Thursday, September 27, 2018

NYONGO AUTAKA MGODI WA GEITA KUWALIPA FIDIA WANANCHI

M51

Na Rhoda James, Geita
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ameutaka Mgodi wa Geita Gold Mine Ltd kuwalipa fidia wananchi waliopata madhara ya nyufa katika katika nyumba zao kutokana na
shughuli za uchimbaji wa madini wa kampuni hiyo.
Naibu Waziri Nyongo aliyasema hayo tarehe 26 Septemba, 2018 wakati alipofungua Maonesho ya Kwanza ya Teknolojia ya Uchimbaji na Uwekezaji wa Madini ya Dhahabu mkoani Geita kwa niaba ya Waziri wa Madini, Angellah Kairuki.
Alitoa rai kwa Wachimbaji wadogo wa madini kote nchini kushiriki maonesho hayo yanayoendelea mkoani humo kwa kuwa yatawanufaisha kwa kupata fursa ya kujifunza kuhusu teknolojia mbalimbali na namna bora ya uchimbaji, uchenjuaji, ikiwemo kupata elimu ya kulinda mazingira na kuzalisha kwa tija.
Pia, aliwataka Wakuu wa mikoa yote nchini pamoja na Wakuu wa wilaya zote kujifunza kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Geita, Gabriel Luhumbi ili kuhakikisha kuwa wananchi wao wanafaidika na rasilimali pamoja na mazao yanayolimwa katika maeneo yao.
“Mkifanya maonesho ya aina hii katika mikoa yenu kulingana na mazao au rasilimali mlizonazo katika mikoa yenu wananchi wenu watafaidika,” alisema Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo.
Vilevile, Naibu Waziri Nyongo, aliwataka wananchi wa   mkoa wa Geita na Kagera pamoja na wadau wa madini ya dhahabu kujipanga ili kuhakikisha kuwa maonesho hayo yanafanyika kila mwaka.
Pia, Naibu Waziri Nyongo alisema kuwa, Wizara ya Madini itaendelea kushirikiana na uongozi kutoka Mkoa wa Geita kuhakikisha kuwa wanayatangaza maonesho hayo kwa kiasi kikubwa ili yaweze kufahamika duniani kote hatimaye wadau wa madini waweze  washiriki kwa wingi.

No comments :

Post a Comment