Sunday, December 5, 2021

Waajiri wasilisheni michango ya wafanyakazi wenu kwa wakati muafaka-Mh.Waziri Soraga

Waziri wa nchi ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji Zanzibar Mheshimiwa Mudrik Soraga

Na Christian Gaya-HakiPensheni, Zanzibar.

Waziri wa nchi ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji wa Zanzibar Mheshimiwa Mudrik Ramadhani Soraga aliwakumbusha waajiri juu ya wajibu wao wa kujisajili na Mfuko wa hifadhi ya jamii  Zanzibar (ZSSF) pamoja na wafanyakazi wao kuwa wanachama wakati wa mkutano mkuu wa sita wa wadau wa Mfuko  huo uliofanyika hivi karibuni katika Ukumbi wa Michezani jijini Zanzibar. 

“Waajiri wa sekta binafsi walitekeleze hilo na kuwasilisha michango kwa wakati ili walengwa wasipate usumbufu unapofika wakati wa kustaafu. Jumuiya ya Waajiri Zanzibar (ZANEMA) ambao nao ni wadau wakubwa wa mkutano huu hawana budi kuwakumbusha waajiri juu ya jukumu hili la kisheria ili kujenga mstakbala mzuri baina ya waajiriwa, ZSSF na waajiri,”Waziri Soraga ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mkutano huo alisema.

Waziri Soraga pia alitoa shukurani zake za dhati kwa uongozi wa Mfuko wa ZSSF kuweza kuendelea na mikutano hii ya wadau ukiwa mkutano wa wa sita  uliyowajumuisha wadau wa Mfuko huo kutoka taasisi za Serikali na za kampuni binafsi.

“Ni jambo lilowazi kwamba fursa kama hizi za kukutana na kujadili kwa pamoja zikitumiwa ipasavyo hutarajiwa kuleta matunda yasiyo mithilika katika Taasisi zetu,” Waziri Soraga alitamka.

Pia aliwakumbusha waajiri kujisajili na kuwasilisha michango kwa wakati ili walengwa wasipate usumbufu unapofika wakati wa kustaafu.

 “Jumuiya ya Waajiri Zanzibar (ZANEMA) ambao nao ni wadau wakubwa wa mkutano huu hawana budi kuwakumbusha waajiri juu ya jukumu hili la kisheria ili kujenga mstakbala mzuri baina ya waajiriwa, ZSSF na waajiri.” Waziri alisisitiza.

Alisema hifadhi ya jamii ni haki ya msingi ya kila mwananchi awe mtu mzima ama mtoto mdogo popote awapo katika ulimwengu huu. Tangazo la Umoja wa Mataifa la mwaka 1948 linasisitiza hayo. Utekelezaji wa agizo hilo ulitokana na Azimio la Shirika la Kazi Duniani nambari 102 la Hifadhi ya Jamii la mwaka 1952.

“Hifadhi ya jamii inaweza kutafsiriwa kwa ujumla kama ni maandalizi au kinga ya kiuchumi na kijamii dhidi ya dhiki inayosababishwa na kupoteza uwezo wa kipato kutokana na umri, maradhi, kuumia kazini au kufariki dunia. Kutokana na athari kubwa ambazo mwanachama anaweza kuzipata kwa kupoteza kipato, uendeshaji wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ni jukumu la Serikali zote duniani,”Waziri Soraga alifafanua.

Alisema sekta ya hifadhi ya jamii kwa Zanzibar inayo historia ndefu sana. Sekta hii ilikuwepo kabla ya Mapinduzi mwaka 1964 lakini walionufaika wakati huo walikuwa ni wachache tu wale ambao waliobahatika kufanya kazi za ukarani katika Serikali ya Kikoloni na pia kulikuwa na hifadhi ya jamii za kikabila au madhehebu.

“Tangu 1964 Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imefanya jitihada kubwa katika kuendeleza hifadhi ya jamii kwa wananchi kupitia mfuko mkuu wa Serikali. Mfumo huu ulikuwa ndiyo njia kuu ya hifadhi ya jamii Zanzibar mpaka mwanzo 1990 wakati Serikali ilipoanza kupambana na hali ngumu ya uchumi. Pia ilichangiwa na ongezeko maradufu la watu kutoka 300,000 mwaka 1967 hadi 750,000 mwaka 1997,”alifafanua zaidi.

Alisema mfuko wa ZSSF ulianzishwa kwa Sheria Na. 2 ya mwaka 1998 ambayo ulirekebishwa na Sheria Na 9 ya mwaka 2000, pia ulirekebishwa kwa notisi ya Serikali ya 2004 na kuanzishwa upya kwa Sheria Na 2 ya mwaka 2005 baada ya kufanyiwa mapitio. Mkutano huu ni fursa adhimu kwenu kupata wasaa wa kukutana na uongozi wa Mfuko, ili kuweza kuona jinsi ya mambo yanavyoendeshwa ndani ya Mfuko wa ZSSF. Lakini pia mtapata fursa ya kutoa maoni yenu ambayo ninaamini yatakuwa chachu ya maendeleo ya Mfuko huu.

“Naomba kutumia fursa hii kukumbushana machache yanayohusu Mfuko huu na jinsi tunavyoweza kuutumia na kufaidika nao. Yapo maeneo ambayo tayari yamekwisha elezwa vizuri na wasemaji waliopita. Madhumuni makuu ya mkutano huu ni kuzidisha mashirikiano baina ya Mfuko na wadau wake sambamba na kuondoa changamoto zinazoukabili. Hivyo naomba muitumie fursa hii kwa kuona utendaji ulivyofikiwa na kutoa mawazo chanya na kuamini kuwa Mfuko huu ni wetu sote,” Waziri Soraga alisisitiza.

Christian Gaya ni mwanzilishi wa Kituo cha HakiPensheni, mshauri na mtaalamu wa masuala ya pensheni, mipango ya kustaafu na elimu ya kuwekeza pensheni. Kwa maelezo zaidi wasiliana: gayagmc@yahoo.com unaweza kutembelea tovuti hakipensheni website: Simu 0655 13 13 41

No comments :

Post a Comment