Baadhi ya wafanyakazi wa kujitolea
wa Kimarekani wakila kiapo mbele ya Kaimu Balozi wa Marekani nchini,
Dk. Inmi Patterson (hayupo pichani) wakati wa hafla ya kuapishwa
iliyofanyika Jumatano hii, Korogwe, Tanga. Wafanyakazi wa kujitolea wa
Kimarekani wa Peace Corps wapatao 59 watahudumu nchini Tanzania kwa
miaka miwili katika sekta ya
Elimu. Wafanyakazi hawa watapangiwa kufanya
kazi katika wilaya 35 nchini kote Tanzania. Hafla hiyo ilihudhuriwa na
mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William
Ole Nasha. (Picha kwa Hisani ya Ubalozi wa Marekani).
Shirika la Wafanyakazi wa Kujitolea wa Kimarekani la Peace Corps lawaapisha Wafanyakazi wa Kujitolea 59 wa sekta ya Elimu
Korogwe, TANZANIA. Tarehe 19
Septemba 2018, Kaimu Balozi wa Marekani nchini Dk. Inmi Patterson
aliongoza hafla ya kuapishwa kwa wafanyakazi wa kujitolea wa Kimarekani
wa Peace Corps wapatao 59 watakaohudumu nchini Tanzania kwa miaka miwili
katika sekta ya Elimu. Wafanyakazi hawa watapangiwa kufanyakazi katika
wilaya 35 nchini kote Tanzania.
Dk. Patterson aliongoza kiapo
rasmi cha wafanyakazi hao wapya wa kujitolea mbele ya mgeni rasmi, Naibu
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.William Tate Olenasha.
Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na viongozi wa serikali, wafanyakazi wa
kujitolea wa zamani wa Peace Corps, wawakilishi wa taasisi wabia na
wanafamilia wa familia za Kitanzania ambazo wafanyakazi hawa wa
kujitolewa waliishi nazo.
Kaimu Balozi Patterson aliwaeleza
wafanyakazi wapya wa kujitolea kuwa: “Wakati ambapo ninyi mnaweza kuwa
Wamarekani wa kwanza kukutana na kufanya kazi na wafanyakazi wenzenu na
majirani zenu wa Kitanzania, ni dhahiri kwamba katika mawazo yao
mtaendelea kuwa wawakilishi wa watu wa Marekani na ubia wa muda mrefu
kati ya Wamarekani na Watanzania.”
Peace Corps ni taasisi ya Serikali
ya Marekani iliyoanzishwa na Rais John F. Kennedy mwaka 1961 ambayo
hivi sasa inahudumia zaidi ya wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya 7,000
katika zaidi ya nchi 70 duniani. Kwa zaidi ya miaka 50, Peace Corps
imekuwa taasisi inayoendesha shughuli za mabadilishano ya kiufundi na
kitamaduni zisizoegemea mrengo wowote wa kisiasa na kidini. Peace Corps
ina dhamira ya kukuza amani na urafiki duniani kwa kutekeleza malengo
matatu yafuatayo:
- Kutoa wafanyakazi wa kujitolea wa Kimarekani watakaochangia kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika nchi itakayohitaji wafanyakazi hao:
- Kukuza uelewa kuhusu Wamarekani miongoni mwa watu katika jamii zinazohudumiwa na Wafanyakazi wa kujitolea;
- Kuimarisha uelewa wa Wamarekani kuhusu dunia na watu wake.
Zaidi ya wafanyakazi wa kujitolewa
wa Peace Corps 3000 wamehudumu nchini Tanzania toka mwaka 1961. Peace
Corps hutoa wafanyakazi wa kujitolea wa Kimarekani wenye utaalamu katika
nyanja mbalimbali ambao hupangiwa kufanyakazi katika jamii wakifundisha
katika shule za sekondari (hisabati, sayansi na Kiingereza), wakitoa
elimu ya afya na utunzaji wa mazingira.
No comments :
Post a Comment