimu na Afya Nchini.
Kwa miaka mingi sasa, huduma za
jamii zitolewazo na makanisa hususani katika sekta ya Afya na Elimu
nchini zimekuwa msaada mkubwa kwa wananchi hususani wa maeneo ya
vijijini, huku zikiwa na ubora wa kiwango cha juu unaoonekana katika
matokeo ya mitihani mbalimbali kwa upande wa elimu na matibabu bora kwa
upande wa afya.
No comments :
Post a Comment