Friday, December 25, 2020

MKIRIKITI AREJESHA MALI ZA WAATHIRIKA 10 WA MIKOPO UMIZA WALIOSAIDIWA NA TAKUKURU


***************************************
Na Mwandishi wetu, Manyara
WAATHIRIKA 10 wa mikopo umiza wa Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, wamerejeshewa mali zao baada ya kuchukua mikopo umiza hiyo na kuishiwa matumaini ya kupatiwa mali zao.
Waathirika hao 10 wa mikopo umiza waliofaidika ni Raphael Ombade aliyerudishiwa gari aina ya Opel Vectra na kadi yake, Yasintha Adiro nyumba na nakala ya hati ya kiwanja, Mosses Makala nyumba tatu na kadi ya pikipiki, Bernady Nyarasya mkataba wa nyumba na Godwin Mmasy pikipiki .
Wengine ni Jimmy Kibindi pikipiki, John Laizer shamba la ekari tatu na nusu na mkataba wa kuweka shamba rehani, Mohamed Matinda gari na kadi yake na Lengayen Rumas gari aina ya Toyota Land Cruser na kadi yake.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Joseph Mkirikiti amekabidhi mali hizo Desemba 24 kwenye mji mdogo wa Mirerani na Kata ya Shambarai Wilayani Simanjiro ambapo mali hizo zilikamatwa baada ya waathirika wa mikopo umiza kusaidiwa kurejeshwa na Taasisi ya Kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU).
Mali hizo ni viwanja, nyumba, pikipiki, magari, mashamba na kadi za pikipiki na magari zilizokopwa kwa shilingi milioni 32 lakini aliyetoa mikopo umiza hiyo akawa anawadai marejesho na riba ya shilingi milioni 80.
Mkirikiti ameipongeza TAKUKURU kwa kufanikisha kurejeshwa kwa mali hizo kutoka kwa waathirika wa mikopo umiza.
Amesema japokuwa waathirika hao wa mikopo umiza walikuwa na mahitaji ya fedha wangepaswa kukopa kwenye taasisi za fedha kuliko kukopa kwa mtu binafsi ambaye hana leseni ya kufanya biashara.
‘Kuna taasisi nyingi za fedha ikiwemo mabenki ambayo yanatoa mikopo kihalali hivyo wananchi msiwe mnajihusisha kuchukua mikopo ambayo hainamanufaa kwenu kwani japokuwa mtu utakuwa una shida ya fedha lakini unaangamia,” amesema Mkirikiti.
Mkuu wa wilaya ya Simanjiro, mhandisi Zephania Chaula amempa siku 14 aliyechukua mali kupitia mikopo umiza hiyo kurudisha mali zilizobakia kwa waathirika hao.
“Naipongeza TAKUKURU Simanjiro kwani inafanya kazi kubwa ya kuisaidia jamii kwenye masuala mbalimbali ila wananchi nanyi msikubali kurubuniwa na watu matapeli kwani kuna hadi viongozi wa dini wanashiriki kufanya hii michezo,’ amesema mhandisi Chaula.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu ametoa rai kwa watu wenye nia ya kufanya biashara ya fedha, wafuate utaratibu wa kukata leseni na kulipa kodi stahiki ili waweze kufanya biashara hiyo kwa mujibu wa sheria.
Makungu amesema baada ya urejeshaji huo ni vyema wananchi wakafahamu kuwa sheria ya biashara ya fedha The Microfinance Act 2018 inatoa katazo kufanya biashara ya fedha kwa kutoza riba bila kuwa na leseni.
“Kifungu cha 16 cha sheria hiyo kinatoa adhabu kali ya kifungo kisichopungua miaka miwili na kisichozidi miaka mitano kwa anayekiuka sheria hii,” amesema Makungu,
Mkuu wa Takukuru wilaya ya Simanjiro Adam Kilongozi ametaja baadhi ya mali zilizokuwa zimechukuliwa kwenye mikopo umiza hiyo ni magari, pikipiki, nyumba, mashamba na kadi za pikipiki na magari.
Kilongozi amempongeza hakimu wa mahakama ya wilaya ya Simanjiro Charles Uisso kwa kutenda haki na kutoa uamuzi sahihi baada ya kupitia maamuzi ya mahakama ya mwanzo Mirerani kwani mkopeshaji hakuwa na leseni ya kufanya biashara hiyo.
Baadhi ya waathirika wa mikopo umiza hiyo wameishukuru serikali kwa kuingilia kati hadi kufanikiwa kurejeshewa mali zao kwani ni muda mrefu walichukua mikopo hiyo na kubambikiwa riba kubwa.
Mkazi wa mji mdogo wa Mirerani, Yasintha  Adiro amesema mume wake Ogola Owende alichukua mkopo wa shilingi milioni 10 na laki tatu na kuweka rehani nyumba na hati ya kiwanja kasha akakimbia na kuhama mji huku akiwaachia watoto.
Yasinta amesema alifungua kesi mahakama ya mwanzo Mirerani na kushindwa kesi hiyo ila akakata rufaa mahakama ya wilaya ya Simanjiro akapatiwa ushindi kwani mwenye mikopo umiza huyo hakuwa na nyaraka zinazomruhusu kukopesha watu hivyo akashinda kesi na kurejeshewa nyumba yake.
Mkazi wa kata ya Shambarai Mosses Makala amesema nyumba zake tatu zilikuwa rehani na aliyempa fedha zake shilingi milioni saba na akatakiwa kurejesha shilingi milini 43 kisha nyumba hizo zikageuzwa kuwa maghala ya kuhifadhi mahindi huku nyumba moja ikibomolewa.
Hata hivyo, mmiliki wa mikopo umiza hiyo Nicas Lyimo amesema baadhi ya mali za wakopaji hao ikiwemo baadhi ya magari zililetwa na wamiliki zikiwa zinavutwa hivyo hatagharamikia kuzitengeneza zaidi ya kunirudishia kama zilivyo.
“Kuna baadhi ya mali ikiwemo pikipiki na magari zililetwa kwangu zikiwa zinasukumwa au kuvutwa na kamba hivyo watarejeshewa zikiwa kwenye hali hiyo zilizokuja kwani hazikuwa zinatumika zilikaa hapa kama dhamana, naomba hilo lifahamike,” amesema Lyimo.
Amesema nyumba moja kati ya tatu za Makala ilibomoka kutokana na mvua zilizonyesha ila nyingine mbili zipo na alihifadhi mahindi na atayaondoa baada ya amri ya serikali.

 

No comments :

Post a Comment