Tuesday, September 8, 2020

Picha : BENKI YA CRDB YAENDESHA KONGAMANO KUBWA LA MAWAKALA WA CRDB... RC TELACK AWAPA TAHADHARI 'MSILIZWE'



Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack akizungumza wakati akifungua kongamano la Mawakala wa Benki ya CRDB kutoka Kanda ya Magharibi (wilaya ya Shinyanga,Kishapu na Nzega) lililolenga kujadili namna ya utoaji wa huduma za kifedha kwa njia ya kidigitali .Kushoto ni Meneja Ufanisi Biashara Upande wa Mawakala kutoka Benki ya CRDB Makao makuu,Goodluck Ruhago akifuatiwa na Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui, kulia ni Meneja wa Benki ya CRDB tawi la Shinyanga Luther Mneney.
*****

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi imeendesha Kongamano la Mawakala wa Benki ya CRDB kwa ajili ya kujadiliana kuhusu miongozo mbalimbali ya namna ya utoaji wa huduma za kifedha kwa njia ya kidigitali ili kuongeza chachu ya kuongeza ufanisi wa kazi,kuongeza umakini katika utoaji huduma za kifedha ili kukuza vipato vyao.

Kongamano hilo la Mawakala wa Benki ya CRDB likiongozwa na Kampeni ya ‘CRDB Wakala… Ulipo tupo’ limefunguliwa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack leo Jumanne Septemba 8,2020 na kuhudhuriwa na Wafanyakazi wa Benki ya CRDB na Mawakala wake takribani 300 kutoka wilaya ya Kishapu,Shinyanga na Nzega.

Akizungumza wakati wa kufungua Kongamano hilo, Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Mhe. Zainab Telack aliipongeza Benki ya CRDB kwa kuwa Benki inayoongoza kuwa na Mawakala wengi Tanzania na kuwezesha Watanzania hasa waliopo katika fursa ya kilimo kupata huduma za benki hasa maeneo ya vijijini.

“Kwenye maeneo ya kilimo haswa yale mazao makubwa ya kimkakati mawakala wamesaidia kufungua akaunti za wakulima ambao serikali inatumia kuwalipa wakulima kwa urahisi na kutokana na ukaribu wa Wakala wa CRDB wakulima wanapata huduma wakati wowote wanapohitaji kuweka na kutoa fedha,mfano wakulima wa zao la pamba na tumbaku kwa kanda hii ya Magharibi”,alisema Telack.

“Pamoja na Benki ya CRDB kupanua huduma za kibenki kupitia mawakala,tumeshuhudia kuongezeka kiwango cha ajira kwa Watanzania wengi ambapo hadi sasa huduma ya Uwakala kupitia Benki ya CRDB imeajiri takribani Watanzania 20,000 kutoka huduma ya Wakala”,alisema.

Mkuu huyo aliwataka Mawakala wa Benki kuchukua tahadhari na kujiepusha na matukio ya utakatishaji wa fedha kwa kuwa ni rahisi zaidi kwa wahalifu kujaribu kuwatumia na kujiingiza kwenye hasara ya biashara.

“Tunatambua Mawakala mnafanya kazi nzuri,mmekuwa mstari wa mbele kuwasaidia wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kukamilisha miamala popote walipo na muda wowote pasipo kuogopa hatari za biashara hiyo. Pamoja na kazi nzuri mnayoifanya,niwasihi kuchukua tahadhari kwa kufuata ushauri wa benki”,alisema Telack.

“Kuweni makini mnapofanya huduma za kifedha,usimwamini mtu yeyote.Lindeni mitaji yenu,hatutaki kusikia mnalizwa. Usimhudumie mteja bila kuhesabu fedha. Chukueni tahadhari kwani mlinzi wa kwanza wa fedha zako ni wewe mwenyewe. Pia msijiingize kwenye vitendo mikopo kinyume cha taratibu”,alisisitiza Mkuu huyo wa mkoa.

Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi Said Pamui alisema katika Kongamano hilo lilohudhuriwa pia na Maafisa wabobezi wa masuala ya fedha kutoka CRDB Makao makuu,Mawakala hao watafundiswa mbinu mbalimbali za kutambua ukatakatishaji wa fedha ili waweze kuchukua tahadhari na kujiepusha na matukio ya utakatishaji wa fedha.

Aidha Pamui alisema Mawala wa Benki ya CRDB wamekuwa sehemu ya watoa huduma za fedha nchini Tanzania hivyo wana mchango mkubwa katika kuhakikisha maendeleo ya nchi yanapaa kiuchumi hasa baada ya kufikia uchumi wa kati.

“Mawakala hawa katika utendaji wao wa kazi lazima wahakikishe hawashiriki wala kusaidia vitendo vya utakatishaji wa fedha kwani kila penye utakatishaji fedha uchumi unadumaa”,alieleza Pamui.

“Na sisi benki ya CRDB kama wawezeshaji wa Makawala wa Benki ya CRDB hatukubali kuwa sehemu ya utakatishaji wa fedha ndiyo maana tumeandaa Kongamano hili ili kuwapa mafunzo ya utoaji wa huduma za kifedha kwa njia ya kidigitali ili watoe huduma za fedha wakiwa wamebobea katika kutoa huduma za fedha kwa umahiri mkubwa”,aliongeza.

Pamui alieleza kuwa Mawakala wa Benki ya CRDB wamesaidia kuongeza muda wa utoaji huduma za kibenki kwa wananchi,ambapo wapo wanaohudumia masaa 24, 18 na hata masaa 12 ambapo ni zaidi ya masaa 8 ambayo matawi ya benki hutoa huduma.

Katika hatua nyingine  Pamui aliwataka Mawakala hao kutoa elimu kwa wateja kuhusu umuhimu wa kutunza Nywila 'Password' za akaunti zao ili kuhakikisha fedha zao zinakuwa salama.

Kwa upande wake,Meneja Ufanisi Biashara Upande wa Mawakala kutoka Benki ya CRDB Makao makuu,Goodluck Ruhago alisema mpaka sasa kuna zaidi ya Mawakala 18,000 nchini,Benki zinazotembea 15 na matawi ya Benki ya CRDB zaidi ya 250 na zaidi ya asilimia 70 ya wateja wa Benki ya CRDB wanafanya miamala kupitia kwa mawakala.

 Naye Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Shinyanga, Luther Mneney aliwakumbusha mawakala wa CRDB kuhudumia vizuri wateja.

Katika Kongamano hilo, Benki ya CRDB imetoa zawadi kwa Mawakala 10 walioongoza kwa kutoa huduma bora ambapo Mshindi wa kwanza ni Idrop (T) Ltd amepata zawadi ya cheti na shilingi 200,000/=, mshindi wa pili Juliana Sebastian Shilatu, cheti na shilingi 100,000/=, mshindi wa tatu Mathew Albert Kihama, cheti na shilingi 75,000/=, mshindi wanne Benard Joseph Lewis, cheti na shilingi 50,000/= na mshindi wa tano Zaba General Supplies amepata zawadi ya cheti na shilingi 50,000=,

No comments :

Post a Comment