Wednesday, December 16, 2020

KAMPUNI YA SIGARA TANZANIA YATATUA KERO ZA WALEMAVU NYASA

Afisa miradi ya Kampuni ya Sigara Tanzania Bw. Oscar Luoga (mwenye shati jeupe) akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mh. Isabella Chilumba Baiskeli 23, fimbo nyeupe 5 na magongo ya kutembelea 100 kwa ajili ya walemavu wa Wilaya ya Nyasa.Picha na Ofisi ya Ded Nyasa

****************************************

Kampuni ya Sigara Tanzania imekabidhi kwa Wilaya ya Nyasa,  vifaa vyenye thamani ya shilingi

14,367,500 kwa ajili ya walemavu wa  wilaya ya Nyasa.Vifaa vimekabidhiwa jana, katika hafla fupi iliyofanyika katika Viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya  ya Nyasa Mkoani Ruvuma.

Akikabidhi Vifaa hivyo Afisa Miradi wa Kampuni ya Sigara Tanzania Bw Oscar  Luoga, amesema kampuni ya Sigara imeona itoe Vifaa hivyo, kwa walemavu wa Wilaya ya Nyasa, ili kuwakwamua kiuchumi kwa kuwa shirika la Sigara linaamini katika kusaidia jamii, hasa yenye uhitaji,na kuunga juhudi za Serikali katika kuleta Maendeleo.

Amevitaja vifaa alikabidhi kuwa ni Baiskeli za Miguu mitatu 23, magongo 100, na Fimbo nyeupe 5 ambavyo viliombwa katika Kampuni yake na Mbunge wa Wilaya ya Nyasa Mhandisi Stella Manyanya, kwa ajili ya kutoa Huduma kwa walemavu ili kuwasaidia waweze kutembea na kujikwamua katika shughuli mbalimbali zakiuchumi.

“Ndugu viongozi wa Wilaya ya Nyasa na wananchi wa Wilaya ya Nyasa kampuni ya Sigara Tanzania imeamua itoe vifaa hivi kwa ajili ya walemavu kwa kuwa tunaamini katika kusaidia wahitaji hasa  jamii yenye uhitaji na kwa mwaka huu tumeamua kuisaidia jamii ya wenye ulemavu Wilaya ya Nyasa hasa kwa kauli Mbiu inayotumika katika kampuni ambayo ni Tunaleta mabadiliko pamoja na, kutoa ni moyo”

Akizungumza katika hafla hiyo Mbunge wa Jimbo la Nyasa Mhandisi Stella Manyanya, amewashukuru kampuni ya Sigara kwa kutoa vifaa hivyo kwa walemavu, ambao wamekuwa na uhitaji wa muda mrefu.kabla ya vifaa hivyo walemavu hao walikuwa wakitambaa chini, na wengine kutembea kwa shida kutokana na ukosefu wa Viungo mbalimbali vya mwili.

Aidha mbunge Manyanya alitoa shilingi milioni moja kwa ajili ya kuwapa walemavu waliokusanyika, katika hafla hiyo kwa ajili ya kuanzisha biashara ndogondogo ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya Serikali Wilayani Nyasa Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mh. Isabela Chilumba, amewashukuru kampuni ya Sigara Tanzania kwa kuwakumbuka Walemavu wa Wilaya ya Nyasa na ameomba makampuni mengine yaweze kuunga mkono na kuwasaidia makundi mbalimbali ukizingatia Wilaya ya Nyasa iko mbali kutoka makao makuu ya Nchi.

“Nichukue fursa hii, kuwashukuru kampuni ya Sigara Tanzania kwa kuwatatulia changamoto walemavu wa wilaya ya Nyasa, niseme tu wako wengi lakini kwa sasa tunashukuru kwa hawa waliopata na tunazidi kutoa wito kwa Makampuni mengine waweze kuisaidia Wilaya ya Nyasa kwa watu wenye ulemavu, ukizingatia tuko mbali na makao ya Nchi Dodoma.

Kwa upande wake Katibu wa Chama cha watu wenye Ulemavu Bw. Bonifasi Mputa amesema anaipongeza Serikali, Kampuni ya Sigara na Mbunge wa Nyasa kwa msaada huo kwa kuwa ni mara ya kwanza kwa watu wenye Ulemavu Wilaya ya Nyasa kupokea msaada huo.

 

No comments :

Post a Comment