Tuesday, May 29, 2012

Wanachama wa NSSF Mwanza wachota bil. 5/-

22nd March 2010
Mfuko wa Hifadhi za Jamii (NSSF)

Wanachama 2,820 wa Mfuko wa Hifadhi za Jamii (NSSF) mkoani Mwanza, wamelipwa mafao yao yanayofikia Sh. bilioni 5.1 katika kipindi cha miezi minane.
Wanachama hao walilipwa kati ya Julai, mwaka jana na Februari, mwaka huu kufuatia maombi yao waliyotuma kwenye mfuko huko kwa kipindi hicho.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Meneja Mkuu wa (NSSF) mkoa wa Mwanza, Sostenes Nguma, katika maadhimisho ya Wiki ya NSSF yanayoendelea kote nchini.
Alisema katika kipindi hicho, NSSF mkoa wa Mwanza ulikusanya zaidi ya Sh. bilioni 11.3 kutoka kwa wanachama wake ambayo ni sawa ya asilimia 92.6 ya lengo la kukusanya zaidi ya Sh. bilioni l. 12.2.
Nguma alisema kudorora kwa hali ya uchumi wa dunia kumechangia Mfuko huo kutofikia malengo waliyojiwekea kwani makusanyo mengi katika mwaka huu hutokana na sekta ya madini, wafanyabiashara na wavuvi.
Kuhusu fao la matibabu linalotolewa na Mfuko huo, Nguma alisema hutolewa bure kwa wanachama waliotimiza masharti na si kweli kwamba hukatwa mafao yao.
Alisema katika Wiki ya NSSF, mfuko huo umekuwa ukijihusisha katika masuala ya kijamii ambapo kwa mwaka huu umepanda miti 1,000 ya matunda, kivuli na maua katika Shule ya Sekondari Nyamagana.
Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Nyamagana, Eromena Mallya, aliishukuru NSSF kwa kuchagua shule yake na kupanda miti hiyo na kuahidi kuitunza kwa hali na mali.
“Tunaushukuru Mfuko kwa kuiona shule yangu inafaa kuwa mfano kati ya sekondari 36 zilizo wilayani Nyamagana, watutembelee mara kwa mara na wataona namna tunavyoianza ikiwa ni sehemu ya utunzaji wa mazingira,” alisema Mallya.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment