Tuesday, May 29, 2012

NSSF kuanza ujenzi wa Kigamboni mwaka huu

23rd March 2011
Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) limesisitiza kuwa ujenzi wa daraja la Kigamboni jijini Dar es Salaam unatarajia kuanza muda wowote mwaka huu.
Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhani Dau, alitoa kauli hiyo jana kwa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), inayoongozwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.
Dk. Dau aliwaambia wajumbe wa Kamati hiyo kuwa NSSF ina fedha za kutosha kukamilisha mradi huo ambao kwa sasa unafikia Dola za Marekani milioni 120.
Kwa upande wa utalii Kamati ya Hesabu za Serikali PAC, wajumbe wake walichachamaa na kutaka maelezo ni kwa nini wawekezaji katika mahoteli wanajenga kwa kutumia makuti.Wabunge wa Kamati hiyo walisema kitendo cha wawekezaji hao kujenga kwa kutumia makuti ni dalili ya wizi na hujuma kwa Serikali.
Walisema vifaa vingi vya wawekezaji vinasamehewa kodi hivyo hawana sababu ya kutumia makuti ambayo ni ya bei nafuu lakini sio ya kudumu na hatari kwa wateja kwa kuwa yanaweza kuungua muda wowote.Wabunge hao walitaka kupatiwa maelezo ni kwa nini baadhi ya mahoteli ya Kitalii yanajibadilisha majina baada ya kumaliza mkataba wa kufanya biashara kwa kuwa wanalenga kukwepa kulipa kodi.
Kamati hiyo pia ilimhoji Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kutokana na kushuka kwa mapato ya serikali ambayo yeye anahusika kuyakusanya.
Akijibu hojahizo za Wabunge hao, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Maimuna Tarishi, alikiri kuwepo tatizo hilo, lakini akasema tatizo halipo kwa wizara yake pekee bali kuna wadau wengi wanaohusika.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment