………………………………………………………………………………………………………..
Tunapoadhimisha kumbukumbu ya siku
ya Mwanamke Duniani hii leo Machi 8, 2020 ikiwa ni miaka 25 tangu
wanawake kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa wakutane jijini
Beijing, China kujadili maendeleo ya wanawake,Tume ya Haki za Binadamu
na Utawala Bora (THBUB) inapenda kuungana na Watanzania wote katika
kusherehekea maadhimisho haya
ambayo kimsingi yanatoa fursa kwa wanawake
kufanya marejeo ya hatua mbalimbali zilizofikiwa katika kuboresha
mustakabali wa wanawake nchini.
Tume inatambua kuwa, Tanzania
kama nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa imeridhia mikataba ya haki za
binadamu kuhusu wanawake ikiwemo makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano
wa beijing mwaka 1995.
Miongoni mwa maeneo ambayo
Serikali imeyafanyia kazi kwa ufanisi mkubwa wakati tunaadhimisha siku
ya mwanamke mwaka huu ni pamoja na usawa wa kijinsia katika kushiriki
kwenye kufanya maamuzi, upatikanaji wa huduma za afya kwa mama na mtoto,
kukemea ukatili wa kijinsia kwa mtoto wa kike na kuwajengea mifumo ya
kuwawezesha wanawake kiuchumi.
Kama kaulimbiu ya mwaka huu inavyosema “kizazi cha usawa kwa maendeleo ya Tanzania kwa sasa na baadae”.
Serikali imepiga hatua kubwa na mpaka sasa tunashuhudia kuongezeka kwa
ushiriki wa wanawake katika ngazi mbalimbali za maamuzi.
Tume inatumia fursa hii
kupongeza kwa dhati jitihada za Serikali katika kujenga mifumo sahihi
kwa mwanamke kujiletea maendeleo yake.
Aidha, katika kuyapa
kipaumbele masuala ya wanawake Tume inaendelea kutekeleza Mpango Kazi
wake wa Miaka Mitano (2018/ 2023) ambapo moja ya malengo yake ni
kuhakikisha wanawake wanaweza kufikia mifumo ya kupata haki kwa urahisi
zaidi.
Licha ya juhudi za Serikali na
Wadau za kahakikisha haki za wanawake zinapatikana kwa usawa na watu
wengine, bado kuna changamoto ya ukatili kwa wanawake na kutokuwateuwa
kwa wingi kugombea nafasi za kisiasa. Hivyo, Tume inatoa mapendekezo
kwa Serikali, Wadau na jamii kwa ujumla kama ifuatavyo;
- Tume inaiomba Serikali iendelee kuweka mazingira mazuri kwa wanawake kwa kuwaongezea nafasi zaidi katika ngazi za maamuzi ili kuweza kufikia maendeleo ya kweli ifikapo mwaka 2025.
- Tume inazishauri mamlaka za umma na binafsi kuongeza juhudi za kuelimisha jamii kuhusu kuachana na mila zote potofu dhidi ya mwanamke ili kumpa fursa nzuri ya kuweza kujiletea maendeleo yao wenyewe.
- Tume inashauri vyombo vinavyosimamia upatikanaji wa haki hususan Mahakama na jeshi la Polisi kuimarisha na kuongeza kasi ya ushughulikiaji wa mashauri yanawayohusu wanawake.
- Tume inaishauri Serikali pamoja na wadau wa haki za binadamu kupitia sheria zote zinazowagusa wanawake ikiwemo sheria za kimila kwa madhumuni ya kuzifuta, au kuzirekebisha ili ziendane na Katiba ya Nchi, Azimio la Beijing na mikataba mbalimbali ya kimataifa na ya kikanda.
Tume inawatakia Wanawake Maadhimisho mema.
Imetolewa na:
(SIGNED)
Jaji (Mst.) Mathew P. M. Mwaimu
MWENYEKITI
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Machi 8, 2020
No comments :
Post a Comment