Tuesday, May 29, 2012

Mifuko ya hifadhi ya jamii yaaswa kuboresha mafao ya wanachama

13th July 2011
Chapa
Maoni
Hifadhi ya jamii (NSSF)
Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (Tughe), kimeitaka mifuko ya hifadhi ya jamii (NSSF) na ya watumishi wa serikali za mitaa (LAPF) kuboresha mafao ya wanachama wao ili wanapostaafu wapate mafao yatakayowawezesha kujikwamua kiuchumi tofauti na ilivyo sasa.
Katibu wa Tughe mkoa wa Mara, Watson Lushakuzi, alitoa kauli hiyo katika taarifa yake ya utekelezaji wa kazi wa chama hicho katika kipindi cha miaka mitano iliyopita iliyowasilishwa kwenye mkutano mkuu wa Tughe mkoa.
Lushakuzi alisema mafao yanayotolewa kwa watumishi wa mifuko hiyo ni kidogo sana jambo linalowafanya wastaafu kuendelea kukabiliwa na hali ya umaskini licha ya kutumikia utumishi wao kwa zaidi ya miaka 30.
Alitolea mfano wa watumishi wengi waliostaafu miaka ya hivi karibuni wakiwa wamejiunga na mifuko hiyo wamejikuta wakiambualia kiasi cha kati ya Sh. 700,000 na milioni 1.2 huku wenzao wa Mfuko wa Utumishi wa Umma (PSPF) wakivuna mamilioni ya shilingi wanapostaafu.
Ameishauri mifuko hiyo ya NSSF, LAPF, PPF na GEPF kuboresha huduma ya mifuko kwa wanachama wake kama ilivyofanyika kwa Mfuko wa Watumishi wa Umma (PSPF) badala ya kuegemea zaidi kutumia fedha za wanachama kuwekeza katika miradi mbalimbali ikiwemo ile ya ujenzi wa majengo ya kibiashara, madaraja na vivuko.
Katibu huyo wa Tughe mkoani Mara ambaye pia ni mwanachama wa NSSF, alisema licha ya makato yanayofanywa na mifuko hiyo, bado huduma wanazotakiwa kupewa wanachama hazitolewi kabisa ikiwa ni pamoja na matibabu, mafao ya ulemavu, huduma za mazishi huku wastaafu wakikosa pesheni ya kila mwezi.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment