Wednesday, January 30, 2019

CHUO CHA BANDARI KUDAHILI WANAFUNZI KIDIJITALI


images
Na.Bushiri Matenda- MAELEZO
Chuo cha Bandari kilichopo Temeke Jijini Dar es Salaam kinatarajia kuanza udahili wa wanafunzi wapya kupitia mfumo wake mpya wa kidijitali ujulikanao kama Student’s Information Management System (SIMS).
Mfumo huo wa kidijitali uliozinduliwa jana tarehe 29-01-2019 na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaac Kamwelwe, utakiwezesha chuo hicho kudahili wanafunzi wengi kwa wakati mmoja lakini pia kutarahisisha kazi ya udahili tofauti na awali ilivyokuwa
ikifanyika.
Mfumo huo ambao ulibuniwa na kutengenezwa na wafanyakazi wa TPA kitengo cha TEHAMA, pia utatumika kukokotoa matokeo ya mitihani na kuanda taarifa ya mwisho wa mwaka wa mafunzo yaani ‘final year transcript’.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa tovuti ya mfumo huo mpya, Waziri Kamwelwe alisema uwepo wa mfumo huo utasaidia kudhibiti udanganyifu uliokuwa ukifanywa na baadhi ya watendaji wasiokuwa waaminifu.
Mhandisi Kamwelwe ameongeza kwamba awali wakati udahili ulipokuwa ukifanywa kwa kujaza fomu kwa mkono ‘manual’, kulikuwa na tatizo la uchakachuaji wa vyeti na upotevu wa pesa.
“Wakati wa application za manual (kujisajili kupitia mikono) kuna fomu za maombi zilikuwa zinapotea na kulikuwa na upotevu wa pesa pamoja na tatizo la kuchapisha vyeti feki na baadhi ya wanafunzi kutohudhuria mafunzo ipasavyo,” alisema Waziri Kamwelwe.
Mhandisi Kamwelwe ameongeza kwamba kipindi hicho kuna baadhi ya wanafunzi waliishia kusajiliwa tu na baada ya miaka miwili unamkuta mtaani na cheti lakini kwa uwepo wa mfumo, hayo mambo hakuna tena.
Kwa upande wake Mkuu wa Bodi ya Magavana ya Chuo hicho, Mhandisi Deusdedit Kakoko alimshukuru Waziri kwa kutenga muda na kuja kuwazindulia tovuti hiyo ambayo ni muhimu mno kwa chuo hicho.
Mhandisi Kakoko ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa TPA amesema  uwepo wa mfumo huo, utarahisisha utendaji kazi wa chuo na kudhibiti wale wote waliokuwa wakitumia mianya ya kutokuwepo kwa mifumo hiyo, kufanya udanganyifu.
Aidha faida nyingine za mfumo huo ni kumwezesha mwanafunzi kuweza kujisajili popote pale alipo ilimradi tu pawe na mtandao wa intaneti, pia taarifa zote za wanafunzi wa chuo hicho zitapatikana kidijitali kupitia mfumo huo.
Mbali na hayo, pia mfumo huo utatumika kuzalisha taarifa ya mwisho ya matokeo ‘final year transcript’, na utawezesha kuoana kwa mifumo ya ndani na nje ya taasisi kama vile NACTE, NECTA na GePG.

No comments :

Post a Comment