Tuesday, May 29, 2012

Sawa NSSF, wengine waige

4th February 2011
Chapa
Maoni
Maoni ya katuni

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), umetangaza kwamba umeanza mchakato wa kuzalisha megawati 300 za umeme ifikapo Desemba, mwaka huu. Hatua ya mfuko huo ina lengo la kusaidia kukabiliana na matatizo ya umeme yanayoikumba nchi kwa sasa na kulilazimisha Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kugawa nishati hiyo kwa mgawo.
Mpango huo ulitangazwa jijini Arusha juzi na Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhan Dau, ingawa hakutoa ufafanuzi kuhusu mahali ambapo umeme huo utazalishwa na gharama za mradi huo.
Aidha, Dk. Dau alisema kuwa mfuko wake unaangalia uwezekano wa kutandaza bomba la gesi kutoka Mnazi Bay hadi Dar es Salaam na Mwanza.
Hatua ya mfumo huo kubuni mradi wa kufua umeme huo imekuja wakati nchi ikiwa katika matatizo makubwa ya ukosefu wa umeme wa uhakika.
Tatizo la umeme nchini ni la muda mrefu kiasi cha kuilazimisha tanesco kuingia katika mikataba na kampuni nyingi za kigeni za kufua umeme wa dharura ikiwemo Independent Power Tanzania Limited (IPTL), Aggreko na Richmond/Dowans kwa kutaja baadhi.
Hata hivyo, baadhi ya mikataba hiyo hadi sasa inalalamikiwa kwamba imegharimu fedha nyingi za walipakodi na kwamba imewanufaisha vigogo na watu wachache.
Kwa mfano, mchakato wa kuipatia mkataba wa Richmond ulibainika kuwa ulitawaliwa na mazingira ya rushwa kutokana na kampuni hiyo kupewa tenda ya kufua umeme wa dharura wa megawati 100 bila kuwa na uwezo, na baadaye kuirithisha mkataba huo kampuni ya Dowans Tanzania Limited kinyemela.
Dowans licha ya kurithi mkataba wa Richmond bila kupitia utaratibu wa kisheria, iliishitaki Tanesco katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Biashara (ICC) kwa kusitisha mkataba wake baada ya Bunge kuazimia usitishwe.
Mkataba wa Richmond uliitikisa nchi baada ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, na mawaziri wawili Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi kulazimika kujiuzulu Februari mwaka 2008, baada ya kuhusishwa na kashfa hiyo.
Licha ya migongano ambayo imekuwa ikijitokeza kati ya serikali na makampuni ya kigeni ya kufua umeme, nchi inakabiliwa na utatizo la kutokuwa na umeme wa uhakika.
Nchi inahitaji angalao megawati 1,000, lakini imekuwa ikishindikana kutokana na sababu mbalimbali hususan kukauka mara kwa mara kwa mabwawa ya kuzalisha umeme kutokana na ukame.
Mabadiliko ya tabianchi yamekuwa yakichangia kukosekana kwa mvua za uhakika na hivyo kuchangia uhaba wa maji katika mabwawa ya kuzalisha umeme.
Tunaipongeza NSSF kwa kuliona tatizo hilo ambalo ni janga la kitaifa na kuamua kujitosa katika mchakato wa kuzalisha umeme.
Kwa kuwa NSSF ina mtaji wa kutosha, bila shaka itafanikiwa kuutekeleza mchakato huo na kuzalisha umeme huo ifikapo Desemba mwaka jana.
Mfuko huo umetangaza kuutekeleza mradi huo wakati hali imeanza kuwa mbaya kwa uchumi wanchi. Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu, jana alisema kuwa mgawo wa umeme unaoendelea utaathiri uchumi katika robo ya mwisho wa mwaka huu wa fedja .
Itakumbukwa kwamba Tanesco ilipandisha gharama za umeme kwa asilimia 18.5 Desemba mwaka jana, hatua ambayo imelalamikiwa na wananchi wengi kwamba itawaumiza kutokana na gharama za maisha kupanda maradufu.
Hatua hiyo pia imelalamikiwa na vyama vya wafanyabiashara kwamba itawaathiri wao na wawekezaji.
Ni vizuri NSSF ikajipanga kwa ajili ya kufanikiwa lengo hilo katika muda uliopangwa kwa kutilia maanani kwamba mfuko huo unaendesha miradi mingi nchini.
Hatua hiyo hainabudi kuwa changamoto kwa mashirika mengine nchini yenye mitaji ya kutosha kuangalia uwezekano wa kuwekeza katika miradi ya kufua umeme badala ya kusubiri Tanesco kufanya hivyo.
Huu ndio wakati kwa serikali kujipanga upya kubuni namna ya kupata vyanzo vingine vya nishati ya uhakika.

CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment