Tuesday, June 8, 2021

JATU YAJA NA KAMPENI BUKU TANO INATOSHA KUWAKOMBOA WANANCHI KIUCHUMI DAR


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

WAKAZI mbalimbali wa Jiji la Dar es Salaam wameelezea kuguswa na ubunifu wa kampeni ya

uchumi na maendeleo ya ununuaji  wa hisa za Kampuni ya Jenga Afya Tokomeza Umasikini(JATU) iliyolenga kuwakomboa kiuchumi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi hao wamesema kwamba kampeni hiyo imewapa mwanga wa kuongeza maarifa zaidi ya kujikwamua kiuchumi kupitia miradi yao ya kimaendeleo.

Kampeni hiyo ambayo ilizinduliwa mapema wiki hii katika eneo la Bunju A jijini Dar es Salaam imelenga kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kumiliki hisa za JATU kama dhamana ya kuendeleza kwa faida shughuli zao za kiuchumi.

Akizungumza  wakati Mkazi wa Bunju Agness Mabula amesem kampeni hiyo inawapa wananchi fikra mpya ya kujiamini zaida katika kukuza biashara zao.

"Huu ubunifu umenifumbua macho, na umenivuta kuingia moja kwa moja katika umiliki wa hisa za JATU kwa sababu nimeona unanipa urahisi mkubwa wa kudhaminika kwa kupewa mikopo mingine yenye riba au isiyo na riba,"amesema  Mabula.

Kwa upande wake Said Mohamed  ambaye ni dereva bodaboda  amesema  kampeni hiyo ni rafiki sana na mipango ya Serikali ya kutokomeza umasikini.

Ameongeza kwa watu wote wanaojihusisha na ujasiliamali, kilimo au  biashara ni wakati mwafaka kwao kujiunga na hisa za JATU kwani zinawaweka kwenye mazingira bora zaidi ya kukuza mitaji yao na hata kukopesheka kirahisi.

Awali akifungua kampeni hiyo ambayo inakwenda kwa kauli mbiu ya  "Buku Tano Inatosha", Meneja Mkuu wa Kampuni ya JATU Steven Muligo amesema kampeni ya ununuzi wa hisa za kampuni hiyo imelenga kutoa elimu kwa Watanzania juu ya kujiamini kwenye mikakati yao ya kujikwamu kwenye umasikini.

Amefafanua  kampuni hiyo imejikita zaidi katika mikakati ya kutokomeza umasikini, hivyo wameamua kutumia utaratibu wa kuuza hisa kwa wananchi ili kuwapa fursa za kuwa sehemu ya umiliki wa kampuni hiyo.

"Hisa yetu moja inauzwa shilingi 500 tu, na mteja ili kujiunga nasi anatakiwa kununua hisa 10, namaanisha shilingi 5,000 na kila mwisho wa mwaka anapata gawio kwa faida ikizingatiwa kwamba hisa za kampuni yetu zipo kwenye soko la hisa la Dar es Saam," amesema.

Ameongeza uwekezaji wa kampuni hiyo upo katika kilimo cha kisasa cha mashamba makubwa ya nafaka, matunda pamoja na biashara mbalimbali za mazao katika mikoa mbalimbali hapa nchini.

 

No comments :

Post a Comment