Friday, August 23, 2019

Ijue hali halisi ya Mfuko wa hifadhi ya jamii wa PSSSF


Wanachama na wadau mbalimbali wa Mfuko wa PSSSF waliokuwa wametembelea banda la PSSSF kwenye maonesho ya 43 ya Biashara Kimataifa ya Dar es Salaam, Sabasaba Julai mwaka huu, wakipewa huduma za aina mbalimbali na wafanyakazi wa PSSSF.

Katika makala zilizopita ikumbukwe ya kuwa tuliona ya kuwa katika mkakati wa kuboresha huduma na kupunguza matumizi katika sekta ya hifadhi ya jamii nchini, Serikali iliamua kuunganisha  Mifuko minne ya PSPF, PPF, GEPF  na LAPF na kuunda Mfuko mmoja unaojulikana kama...
Mfuko wa hifadhi ya jamii kwa watumishi wa umma (PSSSF).
Hivyo basi Serikali kupitia sheria ya mfuko wa hifadhi ya jamii kwa watumishi wa umma namba 2 ya mwaka 2018 ilifuta mifuko ya hifadhi ya jamii ya PPF, PSPF, LAPF, na GEPF na kuanzisha mfuko wa hifadhi ya jamii kwa watumishi wote wa umma yaani PSSSF.
Ambapo kuanzia Agosti Mosi, 2018, waliokuwa wanachama wa mifuko iliyounganishwa yaani PPF, PSPF, LAPF, na GEPF waliohamishiwa katika mfuko wa PSSSF hivyo wataendelea kuwa wanachama na kuchangia katika mfuko wa PSSSF. Wanachama wa mfuko wa PSSSF ni pamoja wataafu na wategemezi wao waliokuwa wanalipwa pensheni na mifuko iliyounganishwa.
Na majukumu makubwa ya mfuko huu wa PSSSF ni kuandikisha wanachama, kukusanya michango, kuwekeza michango hiyo na kulipa mafao. Mafao yanayotolewa na mfuko huu wa hifadhi ya jamii yamegawanyika katika makundi mawili, makundi hayo ni mafao ya muda mrefu na mafao ya muda mfupi.
Mafao ya muda mfupi ni; fao la uzazi, fao la ugonjwa, fao la kupoteza ajira, na msaada wa mazishi. Mafao ya muda mrefu ni pensheni ya ulemavu, pensheni ya urithi pamoja na pensheni ya uzee.
Wakati huo huo mfuko unatoa msaada wa huduma ya elimu kwa watoto mpaka kumaliza elimu ya juu kwa wale ambao mzazi wao walikuwa mwanachama wa PSSSF wakati wa uhai wao.
Sheria ya mfuko wa hifadhi ya jamii PSSSF ya mwaka 2018 inatoa amana ya mkopo wa nyumba ya makazi katika kutambua umuhimu wa jambo hili kwa wastaafu wake.

Inatamka wazi ya kuwa mwanachama wa mfuko wa PSSSF anaweza kutumia sehemu ya mafao yake kama dhamana ya kupata mkopo wa nyumba ya makazi kulingana na utaratibu ulioelekezwa na mamlaka. Na kuonesha ya kuwa sheria hiyo inakwenda na wakati hasa kwa kuwajali wateja wake inasema wazi ya kuwa mwanachama anaweza kwa ruhusa ya bodi kuchukua sehemu ya michango yake kwa namna na kwa kiasi kitakachokuwa kimeainishwa kwenye Kanuni kulingana na kifungu cha 38 cha sheria ya Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA)

Kulingana na sheria ya PSSSF ya mwaka 2018 amana ya mwanachama” maana yake ni michango ya mwajiriwa, michango ya mwajiri na riba yake ambayo ipo kwenye akaunti ya mwanachama. Sheria hiyo inaruhusu wanachama wake kuingilia michango yao ya akiba ya pensheni kwa ajili ya amana ya kujipatia nyumba ya mkopo.  Mkopo huu ni kwa ajili ya kujenga nyumba ya mwanachama wa PSSSF na hutolewa kwa mwanachama aliyefikisha umri wa miaka 55 ambaye amechangia kwa muda usiopungua miezi 180.

Mpaka kufikia sasa, Mfuko wa PSSSF una jumla ya wastaafu wapatao 124,000 na wanachama 763,000 na watumishi wa PSSSF wakiwa wamejipanga kutoa huduma bora kwa wastaafu na wanachama wa mfuko huu wa PSSSF katika ofisi zote za Mfuko zilizo Tanzania bara na Visiwani  zilizofunguliwa tangu Mfuko huu uanze shughuli zake Agosti Mosi, 2018.
Thamani ya Mfuko wa pensheni kwa watumishi wa umma (PSSSF) mpaka sasa imefikia Sh. trilioni 5.8 za Kitanzania. Hivyo kuunganishwa kwa mifuko ya GEPF, LAPF, PSPF na PPF kunatoa fursa ya kuimarisha zaidi sekta ya hifadhi ya jamii hali iliyochangia thamani ya mfuko mpya wa PSSSF kuendelea kukua hata katika kipindi kifupi tangu kuanzishwa kwake.
Mfuko unahakikisha ya kuwa wastaafu wote waliohakikiwa wanalipwa mara moja ili kutekeleza dhamira ya mfuko inayohakikisha wanachama na wastaafu wake wanalipwa kwa wakati muafaka na kwa uhakika.
Zaidi ya elfu kumi ya wastaafu wameshalipwa mafao yao tangu kuanzishwa kwa mfuko huu wa PSSSF mwaka 2018 na wachache ambao hawajalipwa ni wale ambao hawajahakiki taarifa zao kwa muda uliotolewa hivyo wanatakiwa kujitokeza na kuhakikiwa ili warejeshwe katika daftari la malipo.
Baadhi ya mafao yanayoendelea kutolewa na PSSSF ni yale ya muda mfupi na muda mrefu lengo likiwa kuwawezesha wanachama wote kuishi maisha bora hata baada ya kustaafu.
PSSSF inaendelea kutoa elimu ya hifadhi ya jamii na semina ya maandalizi ya kustaafu kwa wanachama wake mahali pa kazi.

Mfuko wa PSSSF hutoa huduma ya uzazi na msaada wa mazishi bure. Kufaidika na mafao ya mazishi na uzazi hakuathiri hata kidogo michango ya mwanachama.
Wanachama wa PSSSF wataendelea kunufaika na huduma za PSSSF na hata pale inapotokea bahati mbaya mwanachama wake amefariki basi haki zake hazitapotea na zinalindwa kwa mujibu wa sheria ili ziwanufaishe warithi wake.
Mfuko wa PSSSF umejenga mifumo bora ya teknolojia ya habari na mawasiliano inayounganisha ofisi zote na makao makuu ya mfuko ili kuimarisha huduma na tija kwa wanachama.
Wanachama wa PSSSF wanayo fursa ya kupata taarifa za michango yao katika ofisi zote za PSSSF nchi nzima pamoja na kupitia simu za mkononi.
Wanachama wanaweza kuwasiliana na Mfuko ili kupata ufafanuzi wa masuala yao, maswali au malalamiko kwa kupiga simu kupitia namba 0800 110 055, 0800 780 060 na 0800 110 040, namba hizi ni bure. Pia wanaweza kutuma ujumbe mfupi kwa namba 0735 117 773 na 0736 117 773
Wanachama wa PSSSF wanaweza kufungua madai yao katika katika ofisi yeyote ya PSSSF iliyoko karibu nao, zilizosambaa karibu mikoa yote 29 na wilaya zote za Tanzania bara na Zanzibar visiwani ili kuongeza ufanisi na kusogeza huduma karibu na wanachama na wadau wake.
Mfuko wa PSSSF ni matokeo ya kuunganishwa kwa mifuko ya PSPF, LAPF, GEPF na PPF ili kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na hasa kuchochea ukuaji wa sekta ya hifadhi ya jamii hapa nchini.
Mpaka sasa Mfuko umeshatumia zaidi ya trilioni moja kulipa mafao kwa wanachama wake hali inayoonesha kuwa mfuko upo katika hali nzuri kiafya, hivyo mfuko wa PSSSF umejipanga ya kuwa unahakikisha unawahudumia wanachama na wadau wake vizuri kwa mujibu wa sheria na kanuni za hifadhi ya jamii.

No comments :

Post a Comment