Tuesday, April 23, 2019

Rais Tshesekedi na Kabila wakutana kujadili uteuzi wa Waziri Mkuu


Wananchi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wanaendelea kusubiri kwa hamu na shauku kubwa uteuzi wa Waziri Mkuu mpya, miezi kadhaa baada ya Felix Tshisekedi kuchukua mikoba ya Joseph kabila kwenye uongozi wa nchi. Wawili hao walikutana na kuzungumzia kuhusu nafasi ya Waziri Mkuu ambayo imesalia wazi, miezi minne baada ya uchaguzi wa urais uliompa ushindi Felix Tshisekedi na kuchukua hatamu ya uongozi wa nchi.
Awali Tshisekedi na mtangulizi wake Joseph Kabila walikuwa hawaelewani kufuatia mvutano wa kisiasa uliokuwa ukiikumba DRC na kisha baada ya uchaguzi wa urais wawili hao waliamua kufanya kazi kwa ushirikiano wakiwa katika muungano mmoja wa kisiasa.
Rais Tshisekedi na Joseph Kabila walikuwa hawajakutana kwa wiki kadhaa kutokana na ziara za kikazi za Tshisekedi. Lakini kwa pande zote mbili, wanahakikisha kuwa rais wa sasa na mtangulizi wake huzungumza mara kwa mara.
Mazungumzo kati ya wawili hao kuhusu uteuzi wa Waziri Mkuu na uundwaji wa serikali yalidumu kwa muda wa saa moja.
Kuhusu suala la Waziri Mkuu, mazungumzo yanaendelea, karibu miezi minne baada ya Felix Tshisekedi kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Wawili hao walikuwa wamechagua timu za mazungumzo, lakini mazungumzo yao yaliambulia patupu. Mazungumzo hayo sasa kuhusu uteuzi wa mtu atakayeshika wadhifa wa Waziri Mkuu yanafanyika katika ngazi ya juu.

No comments :

Post a Comment