Mkutano wa 19 wa taasisi za fedha
nchini uliokuwa ufanyike jijini Arusha tarehe 21 na 22 Novemba 2019 sasa
utafanyika Dar es Salaam kwa tarehe hizo hizo.
Mkutano huo ambao umeandaliwa
na Benki Kuu ya Tanzania kwa kushirikiana na Umoja wa
Mabenki Tanzania
(TBA) utawakutanisha washiriki wapatao 300 ili kujadili namna ya
kuharakisha maendeleo ya ya sekta ya fedha nchini. Watakaohudhuria
mkutano huo ni pamoja an mawaziri wakiongozwa na Waziri wa Fedha na
Mipango, Dkt. Philip Mpango, wakuu wa taasisi za fedha, wachumi
wabobezi, wanataaluma na washirika mbalimbali wa maendeleo.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa
Kamati ya Maandalizi ya Mkutano huo na Mkurugenzi wa Utumishi na
Uendeshaji wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Kened Nyoni, alisema mkutano
huo utafanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es
Salaam.
Mada katika mkutano huo
zitahusu ‘Matumizi ya teknolojia katika kukuza sekta ya fedha ili kuleta
mapinduzi ya viwanda’; ‘Maeneo yenye fursa za uwekezaji katika sekta ya
fedha’, ‘Vigezo vinavyochangia kujenga tabia za ukopaji’, ‘Jinsi ya
kukinga vihatarishi katika sekta ya fedha’; ‘Namna ya kuoanisha sekta ya
fedha na maendeleo ya viwanda’; na ‘Tathmini ya mchango wa sekta ya
benki katika huduma jumuishi za kifedha nchini’.
Benki Kuu ya Tanzania imekuwa
ikiandaa mikutano ya taasisi za fedha kila baada ya miaka miwili tangu
miaka ya 1980. Katika mikutano hii, viongozi wakuu wa taasisi za fedha,
yakiwemo mabenki, mashirika ya bima, mifuko ya hifadhi za jamii na
taasisi zingine za fedha wamekuwa wakikutana na kujadili masuala
mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya fedha na uchumi wa nchi
kwa ujumla. Mkutano wa 18 wa taasisi za fedha ulifanyika mwaka 2016
jijini Arusha na mada kuu katika mkutano huo ilikuwa ni ‘Jinsi sekta ya
fedha inavyoweza kuifanya Tanzania inufaike kiuchumi kutokana na uwepo
wake kijiografia’ (Harnessing Tanzania’s Geographical Advantage: The
role of financial sector).
Imetolewa na Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki
No comments :
Post a Comment