Tuesday, May 29, 2012

NSSF wajitoa kuzalisha umeme

3rd February 2011
Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF)

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umesema umeanza mchakato wa kuzalisha megwati 300 za umeme na kuziingiza katika grid ya taifa ifikapo Desemba mwaka huu, ili kusaidia kuondoa matatizo ya umeme yanayoikumba nchi kwa sasa.
Mpango huo ulitangazwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhan Dau, jijini Arusha.
Dk. Dau bila kutoa ufafanuzi kuhusu mahali ambapo umeme huo utazalishwa, alisema tayari mfuko wake umeshateua mtaalamu mshauri kwa ajili ya kutekelezwa kwa mradi huo, ambao pia hakutaja gharama zake.
Hatua hiyo imekuja wakati nchi ikikabiliwa na matatizo ya umeme na kulilazimisha Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco) kutangaza mgawo mara kwa mara.
Dk. Dau alikuwa akizungumza katika mkutano wa wadau wa NSSF unaofanyika jijini hapa na kuhudhuriwa pia na wawakilishi wa mifuko ya hifadhi ya jamii kutoka nchi jirani za Kenya, Uganda na Burundi.

Aidha, Dk. Dau alisema kuwa mfuko wake unaangalia uwezekano wa kutandaza bomba la gesi kutoka Mnazi Bay hadi Dar es Salaam na Mwanza.
Madhumuni ni kusambaza gesi inayozalishwa hapa nchini katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu,” alisema Dk. Dau bila kutoa ufafanuzi zaidi kuhusiana na mradi huo.
Kuhusu wanachama wa mfuko huo, Dk. Dau alisema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, wameongezeka kutoka 380,000 mwaka 2005/06 hadi 506,216 mwaka 2009/10 ambalo ni sawa na ongezeko la asilimia 33.
Alisema ifikapo Juni mwaka huu wanachama wanategemewa kufikia 518,410.
Kwa upande wa makusanyo, alisema yameongezeka kutoka Sh. bilioni 126.96 hadi Sh. bilioni 315.31 ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 148.
Mategemeo yetu ni kukusanya kiasi cha Sh. bilioni 404.58 ifikapo Juni mwaka huu,” alisema.
Akizungumzia uwekezaji, Dk. Dau alisema shirika limeendelea kuwekeza raslimali katika miradi ya muda mfupi na mrefu. Kutoka mwaka 2005/6 hadi 2009/10 uwekezaji wa Mfuko uliongezeka kutoka Sh. 424.89 bilioni hadi Sh. trilioni 1.03.
Alisema uwekezaji huu umesaidia kuongeza ajira na kuboresha thamani ya shirika.
Kuhusu ulipaji wa mafao, alsema Oktoba mwaka jana, NSSF ilipandisha pensheni kwa asilimia 52 ambapo kutokana na mabadiliko hayo kiwango cha chini cha pensheni kwa wastaafu kimeongezeka kutoka Sh. 52,000 hadi Sh. 80,000 kwa mwezi.
Katika hatua nyingine, Dk. Dau alisema tathmini inayoishia Juni 2009, imeonyesha kuwa NSSF inaweza kujiendesha, hata kama shirika litaacha kukusanya michango na bila kupata mapato yo yote kutoka katika vitega uchumi vyake, bado linaweza kuendelea kutoa mafao yote saba na kukidhi gharama za uendeshaji kwa muda wa miaka saba.
Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, aliipongeza NSSF kwa kujizatiti kuanza ujenzi wa daraja la Kigamboni na mipango ya kuzalisha megawati 300 za umeme na kuziweka katika gridi ya taifa pamoja na kusafirisha gesi asilia.
Hii ni mipango mizuri na ni endelevu kwa ustawi na maendeleo ya taifa. Ujenzi wa daraja la Kigamboni ambao kwa muda mrefu wananchi walitarajia kuwa litajengwa sasa watapata faraja kusikia kuwa utaanza wakati wowote,” alisema.
Kuhusu ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme ni jambo la muhimu zaidi na ni muafaka kwa uchumi wa taifa kwani upungufu wa umeme/kukatika mara kwa mara kwa umeme kunaathiri sana mitambo ya uzalishaji wa bidhaa viwandani, tija na ufanisi katika maofisi kupungua na hivyo kuleta athari kwa taifa,” alisema.
Lakini athari kubwa zaidi ni ile ya kukimbiza vitega uchumi kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza wa ndani na nje ya nchi na hivyo kusababisha ajira kwa wananchi kukosekana,” alisema, na kuongeza:
Jitihada hizi zinazofanyika na NSSF zitapunguza sana kama si kuondoa kabisa kero hizi.”
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa NSSF, Abubakar Rajabu, aliiomba serikali kutoa uamuzi wa kuukubalia mfuko huo kujenga majengo ya ofisi za ubalozi wa Tanzania nje ya nchi ili kuokoa fedha za serikali kwa kupanga ofisi.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment