Tuesday, May 29, 2012

Mkataba wa ujenzi daraja la Kigamboni wasainiwa

10th January 2012
Chapa
Maoni
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Ramadhani Dau, akiwa na Mkurugenzi Mtendaji Shi Yuan kutoka kampuni ya ujenzi ya China Railways Constructin Engineering Group, kwa pamoja wakiweka saini ya mkataba wa ujenzi wa daraja la Kigamboni na maungio yake jijini Dar es Salaam jana. Kazi hiyo ya ujenzi inatarajiwa kuchukua miezi 36.(PICHA: OMAR FUNGO)
Hatimaye ujenzi wa daraja la Kigamboni unatarajiwa kuanza hivi karibuni, baada ya jana Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) na mkarandasi aliyeshinda zabuni ya kutekeleza mradi huo, kutia saini mkataba wa makubaliano.

Ujenzi huo utatekelezwa na kampuni ya China Railway Construction Engineering Group Co. Ltd kwa kushirikiana na China Major Bridge Co. Ltd na utagharimu Sh. 214,639,445,523.80 kwa kipindi cha miaka mitatu.
MAGUFULI: TUFANYE KAZI, TUACHE SIASA
Akizungumza baada ya kusainiwa kwa mkataba huo, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, alimtaka mkandarasi kukamilisha kazi hiyo mapema iwezekanavyo hata kabla ya muda uliowekwa, lakini azingatie ubora wa kazi.
“Sioni sababu ya kusubiri muda huo kwa sababu pesa zipo; nataka mradi huu ukamilike kabla ya muda uliopangwa ili Rais Jakaya Kikwete auzindue kabla hajamaliza muda wake,” alisema.
Dk. Mgufuli, aliwaasa viongozi na wananchi kwa ujumla kuacha siasa kwenye masuala yanayohusu maendeleo kwa kuwa siasa inakwamisha mipango mbalimbali.
“Watanzania sasa wamechoka na maneno wanataka utekelezaji, tufanyekazi tuache siasa, zitatupotezea muda na zitatupeleka pabaya,” alisema Dk. Magufuli.
Aliongeza: “Ifike mahali tuache kusimamia siasa tupambane kuwaletea Watanzania maendeleo.”
Kuhusu miradi mingine, alisema serikali inatekeleza miradi mingi ya ujenzi wa barabara na madaraja na kwamba makandarasi wamekuwa wakituma maombi kila siku.
Alisema serikali imejipanga kupanua barabara ya Morogoro kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze na ya kutoka Arusha-Himo, mkoani Kilimanjaro; pamoja na ile ya mabasi ya mwendokasi kutoka Kimara hadi Kivukoni, jijini Dar es Salaam.
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhan Dau, alisema daraja hilo litakuwa la njia sita za lami za magari na njia za waenda kwa miguu.
Aliishukuru serikali kwa kukubali kuchangia asilimia 40 ya gharama za ujenzi na kuahidi kwamba shirika lake litaendelea kushirikiana na serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali yenye manufaa kwa taifa.
AJIRA 2,000 KUZALISHWA
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki, alisema mradi huo utazalisha ajira za muda mfupi zaidi ya 2,000 na kuwataka wananchi hususani vijana kuzichangamkia na kuhakikisha wanafanyakazi kwa bidii na uadilifu.
Hata hivyo, aliwaonya watu wenye tabia za wizi kutothubutu kwenda kwenye mradi huo kwa kuwa ataimarisha ulinzi kwenye eneo hilo: “Hata ikiwezekana tutaweka kituo cha polisi pale, vijana wa Dar es Salaam changamkieni ajira hizi, lakini msiwe wazembe au wadokozi.”
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Patrick Mfugale, ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya wataalam wanaosimamia ujenzi huo, alisema kamati yake itafanyakazi kwa uadilifu ili kuhakikisha kuwa daraja hilo linajengwa kwa ubora wa kimataifa.
Hafla ya kusaini makubaliano hayo ilihudhuriwa na wadau mbalimbali akiwemo Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, ambaye alisema mradi huo utazalisha pia ajira za kudumu takribani 1,000.
Wengine ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Balozi Hubert Mrango, Wenyeviti wa Bodi mbalimbali ikiwemo ya makandarasi, wahandisi, wabunifu majengo na wakadiriaji majenzi na maofisa wengine waandamizi kutoka Wizara ya Ujenzi na NSSF.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment