Friday, November 13, 2020

Bodi ya Wakurugenzi Tanesco Yafika Manyara kuangalia Utekelezaji wa Agizo la Rais Magufuli

Na John Walter-Manyara 

Kufuatia agizo la Rais Dkt.John Magufuli kwa Shirika la Umeme Tanzania kuwaunganishia wananchi 4,000  Umeme katika mkoa wa Manyara, Bodi ya Wakurugenzi TANESCO ikiongozwa na Mwenyekiti wake Dkt. Alexander Kyaruzi imefika mkoani hapo kufuatilia utekelezaji wa gizo hilo.
Agosti 25,2020 Rais Dr.John Pombe Magufuli akiwa katika kampeni mjini Babati alitoa siku 30 kwa Tanesco mkoa wa Manyara kuhakikisha wananchi 4,000 ambao tayari wamtimiza vigezo vya kupatiwa huduma ya umeme wanapatiwa huduma hiyo.
Dkt. Kyaruzi amesema Kazi hiyo itafanyika  usiku na mchana ili ndani ya siku 30 watu 4,000 na ikiwezekana zaidi wawe wameunganishiwa Umeme katika nyumba zao.
Amesema Tanesco Mkoa, Kanda na Makao Makuu wameweka nguvu kubwa ili kuhakikisha agizo la Rais linatekelezwa kwa muda na ikiwezekana wamalize kabla na kuongeza wateja zaidi ya hao wanaotakiwa kupatiwa Umeme.
Ziara ya Bodi ya Wakurugenzi TANESCO ilitembelea maeneo mbalimbali ya wilaya ya Babati ambapo imeshuhudia shughuli za kuweka nguzo  ikiendelea.
Meneja wa Tanesco mkoa wa Manyara Mhandisi Rehema Mashinji amesema uongozi wa shirika umetoa msaada mkubwa katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya Umeme ambapo mpaka sasa wameshapokea vifaa mbalimbali huku nguzo zikisambazwa kwa nusu ya wateja 4000 wnaopaswa kupata Umeme kwa awamu hii.
Amewataka Wananchi wawe wavulivu wakati huu wakiendelea kusambaza miundombinu ya Umeme katika maeneo yao ili huduma iwafikie.
Ameeleza kuwa Umeme huo unaousambazwa kwa sasa katika maeneo yao  unagharamiwa na Tanesco na sio REA.
Kwa Mujibu wa Meneja wa Tanesco mkoa wa Manyara Mhandisi Rehema Mashinji Shirika katika mkoa huo linawahudumia wateja 41,500.
Mzee Emmanueli Kasmiri ameipongeza bodi ya wakurugenzi wa Tanesco  kufika mkoani Manyara na kukagua miundombinu ya Umeme kwa kuwa itaongeza kasi kwa watendaji wa shirika hilo katika kuwapatia Umeme kwa kuwa ni muda mrefu walikuwa gizani.

 

No comments :

Post a Comment