Tuesday, May 29, 2012

SSRA yaanisha changamoto mifuko ya hifadhi ya jamii

8th October 2011
Chapa
Maoni
Muundo wa kisheria wa mifuko ya hifadhi jamii nchini ni moja changamoto zinazoikabili Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii nchini (SSRA).
Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam juzi na Mkurugenzi Mkuu wa SSRA, Irene Isaka, alipozungumza na wahariri wakuu wa vyombo vya habari kuhusu kazi za Mamlaka hiyo katika kusimamia mifuko ya jamii nchini.
Alisema hali ilivyo sasa mifuko hiyo kisheria inaripoti kwa wizara tofauti, akitaja kuwa Mfuko wa Pensheni Watumishi wa Umma (PSPF), Mfuko wa Pensheni ya Mashirika ya Umma (PPF) na GEPF iko chini ya Wizara ya Fedha; Mfuko wa Bima Afya (NHIF) uko chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii; Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) chini ya Wizara ya Kazi na Ajira na Mfuko wa Watumishi wa Serikali za Mitaa (LAPF) uko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na za Serikali Mitaa (Tamisemi).
Kadhalika, Isaka alisema kila mfuko una sera yake ya uwekezaji, wigo finyu wa hifadhi ya jamii kwa Watanzania yote kwa pamoja ikiwa imesajili asilimia mbili tu ya Watanzania wote.
Mifuko hiyo ina jumla ya wanachama 853,531 kati ya Watanzania milioni 42.
Mkurugenzi huyo alitaja changamoto nyingine kuwa ni mfumo ulipo sasa unabana wanachama kwani hauruhusu kuhamia mfuko mwingine; fofauti kwenye ukokotoaji wa mafao, tofauti kubwa ya mafao kati ya mifuko; ukosefu wa takwimu sahihi; gharama kubwa za uendeshaji wa mifuko, uelewa mdogo wa hifadhi ya jamii kwa watunga sera, waajiri na waajiriwa na umma kwa ujumla.
Isaka alisema ukosefu wa pensheni ya wazee ni changamoto kubwa kwani ni asilimia nne tu ya wazee ndio wanaopata mafao hayo.
Alisema mamlaka hiyo mpya kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imepata mtathmini ambaye anapitia tathimini zote za mifuko, hali ambayo itawasaidia kujua thamani halisi ya mifuko yote nchini.
Alisema baada ya kukamilika kwa zoezi hilo, SSRA watatoa taarifa na miongozo mbalimbali ili kusimamia vema sekta ya mifuko ya jamii nchini.
Isaka alisema SSRA inatarajia kuwa na wiki ya hifadhi ya jamii ambayo itafanyika Novemba mwaka huu ambayo mifuko yote ya hifadhi ya jamii itapata fursa ya kueleza umma shughuli wanazofanya ili Watanzania waijue.

CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment