Zanzibar. Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi ameikabidhi Benki ya CRDB Plc jukumu la kutoa elimu ya fedha na kutoa mikopo isiyo na riba kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo walioko visiwani ikiwa ni sehemu ya kutambua maendeleo ya ajenda ya uchumi wa buluu.
Akizungumza visiwani humo Jumamosi iliyopita wakati akizindua programu ya “Inuka na Uchumi wa Buluu” inayotekelezwa kwa ushirikiano na benki hiyo, Rais Mwinyi alisema serikali yake iliweka kiasi cha Sh81.5 bilioni kwa lengo la kuvinufaisha vikundi vya wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo.
“Tumeipa Benki ya CRDB jukumu la kutoa elimu ya fedha na mikopo bila riba kwa vikundi vya wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo kwa sababu ya rekodi nzuri ufuatiliaji ya benki,” Dk Mwinyi alisema.
Aliongeza kuwa benki hiyo iliyoko jijini Dar es Salaam inatarajiwa kutenga kiasi sawa cha fedha kwa ajili ya kuwapa wafanyabiashara kuwekeza katika sekta mbalimbali zikiwemo za kuuza chakula, bodaboda, saluni za kike, wavuvi, wakulima wa mwani na wafanyabiashara.
Alisema Serikali yake tayari imeanza kuwapatia wafanyabiashara wadogo vitambulisho ili wasinyanyaswe wanapofanya biashara zao akisema serikali hiyo pia inajenga masoko ya kimataifa ili kumpa eneo la biashara kila mtu ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara wadogo wadogo.
“Ushauri wangu kwenu ni kwamba naomba muondoke katika eneo ambalo ujenzi wa masoko hayo unafanyika na niwahakikishie kwamba mara baada ya miradi hiyo kukamilika, mtapewa kipaumbele wakati wa kutenga maduka,” alisisitiza huku akiwaonya wasaidizi wake kuwa yeyote atakayejaribu kukwamisha juhudi za ajenda ya uchumi wa buluu yu mbioni kufutwa kazi.
Mpango huu utakapokamilika, utazalisha ajira rasmi zaidi ya 300,00 huku takribani wamiliki wa biashara 700,000 wakinufaika moja kwa moja na mikopo lakini pia mafunzo ya ujuzi wa masuala ya fedha.
Akitoa maelezo kwa Dk Mwinyi kuhusu shughuli za benki hiyo visiwani humo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema makubaliano hayo na Serikali ya Zanzibar ni fursa mpya kwa wafanyabiashara kujinufaisha na kukua zaidi kufikia kuwa kampuni kubwa baadaye.
“Tangu mwaka jana tayari tumeshatoa mikopo ya zaidi ya Sh150 bilioni kwa wafanyabiashara wa sekta mbalimbali ikiwemo utalii, uvuvi, kilimo na biashara,” Nsekela alisema huku akifafanua chini ya mpango wa ‘Inuka na Uchumi wa Buluu’, wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wadogo tayari wameshaanza kupata mafunzo ya ujuzi wa masuala ya fedha.
Alisema biashara zisizo rasmi ambazo huchangia angalau asilimia moja ya pato la taifa la visiwa hivyo, ni sehemu muhimu ya wateja wanaohudumiwa na benki kubwa nchini kwa upande wa amana na thamani halisi ya mali.
“Kupitia Mpango wa Inuka, benki imetenga Sh60 bilioni kukopesha wafanyabiashara na ikihitajika zaidi itatolewa bila riba kama ilivyokubaliwa na serikali,” aliongeza. Kabla ya kuzindua mpango wa uchumi wa buluu, benki ilikuwa imetoa mikopo yenye thamani ya Sh94 milioni kwa vikundi vitano.
“Pia tumeidhinisha mkopo wa Sh2 bilioni kwa kikundi cha wavuvi kununua boti za
kisasa za uvuvi na nguo maalumu za uvuvi,” Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB alibainisha. Katika mwaka uliopita, CRDB pia iliwekeza mabilioni ya shilingi katika miradi ya jamii kama sehemu ya uwajibikaji wake wa kijamii na shughuli nyingine nyingi za kusaidia kufanyika kwa tamasha la utamaduni la ‘Kizimkazi’ ambalo mwaka jana lilipambwa na Rais Samia Suluhu Hassan.Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Dk Juma Malik Akil alisema Sh81.5 bilioni pamoja na mambo mengine, zitatoa mikopo kwa wavuvi ili kupata boti 577 za uvuvi, meli nyingine ndogo 500 ili kuwezeshawakulima wa mwani ambao wengi wao ni wanawake kutembea kwa urahisi kwenye mashamba yao yaliyoko baharini na ujenzi wa kiwanda cha kusindika mwani katika visiwa vya Pemba.
“Mradi huu unatarajiwa kuwanufaisha wajasiriamali zaidi ya 700,000 moja kwa moja wakati wa hatua ya awali kwa sababu ufadhili huo unaendelea na utadumu miaka kadhaa ijayo,” Dk Akil alisema huku akiwataka walengwa hasa wanaume kuacha matumizi mabaya ya fedha kwa kuoa wake wa pili.
Akitoa ushuhuda wa programu hiyo, mmoja wa wanufaika, Hamis Hamad Hamis kutoka Visiwani Pemba alisema kikundi chake cha wanachama 20 kinachojishughulisha na ufugaji kimeweza kupata mkopo wa Sh25 milioni kuanzisha kiwanda cha kusindika maziwa.
“Kutokana na uongezaji wa thamani, maziwa yetu ambayo yalikosa soko la uhakika hapo awali na hivyo kuharibika, yameongezeka bei ambapo lita sasa inauzwa zaidi ya Sh3,000 kutoka Sh1,500,” Hamis alisema huku akibainisha kuwa kikundi kilichokuwa kinazalisha lita 100 kwa siku pia kimeongeza uzalishaji hadi lita 500.
No comments :
Post a Comment