Friday, May 1, 2020

KAMPUNI YA ASAS YAKABIDHI MTAMBO WA KUTAKASA MWILI MZIMA



Afisa Usalama, Afya Mazingira na Ubora wa Kampuni ya Asas Cosmas Charles(kushoto) akimkabidhi mganga mkuu wa hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Iringa, Alfred Mwakalebela mtambo wa kisasa wa kutakasa mwili kwa ajili ya hospitali hiyo.
Baadhi ya wananchi wakipita kwenye mtambo wa kisasa wa kutakasa mwili mzima kwa ajili ya kupambana na virusi vya corona uliotolewa na kampuni ya Asas ya mkoani Iringa kwa ajili ya hospitali ya rufaa ya Iringa. (picha na Denis Mlowe)
…………………………………………………………………………………..
NA DENIS MLOWE. IRINGA
KAMPUNI ya Asas imegawa msaada wa mtambo maalum wa kutakasa mwili na barakoa zaidi ya 1200 kwa ajili ya hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Iringa na hospitali za ya wilaya kwa ajili ya
kujinga na kuenea kwa Virusi Vya Corona.
Msaada huo umekabidhiwa jana kwa mganga mkuu wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa, Alfred Mwakalebela na Afisa Usalama, Afya Mazingira na Ubora wa Kampuni ya Asas Cosmas Charles  kwa niaba ya mkurugenzi wa uzalishaji wa kampuni hiyo, Ahmed Salim Abri sambamba na kutoa msaada wa ndoo maalum za kunawa mikono 80.
Akizungumza na wanahabari mara baada ya kukabidhi msaada huo, mwakilishi huyo, Cosmas Charles amesema kampuni hiyo imeamua kuunga mkono juhudi za serikali kupambana na ugonjwa wa corona ambao umekuwa tishio nchini na duniani kwa ujumla.
Alisema kuwa kampuni ya Asas mkoa wa Iringa imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia jamii hasa katika suala zima la kupambana kuenea kwa virusi vya corona mkoani hapa na kuweza kutoa misaada mbalimbali kwa jamii.
Alisema kuwa kama kampuni wameitikia maagizo ya serikali kuhusu kuzingatia masuala ya usafi katika maeneo ya kazi kama sehemu ya kupambana na tishio la maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa corona na kutoa misaada mbalimbali kwa jamii wakiwemo madereva bodaboda, umoja wa daladala kwa kuwapatia vifaa mbalimbali vya kujinga dhidi ya maambukizi ya corona.
Alisema kuwa wametoa msaada huo ambao mtambo maalum wa kutakasa mwili mzima ambao ni wa kwanza kwa hospitali za rufaa za nyanda za juu kusini na ya pili nchini kuwana na mtambo huo hali ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa jamii na wafanyakazi wa hospitali hiyo kujikinga dhidi ya maambukizi hayo.
Aidha aliongeza kuwa jamii inatakiwa kuwa na utamaduni wa kujiweka safi katika mazingira wanayoishi na hali ya hii ya kunawa mikono kwa sabuni inatakiwa kuwa utamaduni ambao unafanyika kila siku kuliko kusubiri changamoto kama hizi za gonjwa la corona.
Cosmas alisema kuwa kampuni ya Asas ni wadau wakubwa katika masuala ya afya na wadau wa maendeleo kwa ujumla hivyo msaada huo ni kuhakikisha wananchi wote wanaenda katika hospitali hiyo wanajikinga na maambukizi ya virusi vya Corona ambavyo vimekuwa vinahatarisha maisha ya binadamu kote duniani.
Kwa upande wake Mganga mkuu wa Hospitali ya Rufaa , Alfred Mwakalebela alisema kuwa msaada umekuja wakati muafaka katika mapambano dhidi ya kuenea kwa virusi vya Corona na kuwashukuru kampuni ya Asas kwa kuwa mstari wa mbele katika kusaidia sekta ya afya.
Alisema kuwa kampuni hiyo imekuwa ikisaidia maeneo mbalimbali katika hospitali hiyo ikiwemo ujenzi wa wodi ya watoto,  nyumba ya damu salama, ujenzi wa ICU ya kisasa pamoja na mashine zake ununuzi wa Xlay ya kisasa na bila kuchoka wametoa mtambo bora kabisa wa kutakasa mwili mzima.
Alisema kuwa kampuni hiyo imefanikiwa kujenga karakana ya kutengeneza viungo bandia vya miguu na mikono ambayo inatarajia kuanza kufanya kazi hivi karibuni hali ambayo imesaidia kwa kiasi kubwa kuifanya sekta ya afya kujivunia uwepo wake.
Mwakalebela alisema kuwa kampuni hiyo imefanikiwa pia kuwapatia ndoo maalum za kunawa mikono 80 ambazo watazitumia kuzigawa kwa vituo vya vya afya na hospitali za wilaya  na kuahidi kuvitumia vyema na kuwapa elimu zaidi wananchi wanaokwenda kupata huduma hospitali.
“Kwa kweli kampuni ya Asas imekuwa msaada mkubwa sana kwa wananchi mkoani Iringa na kikubwa zaidi sekta ya afya kwani wameweza kuitendea haki kwa kweli na kuwataka wadau wengine kujitoa kama ambavyo kampuni hiyo imekuwa mstari wa mbele kujitoa kwa jamii.

No comments :

Post a Comment