Monday, April 1, 2019

WAZIRI WA MADINI UGANDA, ATEMBELEA TANZANIA


PICHA NA 1
Kutoka kushoto, Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella wakimsubiri Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris pamoja na ujumbe wake kabla ya kuwasili kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza tarehe 01 Aprili, 2019.
PICHA NA 2
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella (kushoto mbele) akiwaongoza Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo, Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris pamoja na ujumbe wake kwenye ukumbi wa mikutano.
PICHA NA 3
Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris (wa pili kushoto) akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella
PICHA NA 4
Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo, akielezea mafanikio ya nchi ya Tanzania kwenye usimamizi wa sekta ya madini kwa ujumbe wa Uganda.
PICHA NA 5
Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris akifafanua jambo kwenye mkutano huo.
PICHA NA 6
Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo pamoja na Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris (waliosimama katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe kutoka nchini Uganda na Tanzania.
………………
Greyson Mwase na Remija Salvatory, Mwanza
Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris pamoja na ujumbe wake wameanza ziara nchini Tanzania leo tarehe 01 Aprili, 2019 yenye lengo la kujifunza namna sekta ya madini nchini Tanzania inavyoendeshwa. Waziri Lokeris ameongozana na maafisa waandamizi kutoka
Serikali ya Uganda pamoja na wawakilishi wa wachimbaji wadogo. Waziri wa Madini Nchini Uganda pamoja na ujumbe wake walipokelewa na Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella.
Akizungumzia lengo la ziara hiyo kupitia mahojiano maalum aliyoyafanya na vyombo vya habari, mara baada ya kupokelewa na Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo, Waziri Lokeris alisema kuwa lengo la ziara yake ni kujifunza sheria na kanuni za madini nchini Tanzania zinavyosimamiwa vyema pamoja na uendeshaji wa shughuli za uchimbaji wa madini nchini Tanzania kwa vitendo kupitia wawekezaji waliowekeza nchini pamoja na wachimbaji wa wadogo wa madini.
“Tulifanya utafiti na kubaini Tanzania ni  nchi yenye utajiri mkubwa wa madini na uzoefu mkubwa kwenye uchimbaji wa madini na tumeona wachimbaji wadogo wakisaidiwa sana na Serikali ya Tanzania,” Alisema Lokeris.
Aliongeza kuwa,  kati ya maeneo wanayotarajia kujifunza ni pamoja na ushirikishwaji wa wazawa kwenye  shughuli za uchimbaji wa madini (local content) utoaji wa huduma kwa jamii inayozunguka shughuli za uchimbaji wa madini (corporate social responsibility), usimamizi wa sheria ya madini pamoja na kanuni zake.
Aliongeza kuwa ushirikiano wa Tanzania na Uganda umekuwa ni wa muda mrefu na kusisitiza kuwa Serikali ya Uganda ipo tayari kujifunza na kubadilishana uzoefu kwenye usimamizi wa sekta ya madini.
Aliendelea kusema kuwa, Serikali ya Tanzania inapenda kuona wananchi wake hususan waishio vijijini wananufaika na sekta ya madini kupitia uboreshwaji wa huduma za jamii kama vile elimu huduma za afya, na ili kuhakikisha wananchi wake wananufaika, Serikali imeamua kutuma wataalam wake Tanzania kujifunza kutokana na hatua kubwa iliyopigwa na nchi ya Tanzania kwenye usimamizi wa sekta ya madini.
Akielezea changamoto kwenye usimamizi wa sekta ya madini kwa nchi ya Uganda, Waziri Lokeris alieleza kuwa ni pamoja na kutokuwa na teknolojia ya kutosha kwenye uongezaji thamani wa madini pamoja na utoroshwaji wa madini unaofanywa na wachimbaji wadogo.
Wakati huohuo Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo alisema kuwa nchi ya Tanzania ipo tayari kutoa uzoefu wake kwenye usimamizi wa sekta ya madini kwa nchi ya Uganda kupitia wataalam wake.
Alisema katika ziara ya ujumbe huo, mbali na nchi ya Tanzania kutoa uzoefu wake kwenye usimamizi wa sekta ya madini nchini, wanatarajia kuupeleka ujumbe huo kwenye soko la madini mkoani Geita lililozinduliwa hivi karibuni na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kasim Majaliwa pamoja na baadhi ya mitambo ya kuchenjulia dhahabu.
Akielezea mikakati ya Serikali ya Tanzania kwenye usimamizi wa sekta ya madini, Naibu Waziri Nyongo alieleza kuwa ni pamoja na uboreshaji wa sheria ya madini pamoja na kanuni zake ikiwa ni pamoja na uwezeshaji wa wachimbaji wadogo wa madini.
Alieleza  mikakati mingine kuwa  ni pamoja na uanzishwaji wa masoko ya madini katika kila mkoa ili kudhibiti  utoroshwaji wa madini nchini.

No comments :

Post a Comment