Friday, September 28, 2018

MAKAMU WA RAIS AZITAKA TAASISI ZA UMMA KUUNGANA KUDHIBITI VIUMBE WAGENI/VAMIZI


samia2
Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan 
Na Mwandishi Wetu,
MAELEZO
DAR ES SALAAM
28.9.2018

MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan amezitaka Wizara, Wakala, Idara, Taasisi za Serikali zinazohusika na sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, maliasili na utalii na Serikali za Mitaa kuandaa mipango na mikakati  ya pamoja ili kupunguzia gharama kwa Serikali katika
kukabiliana na changamoto ya kuenea kwa viumbe wageni/vamizi nchini.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kikosi kazi kutoka Taasisi za Umma watakaojikita katika kutatua changamoto za viumbe wageni/vamizi leo Jijini Dar es Salaam, Mhe. Samia alisema wakati umefika kwa Wataalamu wa Wizara, taasisi, wakala za Serikali kufanya kazi kwa pamoja ili kuweza kudhibiti athari za viumbe wageni/wamizi ambao wameanza kuleta athari za kijamii na kiuchumi nchini.
Makamu wa Rais alisema kwa mujibu wa Taasisi ya Global Invasive Species Database, Tanzania ina takriban aina 100 za viumbe Vamizi/Wageni wakiwemo wadudu wa magonjwa ya mimea, wadudu, magugu ya kwenye maji na magugu ya nchi kavu, wanyama na miti.
Mhe. Samia alisema  Sekta na Taasisi zote hazina budi kufanya kazi kwa pamoja kwa kupeana taarifa na mikakati ya kukabiliana na changamoto zilizopo pamoja na ushirikishwaji wa wadau wote zikiwemo Halmashauri, Asasi za Serikali na zisizo za Serikali, Sekta binafsi na wananchi ili kuwa na uelewa wa pamoja wa kutafuta ufumbuzi.
“Zamani ulikuwa unakuta Taasisi Fulani inaandika mradi wa mazingira mfano magugu maji, fedha wanazoomba wanatumia wao, na wengine pia wanatekeleza mradi huohuo, umefika wakati sasa kwa taasisi hizi kufanya kazi pamoja ili kuipunguzia gharama Serikali” alisema Samia.
Aidha Samia alisema uharibifu wa makazi ya viumbe asili ndio chimbuko la uwepo wa Viumbe Wageni/Vamizi ambapo shughuli za kibinadamu zinatajwa kuwa ndiyo sababu kuu ya uharibifu/ubadilishaji wa makazi asili ya viumbe.
Anaongeza kuwa katika mkataba wa Kimataifa wa Bioanuai ambao Tanzania imeuridhia, unataja kuwa viumbe wageni/vamizi ni sababu ya pili inayosababisha uharibifu wa makazi ya viumbe asili na hata kusababisha kutoweka kwa viumbe hao wa asili.

Akifafanua zaidi alisema kuenea kwa viumbe hao wameleta na wanaendelea kuleta madhara makubwa katika mazingira hususan kuharibika kwa mifumo ikolojia, upotevu wa bioanuai, na baadhi ya viumbe hao ni sumu hivyo huleta madhara ikiwemo vifo.
Kwa mujibu wa Samia alisema viumbe hao pia wamesababisha baadhi ya wanyama ambao walikuwa kivutio kwenye mbuga za wanyama kuhama kwenye maeneo yao ya asili jambo linalosababisha wanyama hao kutoonwa tena na watalii, ambapo baadhi yao huingia kwenye maeneo ya makazi ya watu na hivyo kuuliwa kirahisi.
“Kwa mfano, nimejulishwa kuwa katika Hifadhi ya Ngorongoro, takribani theluthi moja ya eneo la shimo ambapo ndipo wanyama wanapata malisho yao, limevamiwa na viumbe hawa na linaendelea kuvamiwa” anasema Samia.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba alisema Serikali imeipatia hadidu rejea nane kikosi kazi hicho ili kuweza kubaini ukubwa, athari na changamoto za viumbe hao ambao tayari wameanza kuleta athari za kijamii na kiuchumi katika maeneo mbalimbali nchini.
“Nilifanya ziara katika hifadhi ya Bonde la Ngorongoro na nilibaini kupungua kwa wanyama katika hifadhi hiyo pamoja na kumea kwa majani kwa ajili ya malisho ya wanyama nilielezwa na wataalamu kuwa majani hayo ni mimea vamizi ambayo ni sumu kwa wanyamapori, hivyo kikosi kazi hiki tumewapa maelekezo ya kuja na majibu kuhusu suala hili”.
Waziri Makamba alisema mbali na athari zilizoanza kujitokeza katika hifadhi ya Bonde la Ngorongoro, maeneo mengine yaliyoanza kuathiriwa na viumbe wageni/vamizi hao ni pamoja na Ziwa Jipe lililopo Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara na pamoja jamii ya mimea ya maua yaliyoanza kuota katika maeneo ya Kibaigwa Mkoani Dodoma.
Naye Waziri wa Kilimo, Dkt. Charles Tizeba aliwataka wajumbe wa kikosi kazi hicho kutambua kuwa suala la mazingira ni la usalama wa taifa, hivyo ni wajibu wao kufanya kazi kwa uadilifu na kuleta majawabu yatayoweza kutatua changamoto hiyo katika miaka mingi zaidi.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Prof. Dos Santos Silayo alisema mtawanyiko wa viumbe wageni/vamizi wanasambishwa zaidi na shughuli za kibinadamu na mabadiliko ya tabia nchi ambapo mifano michache iliyopo Tanzania kwa sasa ni pamoja na uwepo wa magugu maji, mti wa mrashia na upandikazaji wa mazao ya mimea na mifugo.

No comments :

Post a Comment