Friday, March 6, 2020

Fahamu umuhimu wa Azimio la ILO kuhusu hifadhi ya jamii kwa wote


Matokeo ya picha ya Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar
Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar, Khamis Juma Maalim katika Mkutano Mkuu wa Tano wa Wanachama na Wadau wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ya Zanzibar (ZSSF)

Na Christian Gaya: Majira Ijumaa 06.Machi.2020

 HIFADHI ya Jamii ni haki ya msingi ya kila mwananchi awe mtu mzima au mtoto mdogo popote awapo katika ulimwengu huu. Tangazo la Umoja wa Mataifa la mwaka 1948 linasisitiza hayo. 
Utekelezaji wa agizo hilo ulitokana na...
Azimio la Shirika la Kazi Duniani nambari 102 la Hifadhi ya Jamii la mwaka 1952.
 “Hifadhi ya Jamii inaweza kutafsiriwa kwa ujumla kama ni maandalizi au kinga ya kiuchumi na kijamii dhidi ya dhiki inayosababishwa na kupoteza uwezo au kipato kutokana na umri, maradhi, kuumia, kazini au kufariki dunia,” anasema Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar, Khamis Juma Maalim alipokuwa mgeni rasmi siku ya Mkutano Mkuu wa Tano wa Wanachama na Wadau wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ya Zanzibar (ZSSF) uliofanyika Februari 26, 2020 kwenye ukumbi wa Uhuru Kariakoo Zanzibar.
 Anasema kutokana na athari kubwa ambazo mwanachama anaweza kuzipata kwa kupoteza kipato, uendeshaji wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ni jukumu la Serikali zote duniani.
“Sekta ya Hifadhi ya Jamii kwa Zanzibar inayo historia ndefu sana. Sekta hii ilikuwepo kabla ya Mapinduzi matukufu ya mwaka 1964 lakini walionufaika wakati huo walikuwa ni wachache tu wale ambao waliobahatika kufanyakazi za ukarani katika Serikali ya Kikoloni na pia kulikuwa na Hifadhi ya Jamii za kikabila au madhehebu,” Waziri anazidi anafafanua zaidi.
 Anasema tangu 1964 Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imefanya jitihada kubwa katika kuendeleza Hifadhi ya Jamii kwa wananchi wake kupitia mfuko mkuu wa Serikali. Mfumo huu ulikuwa ndiyo njia kuu ya Hifadhi ya Jamii Zanzibar mpaka mwanzoni mwa miaka ya 1990 wakati Serikali ilipoanza kupambana na hali ngumu ya uchumi. Pia ilichangiwa na ongezeko maradufu la watu kutoka 300,000 mwaka 1967 hadi 750,000 mwaka 1997.
“Ambapo Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar umeanzishwa kwa Sheria Na.2 ya mwaka 1998 ambayo ilirekebishwa na Sheria Na 9 ya mwaka 2000, pia ilirekebishwa kwa notisi ya Serikali ya 2004 na kuanzishwa upya kwa Sheria Na 2 ya mwaka 2005 baada ya kufanyiwa mapitio makubwa. Aidha kwa marekebisho ya karibuni yalikuwa ni mwaka 2016 na utekelezaji ukaanza 2017,”Waziri wa Katiba na Sheria anasema.
 Aidha anasema marekebisho yote hayo yalikuwa na dhamira mbili kuu: Kwanza ni kuendana na mahitaji ya watumiaji wa sheria kulingana na wakati husika ikizingatiwa sekta hii bado haijakomaa vizuri. Lakini pili ni kuufanya Mfuko huu kuwa na afya njema ya uendelevu wake ili wachangiaji na wasimamizi wa mfuko waweze kunufaika.
 Pia anasema matukio makubwa yaliyofanyika ni uzinduzi wa mfumo wa kujichangia katika mfumo wa hifadhi ya jamii kwa hiari kupitia Benki moja kwa moja. “Hili ni jambo jema ambalo kwa ulimwengu wa kileo mwananchi hatumii muda mwingi katika foleni au kufuatia huduma ya fedha eneo la mbali na anapoishi, bali huduma nyingi zinafanywa kupitia kiganjani au katika meza yako ya nyumbani au afisini. Naamini huduma hii itawarahisishia wanachama wengi kuweza kuwasilisha michango yao kama ambavyo tumeona,”anasema.
 “Napenda kusema kuwa moja kati ya kilio cha ulimwengu ni kwamba Mifuko ya Hifadhi ya Jamii duniani inawahifadhi wale tu walio katika sekta rasmi na inawatenga wale ambao wamo katika sekta isiyorasmi,” Waziri anasema.
 Anakumbusha ya kuwa uzinduzi wa Mfumo wa kujichangia kwa hiari (ZVSSS) uliofanyika miaka mitano iliyopita ni hatua muhimu sana ya kutekeleza kwa vitendo agizo la Shirika la Kazi Duniani-ILO linalosema “Hifadhi ya Jamii kwa wote”.
 “Kuanzishwa kwa Mfumo huu kunatoa fursa kwa wale wote ambao kwa namna moja au nyengine hawakuweza kusajiliwa katika mfumo wa sekta rasmi ili kuweza kunufaika kama wanavyonufaika wenzao katika sekta iliyo rasmi,”anasema.
 Anasema mbali na mafao ya uzeeni pia katika mfuko wa kujichangia kwa Hiari kuna fursa kwa mwanachama kunufaisha mtoto wake kwa mafao ya elimu. Mwanachama anapata fursa ya kumsajili mtoto na kumchangia mafao ya elimu kwani elimu ni hazina njema na uwekezaji mwema kwa mtoto.
 “Hivyo basi natoa wito kwa wananchi wote ambao hawakusajiliwa katika mfumo mkuu, kuitumia fursa hii ya kujisajili katika Mfumo wa kujichangia kwa hiari ili waweze kunufaika na mafao kama yale ya uzeeni ambayo wafanyakazi walioajiriwa wananufaika nayo,”waziri wa katiba na sheria anasisitiza.
 Anasema kuanzisha michuano ya soka ya ZVSSS ni jambo jema ambalo mumeamua kulitumia kama ni nyenzo ya kutafuta wanachama katika maeneo ambayo michezo inafanyika. Kwangu mie pia naangalia kwa jicho jengine ambalo bila shaka ni kuendeleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya DK. Ali Mohamed Shein ambayo imekuwa ikisisitiza suala la mazoezi na michezo kwa jumla.
 Anasema tumeona kuna jitihada ya kuanzisha viwanja vya michezo kila Wilaya, kuwepo na programu maalum ya kuhuisha michezo nchini, lakini pia hata kuwepo siku maalum kila mwaka ya kuvikutanisha vikundi vya mazoezi na wanamichezo ili kushirikiana katika mazoezi ya pamoja na kujadiliana kuendeleza sekata hiyo.
 “Hivyo basi ninawapongeza ZSSF kuanzisha michuano hiyo ikiwa ni miongoni mwa jitihada za kuunga mkono serikali yenu. Wito wangu kwenu ni kuyaendeleza michuano hiyo lakini pia kuangalia katika mikoa mengine Unguja na Pemba,” Waziri anasema. 
 “Napenda kuwakumbusha waajiri wajibu wao wa kujisajili kuwa mwanachama mchangiaji na kuwasajili wafanyakazi wao kuwa wanachama wanufaika wa ZSSF na wito huu unawahusu wenyeji na wageni,” anasema.
 Anawakumbusha waajiri wa sekta binafsi walitekeleze hilo na kuwasilisha michango kwa wakati ili walengwa wasipate usumbufu unapofika wakati wa kustaafu. Anasema jumuiya ya Waajiri Zanzibar (ZANEMA) ambao nao ni wadau wakubwa wa mkutano huu hawana budi kuwakumbusha waajiri juu ya jukumu hili la kisheria ili kujenga mustakbala mzuri baina ya waajiriwa, ZSSF na waajiri.
 “Lakini pia hata Jumuiya za Wafanyakazi kupitia vikao vyao baina ya Wafanyakazi na waajiri wao, ni wajibu kuwakumbusha kutekeleza sheria hii ya ZSSF ambayo ni miongoni mwa sheria za kazi lakini kuwapatia elimu hii ya Hifadhi ya Jamii kwa manufaa yao kwa sasa wawapo kazini na pia wakati wa kustaafu,”Waziri amesisitiza.

No comments :

Post a Comment