Saturday, September 5, 2020

Ujue uhusiano wa hifadhi ya jamii na sekta isiyorasmi


https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhgy_nH3Bg-CFfRR8l21UoshxQUb9SWIWQvpZdlNYkbWtvXCt0r4ii4DCKdPTCvPYffeyQ0bAv3DtkqTOaaXeDEDBmHVqB6DjFVh2ZTSRtxq9grp06Ms0UjYKeXzR0wUugq7xs5xqY2tS4/s640/2.JPG

Afisa wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Hamisi Duma akiwaeleza wadau watarajiwa kuhusu jinsi wakulima wanavyoweza kujiunga uanachama, walipotembelea banda la taasisi hiyo katika Maonesho ya Nanenane Mkoani Simiyu. (Na Mpigapicha Wetu)

Na Christian Gaya Majira Ijumaa 28 Agosti 2020

Idadi kubwa ya Watanzania mpaka sasa bado wanaamini ya kuwa, hifadhi ya jamii ni stahili ya wafanyakazi walioajiriwa pekee, tena...
wale wenye vipato vidogo.
Kabla ya kuwa na sera ya hifadhi ya jamii na kabla ya mabadiliko ya sheria za hifadhi ya jamii kuwa mifuko kamili ya hifadhi ya jamii, sheria nyingi zilikuwa haziwajumuishi wafanyakazi kutoka katika sekta isiyo rasmi sheria hizo zilizokuwa zimepitwa na wakati zilishughulika na wafanyakazi walioajiriwa na kupata mshahara kwa mwezi tu.
Na kwa ajili ya kupanua wigo zaidi wa hifadhi ya jamii na kwa kisheria ya kuwa hifadhi ya jamii ni haki ya kila mtu hivyo basi mtu yeyote aliyejiajiri, mkulima, mchimbaji madini mdogo, mfanyakazi wa ndani, pamoja na wafanya biashara wadogo wanatakiwa kujiandikisha kwa lazima au kwa hiari na kulipa kadri ya uwezo wao ili kupata mafao yote yatolewayo na mIfuko ya hifadhi ya jamii. 
Baada ya mabadiliko ya sheria ya mwaka 2018 ya mifuko ya hifadhi ya jamii, NSSF hivi sasa inahusika na sekta binafsi na sekta isiyo rasmi inayojumuisha wakulima, wavuvi, wafugaji na wajasiriamali ambao wote wanatakiwa kujiunga na shirika hilo na kuchangia kila mwezi.
Hivyo kisheria mfuko wa NSSF ndiyo mpango wa taifa wa hifadhi ya jamii kwa Tanzania Bara, unaotegemewa kushughulika na wafanyakazi wote walio katika sekta binafsi walioajiriwa na makampuni au taasisi za kitaifa na za kimataifa zisizo za kiserikali na ofisi zote za balozi zinazoajiri.
Pamoja na ZVSSS kwa upande wa Zanzibar ambao umeanzishwa na mfuko wa hifadhi ya jamii wa ZSSF kwa ajili ya kupanua wigo wa uwanachama kwa kuandikisha wananchi waliojiajiri  kwenye sekta isiyo rasmi kwa upande wa Tanzania Visiwani.
Jukumu kubwa la mifuko hii ya hifadhi ya jamii ni kuhakikisha ya kuwa inakuwa na mikakati mahususi ya kuondoa fikra ndani ya vichwa vya idadi kubwa ya watanzania kwa kuwaeleza ya kuwa hivi sasa hifadhi ya jamii haina ubaguzi wa aina yeyote, kwa sasa hifadhi ya jamii ni fursa huru kwa wote, kwa walioajiriwa na kwa wale waliojiajiri.
NSSF inatakiwa kujipanga kwa makusudi ya kuhakikisha ya inawaelemisha wananchi wote walio kwenye sekta isiyo rasmi na hata watu binafsi kuwawekea utaratibu wa wao kujiunga, kuchangia na kunufaika.
Mfuko wa NSSF unatakiwa kuonesha kwa vitendo na kwa mifano hai kutoka kwa wakulima, wanafunzi, wavuvi na wajasiriamali namna wanavyochangia na wanavyofaidika huko mijini na vijijini bila ubaguzi.
Inajulikana wazi ya kuwa watanzania wanatambua ya kuwa wengi wao wapo katika sekta ya kilimo na sekta isiyo rasmi ambao kwa vipato vyao wanavyopata wangeweza kujiunga na mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii nchini.
Uzoefu huu unashawishi ya kuwa mfuko wa NSSF sasa utazame katika sekta ya kilimo na wachimbaji wa madini nchini.
Kilimo ndio sekta mama ya uchumi wetu na mpaka sasa inaajiri zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wetu, lakini ukuaji wake ni asilimia 4.4 ambayo ni chini ya kiwango kinachotakiwa cha asilimia 6 kwa mwaka kutokana na kukosa uwekezaji wa kutosha.
Utafiti wa hivi karibuni unaonesha ya kuwa mifuko hii kwa mipango yao mbalimbali ya hifadhi ya jamii iliweza kuwafikia wakulima wapatao 29,000 na wachimbaji madini 7,000 na waliweza kujiunga na baadhi ya mifuko ya hifadhi ya jamii nchini kwa wakati huo.
Na baadhi yao mpaka sasa wanaendelea kunufaika na mafao yanayotolewa yakiwemo ya muda mrefu na ya muda mfupi ikiwemo na mikopo ya gharama nafuu kwa kupitia Benki ya Azania.
Kwa takwimu hizi za utafiti zinaonesha ya kwamba wananchi wengi wamekosa elimu ya hifadhi ya jamii na taarifa sahihi juu ya utendaji wa mifuko hii ya hifadhi ya jamii.
Ikumbukwe ya kuwa hifadhi ya jamii katika nchi hii si jambo jipya au la kigeni, hata katika jamii zetu kabla ya kuja kwa mifumo hii rasmi ya hifadhi ya jamii, kulikuwepo na utaratibu wa jamii kujiwekea mifumo ya hifadhi ya jamii isiyo rasmi na mpaka sasa inafanya kazi vizuri na kutoa huduma nzuri ya kinga ya hifadhi ya jamii. 
Katika jamii zetu kulikuwepo na utaratibu wa kuwahudumia wazee, wasiojiweza na watoto mpaka leo ndani ya makabila na familia zetu za kitanzania bado zinaendelea kutoa huduma hizi za hifadhi ya jamii ingawa kwa kiasi fulani zimeathiriwa na ujio wageni na nguvukazi kubwa kuhamia mijini kutafuta kazi za kuajiriwa.
Mtu hakupoteza heshima na thamani yake katika jamii kwa kuwa amepoteza uwezo wake wa kuchangia katika jamii, ama kwa kustaafu, kwa ajali au kwa kutojaaliwa uwezo wa kuchangia.
Mabadiliko ya kidunia yameifanya mifumo hii ya hifadhi ya jamii isiyo rasmi sasa isiweze kuhimili jukumu hilo la kutoa kinga ya hifadhi ya jamii kwa wale wazee, akina mama wajawazito, walemavu, wajane, wagane, watoto yatima, na wengineo.
Hivyo, mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii ndio mbadala na salama ya ustawi wa jamii au mtu katika dunia ya leo kuanzia tumboni mwa mama yake, utotoni, ujana, mpaka utu uzima. Utafiti unaonesha pia ya kuwa mara nyingi shida na majanga huwafika watu wakati ambao hawajajiandaa vema.
Na ikumbukwe wazi ya kuwa maandalizi ya kustaafu huaanzia pale unapoanza kufanya kazi uwe umeajiriwa au umejiajiri kwenye sekta iliyo rasmi au isiyo rasmi.
Moja kati ya changamoto kubwa iliyo mbele watu wote ni jinsi ya upatikanaji na uendelevu wa kipato cha kukidhi mahitaji ya maisha baada ya kustaafu.
Na hapa haijarishe wewe ni mtumishi wa umma, mfanyakazi uliyeajiriwa kwenye sekta rasmi au uliyejiajiri mwenyewe kwenye sekta isiyorasmi
Kustaafu kunaweza kumaanisha kuondoka katika ajira rasmi yaani kufikia tamati ya ajira yako au kufikia umri wa kustaafu kwa hiyari au kwa lazima.
Na kwa upande mwingine kustaafu ni kuondoka au kuondoshwa katika ajira hususan kwa sababu ya umri kisheria au kufikisha tamati ya mkataba wako.
Kuanza kufikiria kustaafu ni jambo la lazima kwa kila mfanyakazi uwe umejiajiri au umeajiriwa hivyo ni jambo ambalo huwezi kuliepuka hata kidogo katika maisha ya hapa duniani.
 
Mwandishi wa Makala hii ni mwanzilishi wa Kituo cha HakiPensheni, mshauri na mtaalamu wa masuala ya pensheni. Kwa maelezo zaidi: gayagmc@yahoo.com unaweza kutembelea hakipensheni website, Simu +255 655 13 13 41, info@hakipensheni.co.tz

No comments :

Post a Comment